Hamia kwenye habari

Ndugu Anton Ostapenko

APRILI 28, 2021
URUSI

Kusali na Kuimba Nyimbo za Ufalme Kulimtegemeza Ndugu Anton Ostapenko Alipokuwa Mahabusu

Kusali na Kuimba Nyimbo za Ufalme Kulimtegemeza Ndugu Anton Ostapenko Alipokuwa Mahabusu

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Imemhukumu Ndugu Ostapenko

Oktoba 25, 2021, Mahakama ya Jiji la Sharypovo katika Eneo la Krasnoyarsk ilimhukumu Ndugu Anton Ostapenko kifungo cha nje cha miaka sita na miezi mitatu. Hahitaji kwenda mahakamani wakati huu.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Anton Ostapenko

  • Alizaliwa: 1991 (Ekibastuz, Kazakhstan)

  • Maisha Yake: Anafanya kazi ya kukagua matanki ya kupasha maji joto katika kituo cha kuzalisha umeme. Yeye na dada yake, walifundishwa kweli ya Biblia na mama yao walipokuwa vijana. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova katika mwaka wa 2005

    Alifunga ndoa na Natalya mnamo 2015. Wanapenda kuteleza kwenye theluji. Pia Anton anapenda kupiga gitaa, kuvua samaki, na kucheza tenisi

Historia ya Kesi

Aprili 19, 2019, wenye mamlaka katika jiji la Sharypovo walifanya upekuzi katika nyumba kumi za Mashahidi wa Yehova na kuwahoji ndugu na dada waliokuwemo. Ndugu Anton Ostapenko alikamatwa na kuwekwa mahabusu hadi alipoachiliwa Desemba 20, 2019. Alishtakiwa kwa kupanga utendaji wa shirika “lenye msimamo mkali.”

Katika miezi sita ambayo Anton alikuwa kizuizini, kuna pindi chache ambazo aligeuka kutoka kwenye kamera ya usalama na kwenda kwenye beseni la kunawia katika jela alilokuwemo na kulia kwa huzuni.

Sala ndiyo njia kuu iliyomsaidia kupata nguvu. Anton anaeleza hivi: “Nilimsihi Yehova anisaidie kusitawisha uvumilivu.” Anaongezea kusema hivi: “Nilikuwa na mengi ya kujifunza. Kiroho, nilianza kuwa imara zaidi. . . . Inapendeza kwamba unapojikuta katika hali ngumu [kama hii], ni kana kwamba unalazimika kuanza kutumia mambo uliyokuwa ukisoma. Kwa sababu si sikuzote utakuwa na Biblia katika jela lako. Kwa hiyo, kabla ya kukamatwa, nilisoma tu kumhusu Yehova. Lakini hapo [gerezani] Yehova alinionyesha kikamili yeye ni Mungu wa aina gani. Nilifurahi sana kumfahamu kabisa. Hakuwa tu Mungu Mweza-Yote bali alikuwa kwangu kama Baba mwenye upendo ambaye anaelewa kikweli hali zangu na ambaye anatoa msaada na utegemezo katika njia ambazo hata sikuwa nimewahi kuwazia na kwa wakati unaofaa kabisa.”

Nyimbo za Ufalme zilimtia moyo pia. “Mimi na mke wangu tulikuwa na kawaida ya kuimba pamoja, na hilo lilitusaidia kukariri nyimbo hizo. Hilo lilinisaidia sana nilipokuwa mahabusu. Baada ya taa kuzimwa, nilifurahia sana kusali na kuimba wimbo, na hilo lilinisaidia kulala nikiwa na moyo mtulivu.”

Anton anaposubiri uamuzi wa kesi yake, anaweza kuendelea kufanya kazi ya kimwili. Hata hivyo, haruhusiwi kuondoka eneo la Sharypovo. Vizuizi hivyo vinamfanya asiweze kumpeleka mama yake hospitalini kila mara anapoenda kufanyiwa uchunguzi.

Tunasali tukiwa una uhakika kamili kwamba Yehova ataendelea kuwapa amani ndugu zetu wanaovumilia mateso.—Yohana 14:27.