Hamia kwenye habari

MEI 4, 2016
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mashahidi Wakazia Ushikamanifu Katika Kusanyiko la Eneo la 2016

Mashahidi Wakazia Ushikamanifu Katika Kusanyiko la Eneo la 2016

NEW YORK—Mashahidi wa Yehova wanawakaribisha watu wahudhurie Kusanyiko la Eneo la 2016 lenye kichwa “Dumisha Ushikamanifu kwa Yehova!” Kuanzia Ijumaa, Mei 20, kusanyiko hilo litaanza kufanywa bila malipo katika maeneo mbalimbali ya Marekani na duniani pote.

Programu hiyo ya siku tatu itakuwa na hotuba 49 na kila moja itakazia “ushikamanifu.” Isitoshe, Mashahidi wametayarisha video fupi 35 kwa ajili ya kusanyiko na sinema mbili ambazo zitaonyeshwa siku ya Jumamosi na Jumapili. Kila siku, kipindi cha asubuhi na cha mchana kitaanza kwa video ya muziki uliorekodiwa kwa ajili ya kusanyiko hilo.

Kama ilivyokuwa katika makusanyiko mengine yaliyopita, Mashahidi watasambaza mialiko ya kuwakaribisha watu wahudhurie programu hiyo. Tarehe na mahali pa kila kusanyiko inapatikana katika tovuti rasmi ya Mashahidi, jw.org. Waandishi wa habari pamoja na watangazaji ambao wangependa kutangaza programu hiyo wanaweza kuwasiliana na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyo karibu ili kupata habari zaidi.

David A. Semonian, msemaji wa Mashahidi wa Yehova kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote, Brooklyn, New York, alisema hivi: “Tunaamini kwamba ushikamanifu ni sifa muhimu katika kujenga uhusiano mzuri na wengine. Kusanyiko la mwaka huu linakazia mambo ambayo yatawasaidia watu wasitawishe uhusiano mzuri na marafiki, familia, na zaidi ya yote na Mungu. Tunatumaini kwamba wote watakaohudhuria watafurahia programu hii.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000