Hamia kwenye habari

Dada Larisa Artamonova

FEBRUARI 15, 2021
URUSI

Dada Larisa Artamonova Ahukumiwa kwa Sababu ya Imani Yake

Dada Larisa Artamonova Ahukumiwa kwa Sababu ya Imani Yake

Hukumu

Februari 12, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilitoa uamuzi wake katika kesi inayomhusu Dada Larisa Artamonova. Ingawa angeweza kufungwa miaka sita gerezani, mahakama iliamua kumtoza faini ya rubo 10,000 (dola 135 za Marekani).

Maelezo Mafupi Kumhusu

Larisa Artamonova

  • Alizaliwa: 1970 (Birobidzhan, Eneo Lililotengewa Wayahudi)

  • Maisha Yake: Baba yake aliuawa alipokuwa na umri wa miaka mitatu. Amefanya kazi ya kuoka, kuchora kwa kutumia kompyuta, na kushona. Aliolewa mnamo 1990. Ana mwana mmoja anayeitwa Yevgeniy, ambaye ana ugonjwa usio wa kawaida. Dada Larisa ana ugonjwa wa hitilafu ya mfumo wa kinga unaoathiri viungo vyake. Bado anaendelea na utendaji licha ya afya yake. Anafurahia kuendesha baiskeli, kuteleza kwenye barafu, na kuchora picha

    Maswali kuhusu ukosefu wa haki, huzuni, na uovu yalimfanya aanze kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alipata majibu yanayoridhisha katika Maandiko na akabatizwa katika mwaka wa 1995

Historia ya Kesi

Septemba 25, 2019, wenye mamlaka nchini Urusi walifungua kesi ya uhalifu dhidi ya Dada Larisa Artamonova. Mwana wake ameshtakiwa katika kesi tofauti. Wao ni miongoni mwa Mashahidi 22 katika Eneo Lililotengewa Wayahudi wanaoshtakiwa kushiriki katika utendaji wa shirika lenye “msimamo mkali.”

Mama yake na baba yake wa kambo wameshangaa kwamba karibu Larisa apewe hukumu ya miaka sita gerezani kwa sababu ya imani yake ya kidini—hukumu inayolingana na ile aliyopewa mwanamume aliyemuua baba yake.

Muda mfupi kabla ya mateso hayo kuanza katika eneo la Birobidzhan, Larisa na mwana wake walikuwa ameanza kuongeza sana utumishi wao kwa Yehova. Anasema hivi: “Kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova na kuimarisha hali yako ya kiroho na ile ya familia yako kunakusaidia kuepuka kuwa na woga.” Anaongezea hivi: “Shetani anajaribu kuwatumia wale wanaotutesa ili kuingiza akilini mwetu wazo la kwamba utendaji wetu wa Kikristo unahatarisha uhuru wetu. Tofauti na hilo, Yehova anatuhakikishia kwamba uhuru wetu unategemea kufanya kile ambacho sikuzote ametufundisha tufanye.”

Ndugu na dada 22 walioshtakiwa katika eneo la Birobidzhan, wanahakikishiwa kwamba Yehova anapendezwa na uaminifu wao na kwa kweli wanampa Yehova jibu la kumpa Shetani anayemdhihaki.—Methali 27:11.