Hamia kwenye habari

Juu (kushoto hadi kulia): Ndugu Boris Burylov, Aleksandr Inozemtsev

Chini (kushoto hadi kulia): Ndugu Viktor Kuchkov, Igor Turik, Yuriy Vaag

APRILI 21, 2021
URUSI

HABARI ZA KARIBUNI | Ndugu Watano Wadumisha Ujasiri na Shangwe Licha ya Uvamizi na Wengi Kukamatwa Katika Jiji la Perm, Urusi

HABARI ZA KARIBUNI | Ndugu Watano Wadumisha Ujasiri na Shangwe Licha ya Uvamizi na Wengi Kukamatwa Katika Jiji la Perm, Urusi

Mei 12, 2022, Mahakama ya Saba ya Kuchunguza Upya Maamuzi ya Mahakama za Chini ilikataa kwa mara ya pili ombi la rufaa ya Ndugu Boris Burylov, Ndugu Aleksandr Inozemtsev, Ndugu Viktor Kuchkov, Ndugu Igor Turik, na Ndugu Yuriy Vaag. Hawahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Agosti 23, 2021, Mahakama ya Eneo la Perm ilikataa ombi la rufaa ya Boris, Aleksandr, Viktor, Igor, and Yuriy. Hukumu zao za awali zitaendelea kutumika.

Mei 12, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Viwanda ya Jiji la Perm ilitangaza uamuzi wake katika kesi kuwahusu Boris, Aleksandr, Viktor, Igor, na Yuriy. Igor alihukumiwa kifungo cha nje cha miaka saba. Ndugu hao wengine wanne walihukumiwa vifungo vya nje vya miaka miwili na nusu.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Boris Burylov

  • Alizaliwa: 1941 (Sevastopol)

  • Maisha Yake: Alilelewa katika Eneo la Perm. Alijipatia diploma katika ukulima. Alipokuwa mtoto, mama yake alimsomea sehemu za Biblia. Katika miaka ya 1990, alipata Biblia nzima. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1996

Aleksandr Inozemtsev

  • Alizaliwa: 1972 (Kostanay)

  • Maisha Yake: Alitumikia jeshini. Amefanya kazi akiwa fundi umeme, fundi wa magari, na sasa anafanya kazi ya udumishaji wa majengo na kurekebisha nyumba. Baada ya kusoma Biblia na kujifunza na Mashahidi wa Yehova, alipata majibu yenye kuridhisha kuhusu kwa nini watu wanapatwa na ukosefu wa haki na kifo. Alibatizwa mwaka wa 1996. Alifunga ndoa na Olesya mwaka wa 2017 na pamoja wanamlea binti yake mdogo. Aleksandr anafurahia kuchora, kucheza mpira wa magongo, na kuvua samaki

Viktor Kuchkov

  • Alizaliwa: 1967 (Svetlitsa)

  • Maisha Yake: Alipenda kuchonga mbao tangu alipokuwa mtoto. Alijifunza kutengeneza vitu vya chuma na pia amefanya kazi akiwa msanifu wa mifumo na vifaa mbalimbali. Anapenda kuvua samaki na kucheza mpira wa wavu. Alifunga ndoa na Tanya mwaka wa 1988. Wana binti mmoja. Sikuzote amependezwa na habari za kiroho. Katika mwaka wa 1993 alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova

Igor Turik

  • Alizaliwa: 1968 (Nelidovo)

  • Maisha Yake: Anafanya kazi akiwa mpiga-picha na msanifu-majengo. Katika mwaka wa 1990, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alipendezwa na upatano uliomo katika Biblia. Alibatizwa mwaka wa 1998. Alifunga ndoa mwaka wa 2002 na ana mwana na binti. Anapenda kupiga picha, video, na kurekebisha redio

Yuriy Vaag

  • Alizaliwa: 1975 (Lesosibirsk)

  • Maisha Yake: Alijifunza kuendesha kreni. Sasa anafanya kazi akiwa fundi umeme na udumishaji wa majengo. Alipokuwa jeshini, dada yake alianza kumweleza mambo ambayo Biblia inafundisha. Baada ya kuona jinsi dada yake alivyofanya mabadiliko mazuri maishani mwake kwa sababu ya kufuata mafundisho ya Biblia, alichochewa kujifunza Biblia pia. Alibatizwa mwaka wa 1996. Alifunga ndoa na Svetlana mwaka wa 1996. Wana mwana na binti

Historia ya Kesi

Septemba 17, 2018, Maofisa wa Usalama wa Taifa (FSB) na maaskari wengine wa kitengo cha pekee walivamia nyumba nyingi katika Eneo la Perm. Nyumba kumi hivi za ndugu zetu zilifanyiwa upekuzi. Wakati wa upekuzi huo, maofisa walichukua pesa, simu, na vifaa vingine vya kielektroni. Viktor na Igor walizuiliwa kwa siku kadhaa kisha wakawekwa katika kifungo cha nyumbani kwa miezi minne hivi. Kwa sasa, mahakama imewawekea masharti mbalimbali. Majina yao yameongezwa kwenye orodha ya Urusi ya watu “wenye msimamo mkali.”

Kila mmoja kati ya ndugu hao anaendelea kuonyesha ujasiri na shangwe licha ya changamoto wanazokabili.

Yuriy anasimulia jinsi sasa anavyosali kwa Yehova mara nyingi zaidi. Pia, yeye hutafakari kwa ukawaida njia ambazo Yehova humtegemeza na kumwimarisha. Anasema hivi: “Maneno ya Yoshua 1:7 hunisaidia kuwa mtulivu. Nilipata mwongozo katika maneno hayo ambayo nilihitaji kufuata. Ningeweza kuhisi kwamba Yehova alikuwa akinisaidia na kunitunza.”

Viktor anasema kwamba kutafakari kuhusu tengenezo la Yehova kulimsaidia kuendelea kuwa mtulivu wakati wa kesi yake. Anasema hivi: “Nilijaribu kuwazia ukuu wa Yehova, sehemu inayoonekana na sehemu isiyoonekana ya tengenezo lake, undugu wetu, kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na jinsi kweli ya Biblia ilivyo nzuri na inavyopatana na akili. Kufanya hivyo kulinisaidia nisijikazie fikira. Nilipofanya hivyo ghafla nilijihisi nikiwa mtulivu sana.”

Baada ya kurudi nyumbani, Igor alijikuta akicheka alipokumbuka mambo fulani yaliyotokea. Anasema hivi: “Nilipokuwa kizuizini, binti yangu alichora picha ya ulimwengu mpya ili kunitia moyo. Maofisa hawakuniruhusu nipate picha hiyo. Mke wangu anasema walinzi wa gereza walitazama picha hiyo kwa muda mrefu halafu wakamrudishia na kumwambia: ‘Hatuwezi kuruhusu picha hii iingie ndani. Inaonekana kama mchoro wa kumsaidia kutoroka gerezani.’” Anaendelea kusema: “Kwa kweli hawakukosea, ulimwengu mpya ndiyo njia yetu ya ‘kuutoroka’ mfumo huu mwovu!”

Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kutumia roho yake takatifu kuwasaidia ndugu hao pamoja na familia zao. Tunajua kwamba sikuzote Yehova atawapa nguvu wanazohitaji.​—Waefeso 3:20.