Hamia kwenye habari

MEI 25, 2020
URUSI

Dennis Christensen, Sasa Amefungwa Nchini Urusi kwa Miaka Mitatu, Bado Ni Imara na Mwenye Shangwe

Dennis Christensen, Sasa Amefungwa Nchini Urusi kwa Miaka Mitatu, Bado Ni Imara na Mwenye Shangwe

Kufikia leo, Ndugu Dennis Christensen amevumilia kifungo kisicho cha haki kwa miaka mitatu nchini Urusi. Tangu alipokamatwa Mei 25, 2017, baadhi ya rafiki zake wamemuuliza Ndugu Christensen imani yake imeathiriwaje na hali hiyo ngumu. Jibu lake ni lilelile: “Imani yangu imeimarika zaidi.”

Ndugu Christensen anaeleza hivi: “Nimejionea ukweli wa maneno ya kitabu cha Biblia cha Yakobo sura ya 1, mstari wa 2 na 3: ‘Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapopata majaribu mbalimbali, mkijua kwamba sifa iliyojaribiwa ya imani yenu hutokeza uvumilivu.’”

Inapendeza kwamba imani na shangwe ya Ndugu Christensen imeongezeka licha ya hali ngumu na zenye kuvunja moyo.

Ndugu Christensen alipokamatwa, aliwekwa mahabusu katika gereza lililo karibu na nyumbani kwake huko Oryol. Baada ya muda, mke wake, Irina aliruhusiwa kumtembelea. Ndugu Christensen aliendelea kukaa mahabusu kwa miaka miwili hivi. Mnamo Februari 2019, Ndugu Christensen alihukumiwa kifungo cha miaka sita gerezani. Miezi mitatu baadaye, ombi lake la kukata rufaa lilikataliwa. Alihamishwa katika gereza lililo umbali wa kilomita 200 kutoka Oryol, na hivyo kumfanya awe mbali zaidi na Irina.

Kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa, Ndugu Christensen amestahili kujaza ombi la kuachiliwa mapema. Maombi matatu kati ya manne yamekataliwa. Licha ya mambo hayo yanayoweza kumfanya avunjike moyo, Ndugu Christensen anaendelea kuwa imara.

Kwa unyenyekevu Ndugu Christensen anasema hivi: “Mimi na Irina si wakamilifu, lakini tumejifunza kuvumilia na kuendelea kuwa na shangwe licha ya majaribu. Na jambo muhimu zaidi ni kwamba tumemkaribia Mungu wetu ambaye pia ni Baba yetu, Yehova.”

Tunasali na tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwasaidia ndugu na dada zetu nchini Urusi waendelee kuvumilia mateso kwa shangwe.—Mathayo 5:11, 12.