Hamia kwenye habari

MACHI 28, 2018
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mashahidi wa Yehova Waonyesha Umoja Ulimwenguni Pote Wakati wa Kampeni ya Kuandika Barua za Kutuma Urusi

Mashahidi wa Yehova Waonyesha Umoja Ulimwenguni Pote Wakati wa Kampeni ya Kuandika Barua za Kutuma Urusi

Jumanne, Machi 21, 2017, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova liliwaomba ndugu na dada ulimwenguni pote waandike barua za kuwasihi wenye mamlaka wa serikali wenye cheo cha juu zaidi waliokuwa wakitishia kupiga marufuku utendaji wetu katika eneo lote la Shirikisho la Urusi. Ingawa hatuwezi kujua kihususa ni barua ngapi zilizowafikia wenye mamlaka nchini Urusi, baadhi ya wale walioandika walipokea barua rasmi kwamba barua yao ilipokewa. Ingawa serikali ya Urusi iliamua kutosikiliza maombi hayo yenye heshima na ikatumia mamlaka yake vibaya kushambulia ibada ya ndugu zetu, kampeni hiyo ilikuwa wonyesho wenye kustaajabisha wa umoja wa ulimwenguni pote wa tengenezo la Yehova. Pia, kampeni hiyo ilifanikiwa kutuma ujumbe kwa waabudu wenzetu nchini Urusi kwamba ushirika mzima wa ndugu zetu wako tayari kuwategemeza.—1 Petro 2:17.

Msichana mdogo nchini Bolivia akishiriki katika kampeni.

Mashahidi wengi walijitahidi juu chini kushiriki katika kampeni hiyo. Katika nchi fulani, ni gharama kubwa kutuma barua nchini Urusi, kwa hiyo wenye uwezo walitoa michango kwa ukarimu ili wale wasio na uwezo mkubwa waweze kushiriki. Katika visa fulani wahubiri walituma barua kupitia rafiki zao walio katika nchi nyingine ambako gharama za usafirishaji si za juu sana. Ndugu na dada wengi walikutana pamoja kama familia au makutaniko ili kuandika barua zao pamoja na kuzituma pamoja. Kwa njia hiyo, mbali tu na kuokoa pesa za kutuma barua, kampeni hiyo pia ilikuwa tukio la kiroho litakalokumbukwa kwa muda mrefu.

Kuna ripoti za wafanyakazi wa posta ambao walisaidia katika kampeni hiyo. Kwa mfano, meneja wa huduma za kusafirisha vifurushi huko Barranquilla, Kolombia, alisema hivi: “Nilishangazwa na umoja wa ulimwenguni pote uliopo kati yenu, na kwamba mmeungana kwa ajili ya jambo jema kama hili linalotukia Urusi. Akilini mwangu ninawazia kwamba jambo hili linalotukia hapa Barranquilla linaendelea pia katika majiji yote ulimwenguni. Ujumbe huu utakuwa mkubwa, wa kimataifa, nami natumai kishindo chake kitasikika.” Huko Anseong, Korea Kusini, msimamizi wa shirika la posta alifungua kaunta ya pekee kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova ili watume barua zao na hata akawaandalia bahasha ya pekee inayoweza kutumwa nje ya nchi, bila malipo.

Ndugu na dada nchini Guinea wakiwa wamekutana kuandika barua.

Yaroslav Sivulskiy, msemaji wa Mashahidi wa Yehova, anaeleza hivi: “Akina ndugu nchini Urusi waliposikia kwamba Baraza Linaloongoza lilikuwa limeanzisha kampeni ya ulimwenguni pote ya kuandika barua kwa ajili yao, walijua kwamba hata uamuzi uweje, hawako peke yao katika imani.”

Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, anasema hivi: “Kampeni hii ya kuandika barua ilionyesha kwamba sasa zaidi ya wakati mwingine wowote, Mashahidi wa Yehova wana umoja. Kadiri tunavyosonga karibu zaidi na mwisho wa mfumo huu, ndivyo umoja wetu utakavyokuwa muhimu kwa ajili ya wokovu. Tunaposubiri kuona jinsi Yehova atakavyoshughulikia mambo nchini Urusi, tutatumia nafasi zote zinazojitokeza kuwasaidia ndugu zetu. Pia, tutaendelea kumtolea Yehova dua kwa umoja, tukiwa na uhakika kwamba Mungu wetu atawatunza katika kila njia.”—Zaburi 65:2.

Austria

Bolivia

Bosnia na Herzegovina

Denmark

Ekuado

Ujerumani

Ghana

Guatemala

Indonesia

Japani

Nepal

Rumania

Rwanda

Slovakia

Hispania

Sri Lanka

Uswisi

Tanzania

Zambia