Hamia kwenye habari

Mahakama ya Mkoa wa Oryol

URUSI

Hati ya Dennis Christensen Alipozungumza Mbele ya Mahakama Mei 16

Hati ya Dennis Christensen Alipozungumza Mbele ya Mahakama Mei 16

Kesi yake iliposikilizwa Alhamisi, Mei 16, 2019, Dennis alipata nafasi ya kujitetea kwa saa moja hivi. Haya ndiyo maneno (yaliyotafsiriwa kutoka Kirusi) yenye nguvu aliyosema Dennis mahakamani:

Kanuni hii ilitajwa na mwanamume fulani mbaya sana miaka mingi iliyopita: ‘Kadiri uwongo unavyorudiwa, ndivyo unavyozidi kuwa ukweli’—kumaanisha kwamba uwongo unaporudiwa mara elfu moja unakuwa ukweli. Uwongo huo, ambao watu fulani wamejaribu kuupitisha kana kwamba ni ukweli, umesababisha matatizo mengi na kuumiza watu wengi wasio na hatia.

Hayo ni mambo ya zamani, na watu wengi hufikiri kwamba wasomi wa karne ya  21 walijifunza kutokana na mambo yaliyotokea zamani.

Lakini inaonekana kwamba sivyo ilivyo katika kisa hiki. Njia hizo zinatumika tena katika kesi hii dhidi yangu na dhidi ya Mashahidi wengine wa Yehova nchini Urusi. Na si hilo tu, uwongo huo unasababisha matatizo mengi na kuumiza watu wengi wasio na hatia.

Kwa upande wangu, uwongo huu unatia ndani tuhuma za kwamba mimi niliendeleza utendaji wa Shirika la Kidini la Oryol (LRO) la Mashahidi wa Yehova, ambalo mahakama ililihukumu kuwa na msimamo mkali, na kwamba nilikuwa nikitenda kwa siri ili kufikia kusudi hilo.

Mashtaka hayo yamerudiwa tena na tena katika pindi yote ya kesi hii, bila ushahidi wowote. Kwa njia hii, inaonekana kwamba wamejaribu kufanya uwongo huo uwe ukweli.

Ukweli ni kwamba sijawahi kuwa na ushirikiano wowote na Shirika la Kidini la Oryol (LRO) la Mashahidi wa Yehova.

Ni kweli kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova. Mimi pamoja na rafiki zangu huhudhuria ibada mbalimbali za kidini zinazoongozwa na kikundi cha kidini ambacho hakina uhusiano wowote na Shirika la Kidini la Oryol (LRO) la Mashahidi wa Yehova, na mambo haya yanapatana na sheria kulingana na Kifungu cha 28 katika Katiba ya Shirikisho la Urusi.

Sikuendeleza utendaji wa Shirika la Kidini la Oryol (LRO) la Mashahidi wa Yehova lililopigwa marufuku na sikuvunja sheria yoyote ya Urusi. Sijawahi kujihusisha na mambo yoyote yenye msimamo mkali.

Watu wengi wameniuliza: “Kwa nini Mashahidi wa Yehova wenye kupenda amani namna hiyo wanaonwa kuwa wenye msimamo mkali, ni jambo gani hasa linalofanya waitwe watu wenye msimamo mkali?” Na jibu langu ni: “Sijui!”

Mashahidi wa Yehova wanapenda jirani zao kama wanavyojipenda wenyewe. Wanajaribu kufanya mambo mazuri katika jamii (yanayonufaisha jamii). Wao ni watu wanyoofu wanaotii sheria na wanaolipa kodi. Ni nini kinachowafanya wawe “wenye msimamo mkali?” Kwa mimi binafsi, sijui, na hata kadiri kesi hii inavyoendelea, mimi bado sijapata jibu.

Ninatuhumiwa kwa kuendeleza kazi ya shirika dogo la kisheria lenye watu kumi hivi ambalo kilihukumiwa kuwa cha watu wenye msimamo mkali. Ni lini na kwa njia gani mimi nimeendeleza kazi za shirika hilo la kisheria? Ni kazi gani hususa niliyofanya inayoonyesha kwamba nina msimamo mkali?

Sijawahi kupata hata jibu moja kwa ajili ya haya maswali kesi hii inapoendelea. Na, je unajua ni kwa nini sijapata? Kwa sababu wanajaribu kufanya uwongo uwe ukweli kwa kuurudia tena na tena!

Hapa nchini Urusi, kuna mtu anayejaribu kwelikweli kufanya watu hawa wenye kufanya amani, hawa Mashahidi wa Yehova waonekane kama watu wenye msimamo mkali lakini huo ni ukosefu wa haki, ni jambo lisilo na uhusiano wowote na ukweli. Mashahidi wa Yehova hawana msimamo mkali. Na je, unajua kwa nini?

Kwanza kabisa Mashahidi wa Yehova hawatumii silaha na hawajihusishi kabisa katika vita. Katika Vita vya Pili vya Ulimwengu nchini Ujerumani, walidhabihu maisha yao kwa kukataa kutumikia jeshi la Wehrmacht, nchini Ujerumani. Hawakuenda Eastern Front (Eneo la Mashariki la Vita) na hawakuua wanajeshi wa Sovieti.

Katika Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti (USSR), Mashahidi wa Yehova waliteswa kikatili na walisemwa kuwa maadui wa watu kwa kupinga serikali ya Kikomunisti. Lakini hawakuwachukia watu waliowanyanyasa.

Leo, Mashahidi wa Yehova wameungana katika undugu wa ulimwenguni pote unaofanyizwa na watu mmojammoja wanaotoka mataifa mbalimbali na watu. Wanaishi pamoja kwa amani na umoja. Hilo linaonyesha kwamba licha ya kwamba sote tunatofautiana, ni jambo linalowezekana kushinda tofauti zinazowatenganisha watu.

Pili, hakuna sehemu nyingine yoyote duniani, tofauti na nchi ya Urusi, ambako Mashahidi wa Yehova wanaonwa kuwa wenye msimamo mkali. Mashahidi wa Yehova wanaruhusiwa kufanya kazi zao kwa amani na uhuru katika nchi zaidi ya 200 duniani pote. Wao hujulikana kuwa watu wenye amani ambao hawana uhusiano wowote na msimamo mkali.

Wameunganishwa kwa mafundisho yaleyale yanayotegemea Biblia, ambayo yanawachochea waonyeshe sifa nzuri, kama vile upendo, shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, [upole], na kujizuia.

Katika Biblia, sifa hizo zinaitwa “tunda la roho,” na sifa kama hizo hazisababishi matatizo katika jamii. Sifa hizo hazina uhusiano wowote na msimamo mkali. Badala yake, zinawanufaisha watu wote.

Tatu, kutumia Sheria ya Kupambana na Utendaji Wenye Msimamo Mkali ya Urusi kuwapinga Mashahidi wa Yehova ni jambo linaloshutumiwa na wataalamu wa haki za kibinadamu nchini Urusi. Wengi wao wamesema waziwazi kwamba hatua hiyo inaletea suto jina zuri la nchi ya Urusi kwa kuwa ni nchi ya kidemokrasia inayoongozwa wa sheria. Wataalamu hao wasingechambua matumizi ya sheria hiyo ikiwa Mashahidi wa Yehova wangekuwa na dalili yeyote ya kuwa na msimamo mkali.

Nne, watu ulimwenguni pote pia wameshutumu matumizi ya Sheria ya Kupambana na Utendaji Wenye Msimamo Mkali ya Urusi kuwapinga Mashahidi wa Yehova nchini Urusi. Baraza la Bunge la Ulaya linawahimiza wenye mamlaka nchini Urusi waache kutumia sheria hiyo kuwapinga Mashahidi wa Yehova. Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa (CCPR) imesema mara kadhaa kwamba wanahangaishwa kugundua kwamba nchini Urusi sheria ya kupambana na utendaji wenye msimamo mkali inatumiwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova, watu wanaoishi kwa amani na wasio na hatia wananyanyaswa kwa sababu hiyo.

Yesu Kristo aliwaonya wafuasi wake: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yohana 15:20) a Mwishowe, alihukumiwa na kuuawa kwa shtaka la uwongo la kwamba alikuwa na msimamo mkali, jambo ambalo lilikuwa ukosefu mkubwa wa haki.

Lakini hatuishi katika karne ya kwanza, na hata si Enzi za Kati. Tunaishi katika karne ya  21, wakati ambapo haki za kibinadamu na uhuru wa kidini—ni haki ambazo watu wote wanapaswa kuwa nayo kwa kiwango kilekile.

Je, inawezekana kweli kumkataza mtu kumwamini Mungu, kisha kumfunga gerezani kwa sababu hiyo? Ninaamini hilo ni kosa. Hilo hutokea katika nchi zinazotawaliwa na madikteta tu, na si katika nchi ya kidemokrasia inayoongozwa na sheria, ndivyo ninavyofikiri nchi ya Urusi ilivyo.

Kesi hii ilipokuwa ikiendelea, nimesikia kwamba watu fulani nchini Urusi huona mtu anayeamini kwamba imani yake ni ya kweli na anayeitangaza hadharani huwa mtu mwenye msimamo mkali. Jambo hili halipatani na akili kwa sababu watu wa dini zote huamini kwamba wana dini ya kweli. Basi, kwa nini wanaendelea kuabudu katika dini zao ikiwa hawaamini kuwa dini yao ni ya kweli?

Ikiwa hilo linatosha kumtangaza mtu kuwa na msimamo mkali, basi Yesu Kristo angefaa kuitwa hivyo pia. Alimwambia Pontio Pilato hivi: “Nimezaliwa kwa ajili ya hili, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi kuhusu kweli. Kila mtu aliye upande wa kweli huisikiliza sauti yangu.”—Yohana 18:37.

Na hili linamaanisha kwamba kuna kweli ya [Biblia]. Yesu alitangaza kweli na kuwafundisha wanafunzi wake kuihusu. Hakumaanisha ukweli kwa ujumla. Badala yake alizungumza kweli kuhusu kusudi la Mungu. Kimsingi, kusudi la Mungu ni kwamba Yesu, “mwana wa Daudi” (mzao wake), atumike akiwa Kuhani Mkuu na Mtawala wa Ufalme wa Mungu.

Yesu alisema kwamba kusudi lake kuu la kuja ulimwenguni na ya maisha yake hapa duniani lilikuwa kutangaza ukweli kuhusu Ufalme huo. Je, leo watu humwona Yesu kama mtu mwenye msimamo mkali kwa sababu alitangaza ukweli huo?

Mashahidi wa Yehova wanafuata mfano wake na wanatangaza ukweli ambao umeandikwa katika Biblia, kwamba Ufalme wa Mungu ni suluhisho pekee kwa matatizo yote ya mwanadamu. Wanashiriki na watu wote yale yaliyoandikwa katika Neno la Mungu, Biblia.

Pindi fulani Yesu alisali kwa Mungu na kusema: “Watakase kupitia ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Hivyo basi, ni muhimu watu wa namna zote wajifunze ukweli uliopo katika Biblia. Itawanufaisha na haihusiani kabisa na msimamo mkali.

Si Mashahidi wa Yehova pekee wanaothamini Biblia. Mwanasayansi Mrusi Mikhail Lomonosov alisema hivi: “Muumba amewapa wanadamu vitabu viwili. Katika kitabu kimoja Alifunua ukuu wake, na katika kitabu kingine—Alifunua mapenzi yake. Ya kwanza ni ulimwengu tunaouona, ambao Yeye aliumba . . . Na kitabu cha pili ni Maandiko Matakatifu.”

Bila shaka, Lomonosov alichunguza Maandiko Matakatifu kwa makini na alikuwa sahihi. Tunaweza kujifunza mengi kumhusu Mungu kwa kuchunguza uumbaji. Na tunaweza kujifunza mengi zaidi kumhusu tukisoma, kujifunza, na kuchunguza Neno lake, Biblia.

Biblia inasema kuhusu mambo yaliyomo: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, . .  kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa ajili ya kila kazi njema!

Kwenye mikutano ya Kikristo niliyohudhuria na kushiriki, na ambayo yaliongozwa na kikundi cha kidini ambacho hakina uhusiano wowote na Shirika la Kidini la Oryol (LRO) la Mashahidi wa Yehova linalotambulika kisheria, tunazungumzia njia za kufanya matendo mema kwa ajili ya watu.

Katika video mbili za ibada yetu zilizofanywa Februari 19 na 26, 2017, ambazo tulitazama mahakamani, tuliona wazi kwamba hakukuwa na chochote ambacho kingetutambulisha kuwa watu wenye msimamo mkali. Tulizungumzia mambo yanayotegemea Biblia yanayowanufaisha watu wa namna zote. Ibada yetu ilifanyika kwa amani na shangwe, ambayo ndiyo kawaida ya mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova.

Mambo yanayotegemea Biblia tuliyozungumzia hayaletei jamii madhara. Badala yake, yanawasaidia sana na kuwafariji watu wengi. Kwa wale ambao wanaomboleza wapendwa wao waliokufa, Biblia ina ahadi hii yenye kufariji: “Na adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26.

Kifo ni adui ya kila mwanadamu lakini si adui anayemtisha Mungu. Anaahidi hivi katika kitabu cha Isaya 25:8: “Atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atafuta kabisa machozi katika nyuso zote.”

Wazia wakati huo! Hakutakuwa na mazishi au maeneo ya makaburi. Machozi ya shangwe yatachukua sehemu ya machozi ya huzuni, wakati ambapo Mungu atatimiza ahadi yake yenye kustaajabisha ya kuwafufua wafu. Wakati huo, vidonda vyetu visivyohesabika vilivyosababishwa na kifo vitapona.

Mambo hayo yana maana kubwa sana kwangu mimi kwa sababu nimepoteza watu wengi ninaowapenda sana. Wakati nilipokuwa mahabusu, mtu muhimu sana kwangu, alikufa—bibi yangu, Helga Margrethe Christensen.

Yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza katika familia yetu kujifunza Biblia na kuwa Shahidi wa Yehova. Kwanza alimfundisha baba yangu ukweli wa Biblia kisha akanifundisha mimi. Watu wengi waliomjua—majirani, watu alioshirikiana nao, watu wa familia—walimpenda na kumheshimu.

Yeye pia aliwapenda na kuwaheshimu watu wote, bila kujali imani yao, taifa lao, au rangi yao. Alijaribu kusaidia watu wote, na aliwatendea majirani matendo mema. Kwa kusikitisha, huenda watu fulani wangemwita mtu mwenye msimamo mkali. Lakini watu wengi ambao wana uwezo wa kufikiri hawangekubaliana nao.

Ninasubiria siku ambayo Mungu atamfufua, kisha tutakutana tena. Ninasikitika sikuweza kufika kwenye mazishi yake. Nimeshindwa kufariji familia yangu katika kipindi hiki kigumu, kwa kuwa nimekuwa mahabusu kwa tuhuma hizi zisizo na msingi za kuwa na msimamo mkali.

Tumaini la Biblia la ufufuo wa wafu linanifariji na kunihakikishia kwamba sijampoteza milele, siku moja tutaonana tena kwenye dunia iliyosafishwa chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Ikiwa tumaini hili linaweza kunisaidia na kunifariji, nina uhakika kwamba linaweza kuwasaidia wengine na kuwafariji.

Jambo lingine linalotegemea Biblia tunalozungumzia katika mikutano yetu ni paradiso ya wakati ujao itakayokuwa duniani, kutakuwa na chakula cha kutosha kwa ajili ya watu wote na amani miongoni mwa watu wote; hakuna mtu atakuwa mgonjwa, kama ilivyotabiriwa na Isaya 33:24: “Na hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’ Watu wanaokaa katika nchi watasamehewa dhambi yao.”

Je, kuwaeleza wengine ahadi hizo zinaweza kuwa na madhara kwa jamii? Kinyume chake, ahadi hizo zinaweza kuwapa watu tumaini na kuwaletea shangwe. Yesu mwenyewe alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:28.

Kuamini hilo au la ni uamuzi wa kibinafsi wa kila mtu. Mungu hamlazimishi mtu yeyote amtumikie. Kwenye Yeremia 29:11, alisema hivi: “‘Kwa maana ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.’”

Mungu anampa kila mmoja wetu fursa ya kuishi ya maisha bora—kusitawisha urafiki wa karibu naye. Mashahidi wa Yehova wanawaalika watu wachague njia hiyo bora, njia ya kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu ambao utawasaidia kupata uzima wa milele. Mambo hayo hayahusiani na msimamo mkali hata kidogo. “Utendaji wangu wenye msimamo mkali” ni upi na kwa nini wanataka kunifunga gerezani kwa miaka sita?

Sikutenda kama mhalifu au mtu mwenye msimamo mkali. Majirani wangu, msimamizi katika jamii yetu, na maofisa wa mahabusu wanasema mambo mazuri kunihusu. Hivyo, kwa mara nyingine ningependa kuuliza swali hili: “Utendaji wangu wenye msimamo mkali” ni upi na kwa nini wanataka kunifunga gerezani kwa miaka sita?

Sielewi, na kwa hii miaka miwili bado sijapata jibu la swali hili. Labda Mahakama ya Rufaa inaweza kunipa majibu hususa, kwa sababu mahakama ya kwanza haikujibu maswali yangu.

Kama nilivyosema awali, tunaishi katika karne ya 21, si katika Enzi za Kati. Wanadamu wamefanya maendeleo. Lakini inasikitisha sana kwamba watu nchini Urusi wanateswa tena kwa sababu ya imani yao, na hata wanatendewa kikatili kwa sababu ya imani yao.

Februari 15, 2019, Mashahidi saba wa Yehova walipohojiwa, Kamati ya Uchunguzi huko Surgut iliwatesa ili kupata majibu waliyoyataka. Waabudu hao hawakuruhusiwa kutumia Kifungu cha 51 cha Katiba ya Shirikisho la Urusi kwamba wasitoe ushahidi dhidi yao wenyewe na dhidi ya wapendwa wao, hata ingawa kifungu hicho cha Katiba kinawahusu watu wote nchini Urusi.

Walilazimishwa kupiga magoti wakiwa wameinua mikono, wakapigwa kichwani na mwilini, walidhalilishwa kwa msingi wa kitaifa na wa kidini; mfuko ulifungwa juu ya vichwa vyao na kugundishwa shingoni ili wasiweze kupumua, mikono yao ilifungwa nyuma ya mgongo, na miguu yao ikafungwa pia. Walipigiwa kelele na kulazimishwa kusema mambo fulani. Mara kadhaa, baadhi ya Mashahidi hao walihisi kwamba kifo kiko karibu na wakapoteza fahamu kwa sababu ya kukosa hewa. Kisha wakamwagiwa maji, na kupigwa umeme kwa bunduki za kutoa umeme.

Mambo hayo yote yalirekodiwa kwa uangalifu na wataalamu, lakini hakuna kesi hata moja ya uhalifu dhidi ya Kamati ya Uchunguzi. Watu wenye mamlaka hupuuzia tu au kudai kwamba Mashahidi hao walijisababishia majeraha hayo. Huo ni upuuzi mtupu! Huo ni uwongo uliopita mpaka!

Mambo hayo yote yanaaibisha historia ya kisasa ya nchi ya Urusi, na ninatumaini watesaji hao watafikishwa mahakamani na kuadhibiwa. Wanawezaje kuwatendea watu hivyo? Wanawezaje kutumia mbinu hizo za kikatili zilizotumiwa na Hitler na Stalin? Ninatumaini kwamba hali haitazorota kiasi hicho. Natumaini kwamba hilo ni kosa ambalo litarekebishwa hivi karibuni!

Hukumu ya mahakama ya chini inasema: “Ni uhalifu kuendeleza utendaji wa shirika la kidini ambalo limepigwa marufuku na uamuzi wa mahakama kwa msingi wa utendaji wenye msimamo mkali, utendaji wenye msimamo mkali unaohitaji kuadhibiwa.” Hilo linaeleweka. Lakini hilo linanihusuje?

Hayo hayanihusu hata kidogo! Sijawahi kufanya chochote kinachohusiana na shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova (LRO) la Oryol. Sijaendeleza utendaji wa shirika hilo hata kidogo.

Matendo yangu yote yalihusiana na maisha yangu nikiwa Mkristo katika kikundi cha kidini ambacho hakina uhusiano na shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova (LRO) la Oryol. Matendo yangu yote yalikuwa sahihi kisheria na yalipatana na Kifungu cha 28 cha Katiba ya Shirikisho la Urusi.

Sijawahi kuona matendo yangu kuwa mwendelezo wa utendaji “kinyume cha sheria” wa shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova (LRO) la Oryol. Katika mazungumzo yangu kwenye simu, ambayo tuliyasikiliza mahakamani, nilimwambia rafiki yangu: “Sisi ni kikundi cha kidini. Hatuhusiani na LRO au Kituo cha Usimamizi.”

Mahakama ya chini ilipuuza hilo na badala yake ikatumia ushahidi wa uwongo wa shahidi wa siri A. P. Yermolov, mwakilishi wa FSB. Mahakama ya rufaa inaweza kuthibitisha kwamba kihalisi A. P. Yermolov ni Oleg Gennadyevich Kurdyumov.

Mwanzoni, Oleg Kurdyumov alitoa ushahidi kwamba hakujua chochote na kwamba alitumia Kifungu cha 51 cha Katiba ya Urusi. Siku iliyofuata, alitoa ushahidi tofauti akitumia jina bandia A. P. Yermolov. Baadaye, alitoa ushahidi zaidi akitumia jina hilo.

Mahakamani tulipotazama video hizo mbili za ibada zetu za Kikristo zilizochukuliwa Februari 19 na Februari 26, 2017, ambazo hazikuhusiana na shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova (LRO) la Oryol, ilikuwa wazi kwamba Oleg Kurdyumov ndiye aliyerekodi kisiri video hizo za ibada zetu. Lilikuwa jambo la kuchekesha kuona wazi kwamba ndiye aliyekuwa na kamera. Kamera iliposogea, alisogea, na mtu alipoongea naye, ungemsikia akisema waziwazi, “Habari? Jina langu ni Oleg.”

Kwanza, hilo linamaanisha kwamba anafanya kazi akiwa mpelelezi wa siri wa FSB, kwa kuwa alikuwa akirekodi ibada zetu. Lakini sasa, anakuja na kueleza jina lake halisi na kudai kwamba hajui chochote. Siku inayofuata, anadanganya na kutumia jina bandia, uwongo ambao anautumia mahakamani na kutumika akiwa shahidi wa siri. Hiyo ni haki kweli?

Kulingana na sheria, wapelelezi wa FSB, hawana haki ya kutoa ushahidi wa siri mahakamani. Lakini waendesha mashtaka, ofisi ya mwendesha-mashtaka, na hakimu wa mahakama ya chini walifumbia macho ukweli huo na kumruhusu kutoa ushahidi wa uwongo. Na ushahidi huo unatumiwa dhidi yangu. Siwezi kuelewa ni jinsi gani mahakama iliruhusu hilo.

Na jambo linalochanganya hata zaidi ni jinsi waendesha-mashtaka, na ofisi ya mwendesha-mashtaka ingeweza kuruhusu hilo litokee. Ofisi hiyo inapaswa kuhakikisha sheria zote za Urusi zinafuatwa na isiruhusu sheria zozote zipingwe. Lakini iliruhusu hilo litokee kwa kufumbia macho ushahidi wa uwongo.

Ninaiomba mahakama ya rufaa inielewe vizuri. Mimi binafsi, sina chochote dhidi ya watu hao. Nina hakika kwamba ni watu wazuri ambao ningefurahia kunywa nao kahawa wakati ujao, na tutacheka pamoja kuhusu mambo haya yote. Lakini sifurahii ubora wa kazi yao, ambao unasikitisha kweli.

Ninaelewa kwamba mahakama ya chini waliona ikiwa rahisi kutumia shahidi wa uwongo ambaye ni mpelelezi wa FSB, kwa kuwa shahidi huyo wa siri hana dhamiri, anaweza kudanganya kwa urahisi na kupinda ukweli, na kuiambia mahakama chochote kwa kusudi la kunifunga.

Shahidi kama huyo hawezi kutumainiwa na hawezi kuonwa kuwa chanzo cha habari zinazotegemeka. Si sawa kutumia mashahidi wa uwongo kama hao kuwafanya watu wasio na hatia wafungwe gerezani.

Miaka miwili hivi iliyopita, kesi yangu kuhusu kuachwa mahabusu ilipokuwa ikiendelea niliiambia mahakama, “Ninaomba mnirudishie maisha yangu!” Bado ninatoa ombi hilo.

Kuhusiana na kuwekwa mahabusu, ninahisi kwamba hawataki tu kunitenga na jamii na kunifunga. Wanataka kunitenga na watu kwa ujumla ili nisivute uangalifu wao kuhusu vikao vya mahakama.

Kwa kweli, ninaona kifungo changu kuwa kinyume cha sheria, na dhidi ya ubinadamu. Kusudi lake ni kuninyima nafasi ya kujitetea vizuri na kuwaeleza waandishi wa habari maoni yangu kuhusu mambo yanayonipata. Lakini muda huo utafika hakika!

Naam, ningependa mnirudishie maisha yangu ili niendelee kuishi kwa amani na utulivu katika jiji hili maridadi pamoja na mke wangu, Irina. Kwa miaka miwili hivi, sijaishi maisha yangu ya kawaida. Nimeishi maisha ambayo wengine wamenichagulia.

FSB wamenichongea na kupaka tope jina langu zuri. Wametumia hati za uwongo na uchunguzi wa wataalamu na mashahidi wa uwongo wa siri ambao wamesema uwongo dhidi yangu mahakamani.

Wamefanya hayo yote ili kumfanya mwabudu mwenye amani awe mtu mwenye msimamo mkali ambaye ni hatari kwa wengine na kwa usalama wa taifa la Urusi. Kwa kweli, mashtaka hayo yanachekesha na hayapatani na akili.

Inasikitisha kwamba mahakama ya chini iliunga mkono mashtaka hayo na kupuuza ukweli. Mheshimiwa Hakimu, tafadhali komesha hali hii na utetee ukweli. Ninakuomba, “Nirudishie maisha yangu!”

Nilisema hivi miezi mitatu iliyopita katika mahakama ya chini: “Matokeo tu ya kesi hii ambayo ningekubaliana nayo ni kuondolewa mashtaka na kuachiliwa, kuombwa msamaha, na kulipwa fidia. Siwezi kukubaliana na matokeo mengine!” Bado ninahisi vivyo hivyo.

Uamuzi mwingine wowote ungeonyesha ukosefu wa haki na ningeukatia rufaa katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu iliyoko Strasbourg. Bila shaka, ningeshinda kesi huko.

Baada ya hapo, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, watu ulimwenguni pote, na maofisa wenye cheo cha juu nchini Urusi, kutia ndani Rais Vladimir Vladimirovich Putin, watashangaa na kujiuliza ni kwa nini mahakama ya Oryol haingeweza kuona jambo linaloonekana wazi na kila mtu—kwamba kesi hii ilianzishwa kwa msingi wa uwongo ambao wamejaribu kufanya ikae kama ukweli kwa kuurudia tena na tena.

Je, kweli kuna uhitaji wa kufunga safari ndefu hivyo ili kupata haki? Mahakama ya rufaa leo ikiona kwamba kuna uhitaji wa kufanya hivyo, basi ningependa kuwajulisha wote waliopo leo, na wale wanaofuatilia kesi hii, “Niko tayari kufanya hivyo!”

Sitakata tamaa kwa sababu ninajua kwamba sina hatia ya mambo niliyoshtakiwa na kwamba ukweli upo upande wangu. Siogopi kwenda gerezani, ingawa huo ungekuwa uamuzi usio wa haki kabisa.

Siogopi na sina wasiwasi. Nina amani ya moyoni na utulivu. Mungu wangu, Yehova, hataniacha, na tayari ninaona utimizo wa maneno haya yenye kutia moyo:

Mungu ni mwadilifu,

Upendo wangu akumbuka.

Hataniacha kamwe,

Mungu wangu yuko nami.

Ndiye huniruzuku

na kunilinda sikuzote.

Baba yangu, Mungu wangu,

na Rafiki.

Ni hayo tu. Asanteni kwa kunisikiliza!

a Dennis alinukuu tafsiri ya Kirusi ya synodal. Hata hivyo, katika tafsiri yetu tumetumia Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.