Hamia kwenye habari

Kushoto kwenda kulia: Ndugu Aleksey Budenchuk, Aleksey Miretskiy, Feliks Makhammadiyev, Gennadiy German, na Roman Gridasov

FEBRUARI 24, 2020
URUSI

Akina Ndugu Wawasaidia Waabudu Wenzao Waliopigwa Gerezani Nchini Urusi

Akina Ndugu Wawasaidia Waabudu Wenzao Waliopigwa Gerezani Nchini Urusi

Kufuatia ripoti ya ndugu watano ambao walipigwa vibaya sana wakiwa gerezani huko Orenburg, Urusi, akina ndugu katika mji huo walienda katika gereza hilo haraka iwezekanavyo ili kutoa msaada. Ndugu hao waliofungwa, Aleksey Budenchuk, Gennadiy German, Roman Gridasov, Feliks Makhammadiyev, na Aleksey Miretskiy wanatokea mji wa Saratov, ambao uko umbali wa zaidi ya kilomita 800 kutoka Orenburg.

Ndugu Feliks Makhammadiyev akitabasamu, wiki mbili baada ya kupigwa vibaya sana wa walinzi wa gereza, na akiwa amevaa koti ili kufunika majeraha yake

Februari 15, 2020, ripoti za taarifa za mtandaoni zilionyesha kwamba walinzi wa gereza la Penal Colony No. 1 la Orenburg, walitumia marungu kuwapiga ndugu watano kutoka Saratov. Baada ya kusoma ripoti hizo, kikundi cha akina ndugu na dada kutoka Orenburg walisafiri kwenda kwenye gereza hilo. Kwa ujasiri, walijitambulisha kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova, na kuhatarisha uhuru wao pia. Akina ndugu katika kikundi hicho waliwaomba maofisa wa zamu wawaambie kuhusu maendeleo ya ndugu hao watano waliopigwa. Kwa kuwa ripoti zilionyesha kuwa Ndugu Makhammadiyev alikuwa na majeraha makubwa zaidi na alilazwa hospitali, akina ndugu hao wa Orenburg walitaka wahakikishiwe ikiwa alikuwa hai au la. Walizungumza na maofisa hao kwa muda wa saa mbili.

Pia akina ndugu wa Orenburg walichagua kikundi cha akina ndugu ambao wataendelea kutoa msaada kwa ndugu walio gerezani pamoja na wake zao, wakishirikiana na mawakili wa ndugu hao. Mara kwa mara ndugu na dada wa Orenburg huwaandikia barua za kuwatia moyo akina ndugu walio katika gereza la penal colony na hata wamechangia pesa za kusaidia kuwanunulia vyakula vyenye afya zaidi ambavyo havipatikani gerezani.

Roho ya upendo na ya kujitoa iliyoonyeshwa na ndugu na dada zetu imetoa ushahidi mkubwa kwa wafanyakazi katika gereza la penal colony. Wafanyakazi hao wanajionea jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyowajali sana waabudu wenzao—hata wale wanaotokea mamia ya kilomita na ambao hawajawahi kukutana nao.

Inatia moyo kusikia ripoti za ndugu zetu wanaofuata ushauri wa Biblia unaopatikana katika andiko la Waebrania 13:3: “Wakumbukeni wale walio gerezani, kana kwamba mmefungwa pamoja nao, na wale wanaoteswa, kwa kuwa ninyi pia mko katika mwili.”