Hamia kwenye habari

Kuanzia kushoto kwenda kulia: Dada Nataliya Sorokina na Mariya Troshina

FEBRUARI 17, 2021
URUSI

Dada Wawili Nchini Urusi Wanaweza Kufungwa Gerezani Baada ya Kukaa Mahabusu na Kifungo cha Nyumbani kwa Mwaka Mmoja Hivi

Dada Wawili Nchini Urusi Wanaweza Kufungwa Gerezani Baada ya Kukaa Mahabusu na Kifungo cha Nyumbani kwa Mwaka Mmoja Hivi

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Imekataa Ombi la Rufaa

Septemba 15, 2021, Mahakama ya Eneo la Smolensk ilikataa maombi ya rufaa ya Dada Sorokina na Dada Troshina. Hukumu zao za awali zitaendelea kutumika. Hawahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Aprili 22, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Sychyovskiy katika Eneo la Smolensk iliwahukumu Dada Nataliya Sorokina na Mariya Troshina kifungo cha nje cha miaka sita.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Nataliya Sorokina

  • Alizaliwa: 1975 (Dresden, Ujerumani)

  • Maisha Yake: Kutoka Ujerumani alihamia Saint Petersburg kisha akahamia Sychyovka katika Eneo la Smolensk. Anafanya kazi akiwa muuguzi. Anapenda kutengeneza vitu kwa mikono na kujifunza lugha mbalimbali ili awahubiri watu wengi zaidi. Alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alifurahia mambo aliyojifunza kuhusu uumbaji na tumaini la wakati ujao. Hilo lilichochea upendezi wake kufuatia mambo ya kiroho. Alibatizwa mnamo Agosti 1994

Mariya Troshina

  • Alizaliwa: 1977 (Saint Petersburg)

  • Maisha Yake: Tangu utotoni alipenda kujifunza kuhusu historia. Amefanya kazi ya kuwatembeza wageni. Anapenda kujifunza lugha nyingine ili awahubirie watu wengi zaidi.

    Alianza kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Alipendezwa na jinsi Biblia ilivyo sahihi kihistoria na kisayansi. Alijiweka wakfu kwa Yehova Mungu mnamo Julai 1991. Mama yake, ambaye tayari amekufa, alijifunza pia na kubatizwa

Historia ya Kesi

Oktoba 7, 2018, maofisa wa Idara ya Usalama wa Kitaifa (FSB) na polisi wa eneo lao walivamia nyumba nne huko Sychyovka. Maofisa wa FSB walichukua vitu vya kibinafsi vya ndugu na dada 17 kutia ndani vya watoto. Dada Nataliya Sorokina na Dada Mariya Troshina walikamatwa na kuwekwa katika sehemu ya kuwazuilia watu kwa muda.

Kuhusu upekuzi huo wa nyumba, Mariya anasema kwamba kusoma masimulizi ya maisha ya Mashahidi wengine waliokamatwa kwa sababu ya imani kulimsaidia ajitayarishe. Anasema hivi: “Nilijihisi nikiwa mtulivu siku walipopekua nyumba yangu na kunikamata. Sikudhani ningekuwa na amani kadiri hiyo moyoni. Hilo liliwezekana kwa sababu tu ya roho ya Mungu.”

Siku mbili baada ya uvamizi huo, Mahakama ya Wilaya ya Leninskiy ya jiji la Smolensk iliagiza kwamba dada zetu wawekwe mahabusu, ambako walikaa kwa siku 191. Kisha wakapewa kifungo cha nyumbani kwa zaidi ya miezi sita.

Dada wote wawili wanasema kwamba kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova kabla ya kesi hizo kuliwasaidia sana. Nataliya anasema ni muhimu kuwa na mtazamo wa kiroho. Anasema unapokabili mateso, ni muhimu kukumbuka chanzo chake kikuu. Anasema hivi: “Sikuzote Shetani ndiye chanzo cha mateso yanayowapata watu wa Mungu, na kila mmoja wetu anahusika katika suala muhimu.”

Mariya anaongezea hivi: “Uhusiano na Yehova unajengwa siku baada ya nyingine, kwa hiyo ni muhimu kuuona mkono wa Yehova na kutambua njia mbalimbali anazotumia kututunza. Jifunze kumtegemea katika kila jambo. Sitawisha upendezi wa kusoma Biblia kila siku, na ujaribu kukumbuka mfuatano wa matukio na andiko unalopenda zaidi.”

Imani na uvumilivu ambao dada zetu wameonyesha ni mfano bora sana kwetu sote wanapoendelea ‘kumtumaini Yehova ambaye ndiye msaada wao na ngao yao.’—Zaburi 115:11.