Hamia kwenye habari

Dada Svetlana Monis akiwa na mume wake, Alam Aliyev

FEBRUARI 3, 2021
URUSI

HABARI ZA KARIBUNI—DADA AHUKUMIWA | Dada Svetlana Monis Adumisha Mtazamo Mzuri Licha ya Kukabili Mashtaka ya Uhalifu kwa Sababu ya Imani Yake

HABARI ZA KARIBUNI—DADA AHUKUMIWA | Dada Svetlana Monis Adumisha Mtazamo Mzuri Licha ya Kukabili Mashtaka ya Uhalifu kwa Sababu ya Imani Yake

Oktoba 31, 2022, Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilimhukumu Dada Svetlana Monis kifungo cha nje cha miaka miwili na nusu. Hahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Machi 9, 2022, Mahakama ya Eneo Lililotengewa Wayahudi ilibadili hukumu ya Svetlana. Kesi yake ilipelekwa kwenye Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ili isikilizwe tena.

Februari 15, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilimhukumu Svetlana kwa sababu ya kushiriki utendaji wa shirika lililopigwa marufuku. Mahakama hiyo ilimtoza faini ya rubo 10,000 (dola 135 za Marekani).

Maelezo Mafupi Kumhusu

Svetlana Monis

  • Alizaliwa: 1977 (Lesozavodsk)

  • Maisha Yake: Ana ugonjwa wa macho unaoendelea kumwathiri. Anapenda kujifunza lugha mbalimbali. Alijifunza Kichina, Kiingereza, na Kijerumani. Amemlea mwana wake akiwa peke yake. Ameitegemeza familia yake kwa kufungua mkahawa mdogo wa chakula cha Kichina.

    Alianza kujifunza Biblia baada ya kuona ukosefu mwingi wa haki duniani. Alibatizwa mwaka 2005. Mwaka 2015, alifunga ndoa na Alam Aliyev ambaye pia anakabili kesi ya uhalifu.

Historia ya Kesi

Septemba 26, 2019, Luteni D. Yankin, mpelelezi mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) alifungua kesi ya uhalifu dhidi ya Dada Svetlana Monis. Mahakama ilimpiga marufuku kutumia gari lake kwa miezi miwili licha ya kwamba alihitaji kulitumia ili kumsaidia nyanya yake mwenye umri wa miaka 91.

Uchunguzi wa kwanza uliisha Desemba 2019. Baadaye, wakuu waliwasilisha kesi yake kwenye Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan.

Svetlana anasema hivi anapofikiria mateso anayokabili: “Nilikuwa mtulivu walipofanya msako. Wakati huo, kwa mara ya kwanza nilielewa maneno: ‘Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu.’”​—Mathayo 5:10.

Baada ya msako huo, mume wa Svetlana, yaani Alam, aliwekwa kizuizini kwa siku nane. Svetlana anasema hivi: Ilikuwa vigumu sana kwangu kutokuwa na wasiwasi mwingi kumhusu mume wangu. Nilikuwa na wasiwasi kwa sababu hali ya ugonjwa wake mbaya wa uti wa mgongo ilizidi kuwa mbaya, alikuwa ametibiwa hospitalini . . . juma moja tu kabla ya msako huo. Na hakukuwa na njia yoyote ya kuwasiliana na Alam, sikuweza kujua ikiwa alikuwa sawa. Nilimwambia Yehova hisia zangu, na kwamba nilimkabidhi mahangaiko yangu yote yeye na nilikuwa nina uhakika angemtunza Alam kwa njia bora zaidi.”

Svetlana hajawahi kutilia shaka kwamba Yehova yuko pamoja naye. Anasema hivi: “Niliona jinsi alivyonitegemeza. Nilielewa kwamba haukuwa wakati wa kuanza kuogopa. . . . Nilijaribu kutojifikiria mwenyewe. Badala yake, nilijaribu kufikiria jinsi ya kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova.”

Ili kudumisha mtazamo mzuri, Svetlana na Alam walikuwa na bidii ya kuimarisha imani yao. “Kila siku, mimi na mume wangu tulisoma andiko la siku pamoja na sura moja ya Biblia. Kwa kawaida, tunakazia fikira Maandiko yanayotutia moyo tutafute faraja kutoka kwa Yehova na tumtegemee yeye.” Andiko la mwaka 2019 la Isaya 41:10 linalosema: ‘Usiogope, kwa maana mimi ni Mungu wako’ linawakumbusha na kuwapa uhakika Svetlana na Alam kuhusu upendo wa Yehova. Svetlana anasema hivi: “Tuliamua kuchapisha andiko hilo na kuliweka ukutani.”

Uvumilivu wa Svetlana umefanya watu wake wa ukoo wabadili maoni yao kuhusu Mashahidi. Svetlana anasema hivi: “Nimeweza kumhubiria mama yangu, ambaye alinipinga wakati fulani. Sasa anaheshimu maamuzi yetu na anatuonyesha hisia mwenzi na kutuunga mkono. Nyanya yangu mwenye umri wa miaka 91, ambaye ni mshiriki wa dini ya Othodoksi, amekuwa akituonyesha hisia-mwenzi na kutuhangaikia. Ameanza kupendezwa kwa njia ya pekee na Biblia.”

Tunaendelea kuwakumbuka Svetlana na Alam. Tunajua kwamba wataendelea kuwa na mtazamo mzuri Yehova anapoendelea ‘kuimarisha mioyo yao.’​—Zaburi 10:17.