Hamia kwenye habari

Ndugu Roman Baranovskiy pamoja na mama yake, Dada Valentina Baranovskaya

JANUARI 29, 2021
URUSI

HABARI ZA KARIBUNI | Ndugu Roman Baranovskiy na Mama Yake, Dada Valentina Baranovskaya, Wanakabili Kifungo Nchini Urusi

HABARI ZA KARIBUNI | Ndugu Roman Baranovskiy na Mama Yake, Dada Valentina Baranovskaya, Wanakabili Kifungo Nchini Urusi

Mei 4, 2022, Mahakama ya rufaa iliyo Khakassia ilimwachilia huru kutoka gerezani Dada Valentina Baranovskaya mwenye umri wa miaka 71. Mahakama ilikataa malalamiko yaliyowasilishwa na mwendesha-mashtaka, aliyetaka kuzuia kuachiliwa huru kwa dada huyo. Valentina alikaa gerezani kwa zaidi ya mwaka mmoja. Mwana wake, Roman, bado amefungwa gerezani kwa sababu ya imani yake.

Machi 4, 2022, ofisi ya mwendesha-mashtaka ilikata rufaa dhidi ya uamuzi wa kumwachilia Valentina uliokuwa umetolewa na Mahakama ya Wilaya ya Ust-Abakan. Mwendesha-mashtaka alisema kwamba Valentina hapaswi kuachiliwa mapema kwa kuwa “hajatubu uhalifu wake.” Valentina ataendelea kukaa gerezani hadi rufaa ya mwendesha-mashtaka itakaposikilizwa.

Mei 24, 2021, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Khakassia, Urusi, ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Roman Baranovskiy na mama yake mwenye umri wa miaka 70, Valentina. Wataendelea kukaa gerezani. Pia mahakama iliongeza vizuizi watakavyowekewa wakati ujao baada ya kuachiliwa kutoka gerezani.

Februari 24, 2021, Mahakama ya Jiji la Abakan la Jamhuri ya Khakassia ilimhukumu Roman kifungo cha miaka sita gerezani. Pia mahakama hiyo ilimhukumu Valentina, mama ya Roman, kifungo cha miaka miwili gerezani. Hii ndiyo mara ya kwanza kwa mmoja wa dada zetu nchini Urusi kufungwa gerezani kwa sababu ya imani yake. Valentina atatimiza miaka 70 mnamo Aprili 2021 na alipatwa na kiharusi mnamo Julai 2020. Walipelekwa kifungoni mara baada ya uamuzi kutangazwa.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Roman Baranovskiy

  • Alizaliwa: 1974 (Balakovo, Eneo la Saratov)

  • Maisha Yake: Ili kumtegemeza mama yake na yeye mwenyewe, anafanya kazi ya kurekebisha nyumba. Anapenda kucheza gitaa, chesi, na mpira wa miguu

    Alipokuwa kijana, alitafakari kuhusu kusudi la uhai. Anakumbuka: “Mara nyingine nilimwomba Mungu anisaidie kujua kusudi la uhai.” Alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1993. Alibatizwa mwaka wa 1997

Valentina Baranovskaya

  • Alizaliwa: 1951 (Vannovka, Kazakhstan)

  • Maisha Yake: Alifanya kazi ya uhasibu na usimamizi wa matumizi ya fedha hadi alipostaafu mwaka wa 2006. Anapenda kupika na kuandika nyimbo na mashairi

    Mwaka wa 1995, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi akiwa pamoja na mwana wake. Alivutiwa sana alipojifunza kwamba Mungu hawezi kusema uwongo. Alibatizwa mwaka wa 1996

Historia ya Kesi

Usiku wa Aprili 10, 2019, maofisa wenye silaha katika eneo la Abakan, walivamia nyumba nne kutia ndani nyumba ya Ndugu Roman Baranovskiy pamoja na mama yake, Valentina. Maofisa hao walichukua Biblia zao, vifaa vya kielektroni, na hati zao. Mashtaka ya uhalifu yalifunguliwa dhidi ya Roman na Valentina.

Roman anakumbuka hivi: “Walipovamia nyumba yetu, tulikuwa katika mkutano wa katikati ya juma na tulikuwa tumetoka kuzungumzia 1 Wakorintho 10:13. Mstari huo una wazo muhimu—Yehova haamui ni jaribu gani tutakalovumilia . . . Si kwamba anasema: ‘Una nguvu za kutosha, utavumilia jaribu hili. Lakini wewe ni dhaifu, chukua jaribu hili rahisi ushughulike nalo.’ Ikiwa angekuwa anafanya hivyo, basi tungehitaji kujitegemea ili tuweze kuvumilia jaribu lolote. Yeyote kati yetu anaweza kupatwa na jaribu la aina yoyote. Tukimtegemea Yehova, tunaweza kuvumilia.”

Mwezi wa Julai 2020, Valentina alipatwa na kiharusi. Anasema hivi: “Kadiri afya yangu ilivyozidi kuwa mbaya, ndivyo ilivyokuwa wazi kwamba Yehova alikuwa akinisaidia. Niliona hilo kwa sababu sikuacha kusali, na ni kana kwamba alinibeba na kuniweka mikononi mwake. Nilihisi amani na utulivu usioweza kuelezeka.”

Mambo yote ambayo Valentina alijionea yalimfanya afikie mkataa huu wenye usadikisho: “Nimeazimia kumtumikia Baba yangu milele na kuendelea kuwa mwaminifu kwake hata hali iweje.”

Roman anasema kwamba kutafakari mifano ya watu waliovumilia majaribu inayopatikana katika Biblia na ya nyakati zetu, kumeimarisha imani yake. Anapotafakari mifano hiyo, mara nyingi yeye hujiuliza: ‘Walipata changamoto gani na kwa nini? Ni nini kilichowasaidia kuendelea kuwa waaminifu? Yehova aliwategemeza jinsi gani kupitia roho yake?’ Majibu ya maswali hayo yamempa Roman uhakika wa kwamba, hata jaribu liwe la aina gani, “Yehova ataandaa nguvu zisizo za kawaida ikihitajika.”

Tunasali kwamba Roman, Valentina, na ndugu na dada zetu wapendwa wote nchini Urusi waendelee kumtegemea Yehova ambaye ni kimbilio na nguvu kwa ajili yao.​—Zaburi 46:1.