Hamia kwenye habari

Kuanzia kushoto kwenda kulia: Ndugu Dmitriy Malevaniy, Dada Olga Opaleva, Dada Olga Panyuta, na Ndugu Aleksey Trofimov

JUNI 29, 2021 | HABARI ZILIONGEZWA: FEBRUARI 13, 2023
URUSI

HABARI ZA KARIBUNI—HUKUMU ZA GEREZA | Mashahidi Wapata Shangwe na Nguvu Chini ya Majaribu

HABARI ZA KARIBUNI—HUKUMU ZA GEREZA | Mashahidi Wapata Shangwe na Nguvu Chini ya Majaribu

Februari 10, 2023, Mahakama ya Wilaya ya Spassk iliyo katika Eneo la Primorsky iliwahukumu Ndugu Dmitriy Malevaniy, Dada Olga Opaleva, Dada Olga Panyuta, na Ndugu Aleksey Trofimov. Ndugu Malevaniy alihukumiwa kifungo cha miaka saba gerezani. Ndugu Trofimov alihukumiwa kifungo cha miaka sita na miezi sita gerezani. Dada Panyuta alihukumiwa kifungo cha miaka minne gerezani. Wote watatu walipelekwa kizuizini moja kwa moja kutoka mahakamani. Dada Opaleva alihukumiwa kifungo cha nje cha miaka minne na miezi sita. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Dmitriy Malevaniy

  • Alizaliwa: 1990 (Spassk-Dalny)

  • Maisha Yake: Anafundisha jinsi ya kutengeneza programu za kompyuta. Naye mke wake, Ulyana, ni msanii. Alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova alipokuwa tineja. Alisadiki kwamba Biblia inategemeka na kwamba kuishi kulingana na kanuni za Biblia kunatusaidia kuwa na maisha mazuri zaidi. Alibatizwa mwaka wa 2004

Olga Opaleva

  • Alizaliwa: 1952 (Spassk-Dalny)

  • Maisha Yake: Alipokuwa kijana alimwamini Mungu lakini hakupendezwa na Biblia. Alikutana na Mashahidi wa Yehova muda mfupi baada ya kifo cha binti yake aliyekuwa na umri wa miaka 22. Alifurahi kujifunza kuhusu tumaini la ufufuo lililo katika Biblia. Kadiri imani yake ilivyoongezeka alianza kushiriki tumaini hilo na wengine. Alibatizwa mwaka wa 1995. Anapenda muziki na kuimba tangu akiwa mtoto. Anapenda hasa kuimba nyimbo za Ufalme

Olga Panyuta

  • Alizaliwa: 1959 (Nizhny Novgorod)

  • Maisha Yake: Kabla ya kustaafu alikuwa mwalimu wa chekechea na pia aliajiriwa na serikali ili kusaidia watu wenye mahitaji mbalimbali katika jamii. Aliolewa na Vladimir mwaka wa 1982. Wana mabinti wawili na mwana mmoja na wote ni watu wazima sasa. Alijifunza na Mashahidi wa Yehova na akavutiwa na ujumbe wa Biblia uliokuwa wazi na unaoeleweka. Alibatizwa mwaka 1996

Aleksey Trofimov

  • Alizaliwa: 1959 (Mamakan, Irkutsk Region)

  • Maisha Yake: Alikutana na Tamara alipokuwa chuoni na kumwoa. Wana watoto wanne na wajukuu kadhaa. Amefanya kazi ya kutengeneza makufuli na hivi karibuni amekuwa akisimamia chumba chenye mashine na vifaa vya kudhibiti joto katika jengo. Aliamua kumtumikia Yehova katika miaka ya 1990 baada ya kujifunza kwamba Neno la Mungu linafundisha jinsi ya kuwa na maisha yenye maana zaidi. Alibatizwa mwaka 1996

Historia ya Kesi

Novemba 25, 2018, polisi walivamia nyumba nne za Mashahidi katika mji wa Spassk-Dalny. Polisi walitumia msumeno unaotumia umeme ili kukata mlango wa nyumba ya Dada Olga Opaleva. Walipoingia walimuuliza kwa nini hakufungua mlango. Alishindwa kujieleza kwa ufasaha. Polisi hao waliita gari la kubebea wagonjwa na ikabainika kwamba alikuwa amepata kiharusi. Baadaye siku hiyo, polisi hao walimtoa hospitalini na kumpeleka kituoni ili kumhoji. Kwa sababu ya kiharusi hicho Olga hawezi kutumia mkono na mguu wake wa kuume kikamili. Mwana wake, Ndugu Vitaliy Ilinykh, ambaye humtunza amehukumiwa katika kesi tofauti.

Ndugu na dada hao wanne waliwekwa kizuizini kwa siku mbili. Novemba 27, 2018, waliachiliwa na kufungwa kifungo cha nyumbani. Baada ya mwaka mmoja, vizuizi vyao vilipunguzwa.

Wanashtakiwa kwa kupanga na kujihusisha na shirika “lenye msimamo mkali.”

Watu wa familia na marafiki wao, kutia ndani wasio Mashahidi wamesema kwamba hawaelewi ni kwa nini wananchi wanaopenda amani wanaadhibiwa kwa sababu ya imani yao. Katika kisa cha Dmitriy, hata wafanyakazi wenzake ambao hawashiriki maoni yake ya kidini wanamuunga mkono na kumhimizi asife moyo.

Dmitriy anatambua kwamba shangwe aliyo nayo wakati anapokabiliana na mateso ni ishara inayoonyesha kwamba Yehova yuko pamoja naye. Anasema kwamba: “Kama vile fimbo ya Musa ilivyoonyesha kwamba Yehova alikuwa pamoja naye, basi shangwe yangu inaonyesha pia kwamba Yehova yuko pamoja nami.” Anaongezea kwa kusema shangwe yake “itatoa ushahidi mkubwa kwa wote wale wanaofanya kazi mahakamani na wanaofanya uchunguzi wa kesi.”

Olga Opaleva anasema hivi: “Ninaona jinsi ninavyoendelea kuvumilia, ninaona kwamba Yehova ananisaidia katika kila hali. Nimeanza kumtegemea Yehova katika kila kitu, hata mambo madogo zaidi, ninajaribu kumtupia Yeye kila kitu akibebe.”

Aleksey anakumbuka kile kilichomsaidia akiwa mahabusu na katika kifungo cha nyumbani: “[Yehova] alinisaidia kuwa imara. Nilianza kuhisi hivyo nilipokuwa nimefungiwa kizuizini kwa muda. Nilimwomba Yehova anipe ujasiri. Mara moja nikaanza kuhisi mikono yangu na miguu yangu ikiacha kutetemeka na sauti yangu pia. Niliamua akilini mwangu kwamba nitaweza kuishi chini ya hali hizi mpya.”

Olga Panyuta anasema hivi: “Jina la Yehova linasutwa, hivyo tunahitaji kumtegemea Yehova na tumtolee utumishi wa moyo wote tunapofanya mapenzi yake na kuimarisha uhusiano wetu na yeye.”

Ndugu na dada zetu wanapoendelea kusubiri hukumu tunasali kwamba wataendelea kumtegemea Yehova akiwa “Mwamba” wao ili awape nguvu za kuvumilia.​—Kumbukumbu la Torati 32:4.