Hamia kwenye habari

MACHI 20, 2014
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Guy H. Pierce, Mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, Amekufa

Guy H. Pierce, Mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, Amekufa

NEW YORK—Guy H. Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova katika makao yao makuu ya ulimwenguni pote huko Brooklyn, New York, alikufa Jumanne, Machi 18. Alikuwa na umri wa miaka 79.

Bw. Pierce alitumikia katika halmashauri kadhaa zinazosimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuwafundisha watu Biblia ulimwenguni pote. Majukumu yake katika tengenezo yalimfanya asafiri sana, naye alitumia fursa hizo kuwatia moyo Mashahidi wenzake kotekote duniani. Licha ya majukumu mengi aliyokuwa nayo, Bw. Pierce alijulikana vyema kama mtu ambaye aliwasikiliza kwa makini wale waliohitaji msaada au ushauri fulani, na alikuwa na tabasamu na ucheshi uliowastarehesha wengine. Wale waliomjua vizuri walimtambua kama mtu ambaye aliwavutia watu wa malezi na tamaduni tofauti-tofauti. Katika hotuba moja aliyotoa kwenye programu ya kuhitimu ya wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, Bw. Pierce alisema maneno haya ambayo yeye mwenyewe aliyafuata: ‘Uwe imara kuhusiana na kanuni zinazofaa, lakini badilikana kulingana na hali. Usiwadharau watu wa nchi ambayo unatumikia kwa sababu utamaduni wao ni tofauti.’

Guy Hollis Pierce alizaliwa Auburn, California, Novemba 6, 1934. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova Agosti 14, 1955, akiwa na umri wa miaka 20. Alifunga ndoa na Shahidi mwenzake, Penelope (Penny) Wong, Mei 30, 1977, na wakapata watoto pamoja. Bw. na Bi. Pierce waliamua kuwa walimu wa Biblia wa wakati wote (wanaoitwa na Mashahidi mapainia wa kawaida). Baadaye, alikuwa mtumishi anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova, akitembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kotekote nchini Marekani, ili kuwatia moyo kiroho wahudumu wenzake katika makutaniko hayo. Mwaka wa 1997, Bw. na Bi. Pierce walialikwa kufanya kazi ya wakati wote katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Marekani. Oktoba 2, 1999, Bw. Pierce alitangazwa kuwa mshiriki mpya wa Baraza Linaloongoza.

Bw. Pierce alikuwa mwenyekiti kwenye mkutano wa 129 wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Mkutano huo ulifanywa mwisho-juma wa Oktoba tarehe 5 na 6, 2013. Watu 1,413,676 kutoka nchi 31 walihudhuria mkutano huo, baadhi yao walikuwepo kibinafsi kwenye jumba ambalo mkutano huo ulifanyiwa na wengine waliunganishwa kupitia Intaneti. Kulingana na habari za tovuti rasmi ya Mashahidi, huo ndio uliokuwa mkutano wenye hudhurio kubwa zaidi kuliko mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova.

Mbali na mke wake, Penny, Bw. Pierce ameacha watoto sita, wajukuu kadhaa pamoja na vitukuu. Atakumbukwa sana na Mashahidi wa Yehova kote duniani ambao aliwaona kama familia.

Katika taarifa, washiriki wenzake wa Baraza Linaloongoza walisema kuhusu “imani yake dhabiti na msimamo wake imara kwa ajili ya sheria na kanuni za Yehova,” wakiongezea kusema: “Maisha yake ya uhodari na uaminifu alipokuwa duniani yataendelea kutuimarisha kadiri miaka inavyopita.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000