Hamia kwenye habari

MEI 15, 2014
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mashahidi wa Yehova Watangaza Makusanyiko ya Kimataifa

Mashahidi wa Yehova Watangaza Makusanyiko ya Kimataifa

NEW YORK—Mashahidi wa Yehova wametangaza kwamba watakuwa na makusanyiko ya kimataifa ya siku tatu katika majiji mbalimbali ulimwenguni pote kuanzia Juni 2014 na kuendelea hadi Januari 2015. Makusanyiko hayo yataanza kufanywa Marekani na kisha nchini Australia, Ekuado, Korea Kusini, Mexico, Ugiriki, Uingereza, Ujerumani na Zimbabwe. Matukio hayo ya kimataifa yatafanyika sambamba na makusanyiko madogo ya eneo ambayo Mashahidi hupanga kila mwaka.

Makusanyiko ya kimataifa yataanza Juni 6, 2014, katika uwanja wa Ford Field, Detroit, Michigan, Marekani. Watu 45,500 hivi wanatarajiwa kuhudhuria tukio hilo, kutia ndani wajumbe 2,500 kutoka nchi nyingine.

Wajumbe kutoka nchi mbalimbali na pia wamishonari watahudhuria makusanyiko hayo ya kimataifa. J. R. Brown, msemaji wa Mashahidi wa Yehova katika makao yao makuu ya ulimwenguni pote jijini Brooklyn, New York, anasema: “Makusanyiko yetu ya kimataifa ni matukio yenye kusisimua sana na ni nyakati za kusherehekea. Tunaamini kwamba watu watafurahia sana kuhudhuria makusanyiko hayo pamoja na familia na rafiki zetu, ambayo yatakuwa na programu za pekee sana.”

Kichwa cha makusanyiko hayo ni “Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu!” Bw. Brown anaeleza kuwa “programu itakazia kichwa kikuu cha Biblia na mafundisho mawili ya msingi ya Mashahidi wa Yehova: kwamba Ufalme wa Mungu ulisimamishwa mwaka wa 1914 na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa Ufalme huo. Kwa kweli, makusanyiko hayo yanaadhimisha miaka 100 ya Ufalme wa Mungu.”

Mashahidi wanajitayarisha kwa ajili ya kampeni ya ulimwenguni pote ya kuwaalika jirani zao wahudhurie kusanyiko linalofanywa katika eneo lao. Kama ilivyo katika mikutano yote ya Mashahidi, hakutakuwa na kiingilio wala sadaka hazitakusanywa.

Habari kuhusu tarehe na mahali hususa patakapofanyiwa Makusanyiko ya mwaka wa 2014 ya “Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu!” zinapatikana katika tovuti yetu rasmi ya Mashahidi wa Yehova, jw.org. Waandishi wa habari wanaweza kuwasiliana na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ili wapate jina la mtu anayewasiliana na waandishi wa habari na pia habari nyingine zinazohusu makusanyiko hayo.

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000