Hamia kwenye habari

Mahakama ya Mkoa wa Oryol

URUSI

Hati ya Dennis Christensen Alipozungumza Mbele ya Mahakama Mei 23

Hati ya Dennis Christensen Alipozungumza Mbele ya Mahakama Mei 23

Wakati wa kusikilizwa kwa rufaa yake Alhamisi, Mei 23, 2019, Dennis aliweza kuzungumza mahakamani kwa mara ya mwisho. Haya ndiyo maneno aliyosema (yaliyotafsiriwa kutoka Kirusi):

Sasa ningependa kuwashukuru sana wote ambao wamenisaidia na kunitegemeza kwa miaka miwili katika kesi hii ya uhalifu.

Kwanza, ningependa kumshukuru mke wangu, Irina, ambaye tangu mwanzo amefanya yote aliyoweza ili kunisaidia na kunitegemeza. Amenitunza, akaniletea nguo, chakula, dawa, na vitu vingine nilivyohitaji nikiwa mahabusu. Alinitegemeza kihisia na kiroho kwa kunitembelea na kuniandikia barua, ambazo nilipokea kila siku.

Mke wangu mpendwa, imani yako yenye nguvu, subira yako, utulivu wako, upendo wako kwangu na kuelekea kweli, pamoja na kutarajia mema—hayo yote yameniwekea mfano mzuri wa kuiga. Unapaswa kujua kwamba ninakupenda sana na ninajivunia kuwa na mke kama wewe!

Pia ningependa kuwashukuru watu wa familia yangu walio huko Denmark, hasa baba yangu aliyezeeka na dada yangu. Jueni kwamba ninawakosa sana. Ninawapenda na ninathamini mambo yote ambayo mmenifanyia. Muda ambao nimekuwa mahabusu, mmenitegemeza kwa kuandika barua nyingi na kupiga simu mara nyingi. Nina uhakika kwamba hamtakata tamaa na kukosa tumaini kwamba siku moja tutakuwa pamoja tena tukiwa familia.

Pia ningependa kuwashukuru marafiki wangu wengi walio ulimwenguni pote. Mmenitegemeza na barua zenu, maneno yenye kutia moyo, picha maridadi, na zawadi. Vitu hivyo vyote vimenisaidia kujua kwamba siko peke yangu na kwamba nina familia kubwa ulimwenguni pote.

Marafiki wapendwa, ningependa mjue kwamba kila barua, iwe kubwa au ndogo, imenitia moyo na kuniimarisha. Tafadhali msivunjike moyo ikiwa siwezi kujibu barua zenu. Nitawatafuta, niwashukuru, na kuwakumbatia wakati ujao—Naahidi hilo!

Pia ningependa kushukuru Ubalozi wa Denmark jijini Moscow na wafanyakazi wake wote. Mlikuja kusikiliza kesi yangu mara nyingi na mkanitembelea nikiwa mahabusu mara kadhaa. Ushauri wenu umenisaidia, pamoja na mwongozo wenu, na ninathamini sana kitia-moyo chenu. Ninathamini jinsi mlivyonitegemeza na kunisaidia.

Pia ningependa kuishukuru Mahakama ya Rufaa kwa kuniruhusu kuwepo wakati wa kesi hii. Niliposikiliza kesi kwa kuunganishwa na video nikiwa mahabusu, ilikuwa vigumu kwangu kusikia kila kitu kilichosemwa. Nilikisia nusu ya mambo yaliyozungumziwa. Hilo halikunisaidia kujitetea kwa njia inayofaa. Pia unapounganishwa kupitia video ukiwa mahabusu, unaketi ndani ya seli kama mnyama aliyefungiwa ndani ya zoo. Ninaiona hiyo kuwa njia isiyofaa na isiyo ya kibinadamu ya kushughulika na watu katika karne ya 21.

Kufikia sasa, nimekuwa mahabusu kwa miaka miwili hivi, na kesi hii imekuwa ikiendelea kwa miezi 15 tayari. Ili kustahimili hayo yote, kutokata tamaa, na kutovunjika moyo, ni muhimu kuwa na nguvu zisizo za kawaida. Katika Biblia, Wafilipi sura ya 4, na mstari wa 13 unasema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”  a Katika kitabu cha Isaya sura ya 12, na mstari wa 2 tunasoma hivi: “Tazama! Mungu ni wokovu wangu. Nitamtumaini nami sitaogopa; kwa maana Yah Yehova ni nguvu zangu na uwezo wangu, naye amekuwa wokovu wangu.””

Wakati huo wote nimehisi kwamba Mungu wangu Yehova yupo kando yangu akinipa nguvu za kuvumilia haya yote; nguvu ili nisikate tamaa, nisivunjike moyo, niwe na shangwe na furaha, na niendelee kutabasamu. Ninathamini sana hilo, na ninajivunia kumtumikia nikiwa Shahidi wa Yehova.

Watu wengi wameniuliza jinsi kesi hii ya uhalifu ilivyoniathiri. Bila shaka, si rahisi kuwa mahabusu kwa muda mrefu kama huu, kutenganishwa na mke wangu, na kukosa ushirika wa karibu pamoja na watu wa familia yangu na marafiki. Kwa miaka miwili sasa, nimeishi maisha ya upweke sana. Unaweza sema nilikuwepo kimwili tu. Nimetumia saa 23 kati ya saa 24 kila siku nikiwa katika seli ya mita 3 kwa mita 6 hivi. Kwa saa moja kila siku nilitembea katika eneo la kufanya mazoezi, hilo pia ni la mita 3 kwa mita 6, lakini angalau nilikuwa nimetoka nje. Katika kipindi hicho, nimekutana na watu mbalimbali na kuwa na mazungumzo mengi yenye kupendeza. Nilitambua kwamba wengi wao walikuwa wakitamani kesi zao zifanyiwe uchunguzi na kusikilizwa kwa haki. Wengi wao wanahisi kwamba hakuna anayewasikiliza, kama nilivyohisi kwa miaka miwili ambayo nimekuwa hapa. Nimejaribu kuwaimarisha na kuwatia moyo kadiri nilivyoweza, kwa sababu nina uhakika kwamba Yesu Kristo angefanya vivyo hivyo.

Nimepata marafiki wengi wapya. Baadhi yao wamekuja kusikiliza kesi; wengine wameniandikia barua. Ninawajua wengine kibinafsi, lakini wengine siwafahamu bado. Baadhi yao wana imani ya kidini kama yangu; wengine wana imani tofauti. Lakini wamenitegemeza kwa sababu hawawezi kustahimili ukosefu wa haki unaotendeka hapa nchini Urusi, ambako watu fulani wanajaribu kusema kwamba Mashahidi wa Yehova—raia wenye amani wanaowapenda majirani wao kama wanavyojipenda—ni wahalifu na watu wenye msimamo mkali. Hilo halipatani na akili hata kidogo na linashangaza. Wengi wanashtuka kwamba mambo kama hayo yanafanyika hapa nchini Urusi katika karne ya 21.

Watu fulani wameuliza kesi hii ya uhalifu imeathirije imani yangu. Kwa sababu ya kesi hii ya uhalifu, imani yangu imeimarishwa na nimejionea kile kilichoandikwa katika Biblia barua ya Yakobo sura ya 1, mstari wa 2-4: “Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapopata majaribu mbalimbali, mkijua kwamba sifa iliyojaribiwa ya imani yenu hutokeza uvumilivu. Lakini acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.”

Mimi si mkamilifu, lakini nimejifunza kuvumilia na kudumisha shangwe ninapojaribiwa. Na la muhimu zaidi ni kwamba nimemkaribia Mungu wangu Yehova hata zaidi. Ninahisi tamaa kubwa zaidi kuwaambia wengine kumhusu na kuhusu kusudi lake; tamaa kubwa zaidi ya kuendelea kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu, suluhisho pekee la matatizo ya wanadamu; tamaa kubwa zaidi ya kuwatangazia wengine habari njema kutoka kwa Biblia kuhusu amani na uzima wa milele katika Paradiso duniani, kuwasaidia wamkaribie Muumba na kusitawisha imani yenye nguvu katika yeye na ahadi zake.

Maneno haya yanaitwa “Maneno ya mwisho ya kujitetea,” na huenda haya ndiyo maneno ya mwisho mtakayosikia kutoka kwangu leo. Huenda hii ni awamu ya mwisho ya kesi ya uhalifu na itahitimisha miaka miwili ya maisha yangu hapa. Lakini ningependa kuwahakikishia kwamba haya si maneno yangu ya mwisho kuhusu kesi hii na ukosefu wa haki nchini Urusi dhidi ya watu wenye amani na wasio na hatia. Ndiyo nimeanza tu, na bado nina mengi ya kuwaambia hadharani. Sitanyamaza, kana kwamba nina hatia au ninaficha kitu fulani. Nina dhamiri safi—sijafanya kosa lolote, sijavunja sheria za nchi ya Urusi, na sina chochote cha kuaibikia.

Mambo yanayonipata na kuwapata Mashahidi wa Yehova wengine hapa nchini Urusi—mashtaka ya uwongo ya kuwa na msimamo mkali, kuhojiwa, kukamatwa, kupekuliwa, kuporwa mali zetu, kufanyiwa uchunguzi, kutishwa, na sasa hata kuteswa—hayo ndiyo mambo ya kuaibikia. Bila shaka hayo ni mambo ya kuaibisha. Ukweli hudhihirika sikuzote na haki itashinda mwishowe. Katika Biblia, Wagalatia sura ya 6, mstari wa 7 inasema: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”

Mahakama ya chini ilinihukumu kifungo cha miaka sita, lakini kwa kufanya nini? Hakuna! Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba nimefanya kosa lolote. Kinyume chake, kuna uthibitisho mwingi kwamba nilitumia haki nilizoruhusiwa na Kifungu cha 28 cha Katiba ya Shirikisho la Urusi. Ninafuata sheria ya serikali ya Urusi, mimi ni mnyoofu. Mimi ni Mkristo, Shahidi wa Yehova, na ninawapenda Warusi. Kwa nini ninaadhibiwa? Kwa nini ninahukumiwa kifungo cha miaka sita gerezani? Hakuna sababu. Huu ni ukosefu wa haki.

Ninatumaini kabisa kwamba mahakama ya rufaa itatetea sheria leo na kuhakikisha kwamba haki inatekelezwa. Ninatumaini kwamba mahakama hii itakomesha mateso ya kidini hapa nchini Urusi. Ninatumaini sana kwamba mahakama ya rufaa itaufanya ulimwengu wote ujue kwamba hapa nchini Urusi kila mtu ana uhuru wa kidini.

Hivi karibuni, maneno haya ya Mika sura ya 4, mstari 3 na 4 yatatimizwa: “Atatekeleza hukumu miongoni mwa mataifa mengi . . . Watafua panga zao ziwe majembe ya plau na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.”

Sikuzote Mungu huhukumu kwa haki, na hakutakuwa na kutoelewana, jeuri, au vita chini ya utawala wake. Badala yake, kutakuwa na amani na hakutakuwa na mahangaiko. Kwa maneno mengine, wanadamu wote watakuwa na furaha ya kweli.

Mheshimiwa, kupitia uamuzi wako leo, unaweza kuchukua hatua kubwa itakayotuelekeza huko, upande wa haki na amani; hatua kubwa upande wa ulimwengu usio na woga, huzuni, na ukosefu wa haki. Natumaini kwamba utachukua hatua hiyo. Natanguliza shukrani zangu!

a Dennis alinukuu tafsiri ya Kirusi ya synodal. Hata hivyo, katika tafsiri yetu tumetumia Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.