Hamia kwenye habari

Kushoto hadi kulia: Ndugu Alam Aliyev, Ndugu Valeriy Kriger, Ndugu Sergey Shulyarenko, Ndugu Dmitriy Zagulin

MACHI 18, 2021 | TAREHE YA KARIBUNI: DESEMBA 20, 2022
URUSI

HABARI ZA KARIBUNI—NDUGU WAMEHUKUMIWA | Ndugu Wanne Katika Eneo la Birobidzhan Wanaweza Kufungwa Gerezani

HABARI ZA KARIBUNI—NDUGU WAMEHUKUMIWA | Ndugu Wanne Katika Eneo la Birobidzhan Wanaweza Kufungwa Gerezani

Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan katika Eneo Lililotengewa Wayahudi, iliwahukumu Ndugu Alam Aliyev, Ndugu Valeriy Kriger, Ndugu Sergey Shulyarenko, na Ndugu Dmitriy Zagulin. Ndugu Aliyev alihukumiwa miaka sita na nusu gerezani na Ndugu Zagulin akahukumiwa miaka mitatu na nusu gerezani. Ndugu Kriger na Ndugu Shulyarenko walihukumiwa miaka saba gerezani. Ndugu wote wanne walipelekwa gerezani moja kwa moja kutoka mahakamani.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Alam Aliyev

  • Alizaliwa: 1963 (Kijiji cha Lyaki, Azerbaijan)

  • Maisha Yake: Alitumikia jeshi la Muungano wa Sovieti huko Ujerumani. Baadaye alifanya kazi kwenye mashua ya uvuvi. Mnamo 1989 alihamia Khabarovsk, Urusi. Sasa anafanya kazi kiwandani

    Alianza kujifunza Biblia muda mfupi baada ya kuhamia Urusi. Alibatizwa mnamo 1991. Alifunga ndoa na Svetlana mnamo 2015. Wanafurahia kwenda matembezi

Valeriy Kriger

  • Alizaliwa: 1968 (Eneo Lililotengewa Wayahudi)

  • Maisha Yake: Alilelewa katika familia ambayo haikuwa ya kidini. Akiwa mtoto alifurahia kufanya sarakasi. Alisomea kazi ya kukanda watu na sasa ana biashara yake. Alibatizwa mnamo 1994. Alifunga ndoa na Natalya mnamo 2017. Wanafurahia kucheza mpira wa wavu na kwenda matembezi

Sergey Shulyarenko

  • Alizaliwa: 1984 (Khabarovsk)

  • Maisha Yake: Alipokuwa mtoto familia yao iliishi nchini Turkmenistan kwa kuwa baba yake alitumikia katika jeshi huko. Alianza kufanya kazi akiwa msaidizi wa kiwanda. Anapenda kuchora na kujifunza lugha nyingine. Mama yake ndiye aliyemfundisha kuhusu Yehova. Alibatizwa mnamo 1997 akiwa na umri wa miaka 13

Dmitriy Zagulin

  • Alizaliwa: 1973 (Khabarovsk)

  • Maisha Yake: Alipokuwa mtoto alitamani kuwa mwanajeshi. Alijifunza karate na akazoezwa kuruka kutoka kwenye ndege kwa kutumia parachuti. Kwa sasa anafanya kazi kwenye kampuni ya reli. Alianza kujifunza Biblia katika mwaka wa 1991. Alibatizwa mnamo 1992. Alifunga ndoa na Tatyana mnamo 2012

Historia ya Kesi

Mei 17, 2018, maofisa 150 wa usalama katika eneo la Birobidzhan walifanya uvamizi ulioitwa “Siku ya Hukumu.” Ndugu Alam Aliyev alikamatwa na kuwekwa mahabusu kwa siku nane kwa shtaka la “kupanga shughuli za shirika lenye msimamo mkali.” Ndugu Valeriy Kriger, Sergey Shulyarenko, na Dmitriy Zagulin walishtakiwa pia. Ndugu wote wanne walizuiwa wasisafiri. Mbali na hilo, wake za Ndugu Alam, Ndugu Valeriy, na Ndugu Dmitriy wameshtakiwa katika kesi tofauti.

Kabla ya kukamatwa, Alam alikuwa amefanya utafiti kuhusu jinsi ya kuvumilia mateso. Pia aliwaeleza wengine kutanikoni mambo aliyokuwa amejifunza. Anasema hivi: “Niliwatia moyo ndugu na dada wasiogope wanapokabili mateso. Habari hizo zilikuwa za wakati unaofaa kwa sababu juma moja baadaye, nyumba za familia 21 zilivamiwa na kufanyiwa upekuzi.”

Valeriy na mke wake, Natalya, hawakuweza kuhudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova lililofanyiwa Seoul, nchini Korea Kusini, kwa sababu ya vizuizi walivyowekewa vya kusafiri. Pia, hawakuruhusiwa kuwatembelea wazazi wake wanaoishi nchini Israel. Kwa kusikitisha, baba yake alikufa Februari 2019. Miezi michache kabla ya hapo, mama yake alikuwa amefanyiwa upasuaji wa uti wa mgongo na alihitaji kutunzwa kila wakati. Valeriy anasadiki kwamba Yehova aliandaa msaada. Ingawa wazazi wake si Mashahidi wa Yehova, ndugu na dada zake wa kiroho nchini Israel ndio waliosaidia kumtunza mama yake. Anaeleza hivi: “Tulisali kwa Yehova kuhusu hali ya mama yangu, na Yehova alijibu sala zetu. Ndugu na dada zetu nchini Israel walimtunza na kumfariji mama yangu. Walimtembelea, wakazungumza naye, na kumkaribisha kwenye mikutano. Ingawa hatungeweza kuwa pamoja na mama yangu, tulijionea mkono wa Yehova; jinsi anavyoweza kuwatumia ndugu na dada zetu kutusaidia.”

Mateso hayo yanamthibitishia Dmitriy jambo ambalo tayari alijua. Anasema hivi: “Kila kitu kinapokuwa shwari maishani na wakati ambapo hakuna vizuizi katika ibada yetu kwa Mungu, ni rahisi kupuuza hazina za kiroho tulizoandaliwa. Hata hivyo, wenye mamlaka wanapotuzuia kumwabudu Mungu kwa uhuru, ndipo tunapoelewa jinsi ilivyo muhimu kutumia hali zetu za sasa kujitayarisha kwa ajili ya mateso ya wakati ujao. Hivyo, ni jambo la hekima kutumia uhuru tulio nao leo ‘kujiwekea hazina mbinguni.’ Hilo litatusaidia kuvumilia hadi mwisho na kudumisha imani yetu ikiwa imara.”—Mathayo 6:20.

Ni wazi kwamba Yehova anawapa ndugu zetu wapendwa nchini Urusi “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili wavumilie.—2 Wakorintho 4:7.