Hamia kwenye habari

Dada Yuliya Kaganovich

FEBRUARI 11, 2021
URUSI

Kujitayarisha Kulimsaidia Dada Yuliya Kaganovich Kuvumilia Mateso

Kujitayarisha Kulimsaidia Dada Yuliya Kaganovich Kuvumilia Mateso

Hukumu Inatarajiwa

Februari 18, 2021, a Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi inatarajiwa kutangaza uamuzi wake katika kesi inayomhusu Dada Yuliya Kaganovich. Bado mwendesha-mashtaka hajatuma ombi la hukumu yake.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Yuliya Kaganovich

  • Alizaliwa: 1966 (Mikhaylovka, Eneo la Volgograd)

  • Maisha Yake: Alisomea kuwa mhandisi ujenzi. Alipokuwa kijana, alijifunza kucheza dansi, akahitimu shule ya muziki, akacheza ala ya muziki katika okestra, na akaimba katika kwaya. Mume wake Aleksandr si Shahidi, lakini anamuunga mkono Yuliya na anaamini kwamba kesi ya uhalifu dhidi yake ni ukosefu mkubwa wa haki.

    Baada ya kufiwa na wapendwa wake alianza kutafakari kuhusu kusudi la uhai. Majibu ya Biblia yalimsaidia kuwa na amani na tumaini. Alibatizwa mnamo 1998. Kanuni za Biblia zimemsaidia kuimarisha ndoa yake, kuboresha uhusiano wake na wengine, na kumlea mwana wake Artur, ambaye ni Shahidi wa Yehova pia.

    Ana matatizo ya afya na kesi hiyo ya uhalifu inazidi kudhoofisha afya yake.

Historia ya Kesi

Dada Yuliya Kaganovich anasema hivi: “Mlango wangu ulipobishwa mapema asubuhi, nilijua mara moja ni akina nani. Moyo wangu ulikuwa ukidunda kwa kasi, na nilijikuta nikirudia-rudia maneno haya: ‘Yehova nisaidie. Yehova nisaidie.’”

Dada yetu mwenye umri wa miaka 53 alianza kuteswa kwa sababu ya dini yake Oktoba 10, 2019 katika jiji la Birobidzhan, Urusi. Upekuzi huo uliofanywa asubuhi sana katika nyumba ya Yuliya ulikuwa sehemu ya uvamizi uliofanywa na maofisa wa Urusi wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB). Walivamia nyumba zaidi ya 20 za ndugu na dada zetu katika eneo hilo.

Uvamizi huo uliwaletea mkazo mkubwa sana, lakini Yuliya na Mashahidi wengine waliendelea kuwa imara kwa sababu walikuwa wamejitayarisha.

Yuliya anasema hivi: “Mara nyingi kwenye mikutano tulisema kwamba kunaweza kuwa na upekuzi, hivyo tunahitaji kujitayarisha. Kwa kuwa nilijua kinachoweza kutokea, nilijitayarisha kiakili jinsi nitakavyotenda na mambo nitakayosema.” Anaongezea hivi: “Nilitambua jinsi ilivyo muhimu sana kufikiria mapema mambo ya kufanya. Kwa sababu hiyo, nilifaulu kufikiria upesi badala ya kuchanganyikiwa na kuwa na wasiwasi, bila kujua jambo la kufanya.”

Kama ilivyotarajiwa, wenye mamlaka wa Urusi walifungua kesi ya uhalifu mara tu baada ya uvamizi huo. Yuliya na wengine walishtakiwa kwa kushiriki katika utendaji unaodaiwa kuwa wenye msimamo mkali.

Machi 3, 2020, maofisa walipeleka kesi hiyo kwenye Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan. Kesi iliahirishwa kwa miezi mitano kwa sababu ya ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19). Yuliya alirudi mahakamani Oktoba 22, 2020.

Yuliya anasema: “Kwa upande mmoja, sikutaka kuwa katika hali hiyo. Lakini kwa upande mwingine, nilikuwa na shangwe kutetea enzi kuu ya Yehova.”

Anasema hivi: “Andiko la Isaya 41:10 lilinifaa sana. Nilichapisha mstari huo na kuubandika nyumbani kwangu ili niendelee kukumbuka maneno hayo kutoka kwa Yehova Mungu yenye kunipa uhakika. Nimejionea Yehova akiimarisha magoti yangu yanayotetemeka.”

Yuliya alijitahidi sana kukariri maandiko kadhaa yaliyomsaidia kuendelea kuwa mtulivu, jasiri, na mwenye shangwe licha ya hali hizo zenye mkazo.

Sisi sote na tutende kwa hekima sasa kwa kujitayarisha kiakili, kihisia, na kiroho kwa ajili ya majaribu yatakayotupata wakati ujao. Tuna uhakika kwamba “Yehova hatawanyima jambo lolote jema Wale wanaotembea kwa utimilifu.”—Zaburi 84:11.

a Inaweza kubadilika.