Hamia kwenye habari

MACHI 13, 2014
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mashahidi wa Yehova Watoa Chapa Kubwa ya Biblia Iliyorekebishwa Karibuni

Mashahidi wa Yehova Watoa Chapa Kubwa ya Biblia Iliyorekebishwa Karibuni

NEW YORK—Katika jitihada zao za kuhakikisha kwamba watu wengi zaidi wanaweza kuipata Biblia, Mashahidi wa Yehova wanatoa chapa kubwa ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa. Wamepanga kuchapisha kwanza nakala 424,000 za toleo hilo la Biblia. Kazi ya kuchapisha Biblia hizo inafanywa nchini Marekani na Japani.

Mashahidi walitoa chapa ya kawaida ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa katika mkutano wa pekee uliofanyika Oktoba 5-6, 2013 ambapo watu kutoka nchi 31 waliunganishwa kusikiliza mkutano huo. Toleo hilo la mwaka wa 2013 ndilo la karibuni zaidi kufanyiwa marekebisho makubwa ya tafsiri hiyo tangu mwaka 1984. Halafu Oktoba 7, 2013, Mashahidi waliweka Biblia hiyo katika programu inayoitwa Maktaba ya JW (JW Library), ambayo imeshapakuliwa mara milioni 1.4 hivi. Biblia iliyorekebishwa ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika mifumo mbalimbali ya kielektroniki kwenye www.pr418.com.

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa ina marejeo ya pambizoni 60,000 hivi yanayowasaidia wasomaji kuelewa muktadha wa masimulizi ya Biblia. Pia, Biblia hiyo ina michoro yenye rangi, ramani za maeneo ya nyakati za Biblia, na chati zinazoonyesha habari za maisha ya kila siku katika nyakati za Biblia. Nyongeza ya Biblia hiyo inatoa ufafanuzi wa habari mbalimbali kama vile kanuni za kutafsiri Biblia na historia ya jinsi Biblia ilivyoandikwa na kuhifadhiwa.

Jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika toleo la mwaka wa 1984 la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata hivyo, toleo lililorekebishwa la mwaka wa 2013 linatia ndani pia utafiti wa karibuni zaidi kuhusu sehemu ambazo jina la Mungu linapatikana katika hati za zamani zaidi. Kutokana na uchunguzi zaidi uliofanywa katika Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi na hati nyingine za kale, jina la Mungu limeongezwa katika sehemu nyingine sita katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa. Jina la Mungu limeongezwa kwenye Waamuzi 19:18; 1 Samweli 2:25; 6:3; 10:26; 23:14; 23:16. Nyongeza nyingine inaeleza zaidi kuhusu matumizi ya jina la Mungu katika Kiebrania na Kigiriki cha kale, na pia ina orodha ya lahaja na lugha kadhaa za kisasa zilizo na jina la Mungu katika tafsiri zao za Biblia.

Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakichapisha, wakisambaza, na kutafsiri Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ambayo inaheshimiwa sana na wasomi kwa sababu ya usahihi wake. Biblia kamili ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa kwa mara ya kwanza katika Kiingereza mwaka wa 1961. Katika mwaka wa 1963, gazeti The New York Times liliripoti kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ingepatikana katika lugha nyingine sita, kama ilivyotangazwa katika kusanyiko la Mashahidi lililofanyika Yankee Stadium. Tangu wakati huo, Mashahidi wametoa Biblia hiyo katika lugha zaidi ya 120. Katika miaka ya karibuni, Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mpya iliamua kurekebisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ili kwenda sambamba na mabadiliko katika lugha za kisasa na pia kufafanua misemo fulani ya Biblia ili wasomaji waelewe na kusoma kwa urahisi zaidi. Maendeleo hayo katika kazi ya kutafsiri Biblia yanaonekana wazi katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa.

“Zaidi ya miaka 50 iliyopita, tulisisimuka sana kupata yale matoleo ya kwanza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, lakini inasisimua hata zaidi kupata toleo lililorekebishwa karibuni zaidi,” anasema J. R. Brown, msemaji wa Mashahidi wa Yehova. “Lengo letu ni kwamba watu wote waelewe Maandiko Matakatifu kwa kutumia lugha ambayo ni sahihi, yenye kuheshimika, na ya kisasa.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000