Hamia kwenye habari

Dada Tatyana Sholner

JUNI 21, 2021
URUSI

HABARI ZA KARIBUNI | Dada Tatyana Sholner Amtegemea Yehova na Kuwa na Shangwe Licha ya Majaribu

HABARI ZA KARIBUNI | Dada Tatyana Sholner Amtegemea Yehova na Kuwa na Shangwe Licha ya Majaribu

Septemba 14, 2022, Mahakama ya Tisa ya Kuchunguza Maamuzi ya Mahakama za Chini ilikataa ombi la pili la rufaa la Dada Tatyana Sholner. Hahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Desemba 16, 2021, Mahakama iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilikataa ombi la rufaa la Tatyana.

Juni 25, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilimhukumu Dada Tatyana Sholner kifungo cha nje cha miezi 30. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Tatyana Sholner

  • Alizaliwa: 1993 (Birobidzhan)

  • Maisha Yake: Baba yake alikufa ghafla alipokuwa mtoto, hivyo mama yake alimlea yeye na kaka yake. Anafanya kazi kwenye duka la dawa. Anapenda kuteleza kwenye barafu, kuendesha baiskeli na kucheza mpira wa wavu

    Alianza kupendezwa na ujumbe wa Biblia alipokuwa akijifunza kushona katika shule ya ufundi. Alivutiwa na mwanafunzi mwenzake ambaye ni Shahidi wa Yehova. Alifarijiwa na tumaini la ufufuo binamu yake mwenye umri wa miaka 12 alipokufa katika mwaka wa 2014. Alibatizwa 2017

Historia ya Kesi

Februari 6, 2020, wenye mamlaka katika Birobidzhan, nchini Urusi, walifungua kesi za uhalifu dhidi ya dada Wakristo sita, na Tatyana alikuwa miongoni mwao. Wameshtakiwa kwa kosa la kuwa na “msimamo mkali” kwa sababu tu ya kutenda kulingana na imani yao. Jumla ya kesi 19 dhidi wa Mashahidi wa Yehova zimefunguliwa katika Eneo Lililotengewa Wayahudi.

Tatyana ana uhakika kwamba Yehova anamsaidia kuvumilia anapoendelea kukabiliana na mashtaka haya. Anasema hivi: “Matatizo haya yalipoanza, ratiba yangu ya kiroho iliathiriwa kwa muda mfupi, lakini sikusahau kusoma Biblia kamwe. Nilimwambia Yehova kuhusu wasiwasi wangu wote na jinsi nilivyohisi. Nilisali na kumwomba Yehova roho yake takatifu ili niweze kuvumilia na kubaki mwaminifu kwake hadi mwisho. Na nilimwomba aniimarishe, anipe ujasiri na hekima ili niweze kutetea jina la Mungu bila woga mahakamani.”

Kisha akasema: “Kujua kwamba Yehova huwategemeza, huwasaidia na kuwalinda watumishi wake siku zote kunanisaidia kubaki nikiwa na shangwe. Anaushika mkono wangu kwa mkono wake wa kuume wenye nguvu. Hili hunisaidia nimtumaini kikamili na kubaki mtulivu ninapoendelea kukabiliana na majaribu.”

Tunapoendelea kusubiri matokeo ya kesi hii, tuna uhakika kwamba Tatyana ataendelea ‘kuvumilia chini ya dhiki’ kwa msaada wa Yehova.​—Waroma 12:12.