Hamia kwenye habari

Dada Anastasiya Sycheva

JANUARI 22, 2021
URUSI

Mahakama Nchini Urusi Yamhukumu Dada Anastasiya Sycheva kwa Kuhudhuria Mikutano

Mahakama Nchini Urusi Yamhukumu Dada Anastasiya Sycheva kwa Kuhudhuria Mikutano

Hukumu

Januari 21, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Obluchenskiy katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilimhukumu Dada Anastasiya Sycheva. Alihukumiwa miaka miwili ya kifungo cha nje. Hatahitaji kwenda gerezani kwa sasa.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Anastasiya Sycheva

  • Alizaliwa: 1977 (Teploozyorsk, Eneo Lililotengewa Wayahudi)

  • Maisha Yake: Alikuwa na ndugu wanne, ndugu wawili tayari wamekufa. Alihitimu chuo cha tiba na kupata shahada ya uuguzi. Alifanya kazi katika hospitali ya meno kisha akaajiriwa katika hospitali inayotibu magonjwa ya akili. Baada ya dada yake mkubwa kufa, alikubali kuwatunza watoto wawili wa dada huyo. Alimtunza mama yake hadi alipokufa baada ya kuugua kwa muda mrefu

    Alipokuwa kijana, alitafakari sana kuhusu jinsi uhai ulivyo mfupi. Kufanya hivyo kulimchochea aanze kuichunguza Biblia. Alipofanya hivyo alipata majibu ya maswali yake. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1994

Historia ya Kesi

Oktoba 2019, wenye mamlaka nchini Urusi walimweka Anastasiya katika orodha ya watu “wenye msimamo mkali.” Septemba 25, 2019, Idara ya Upelelezi ya Usalama wa Taifa (FSB) ya Birobidzhan, ilifungua kesi ya uhalifu dhidi ya Anastasiya. Alishtakiwa kwa kuendelea kimakusudi na shughuli za shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova kwa kushiriki katika mikutano ya kidini na kuwaambia wengine kuhusu imani yake.

Wakati wa kesi, upande wa mashtaka ulicheza rekodi za sauti na video za Anastasiya akizungumza na simu na zilizoonyesha mikutano aliyohudhuria. Upande wa mashtaka ulidai kwamba rekodi hizo zinamwonyesha dada yetu akijihusisha na utendaji wa “msimamo mkali.” Anastasiya alitumia rekodi hizo kutoa ushahidi. Alisema kwamba katika mikutano ya Mashahidi wa Yehova, watu hufundishwa jinsi ya kuwa na huruma, rehema, subira, na sifa nyingine za Kikristo.

Mambo aliyosema mwishoni mwa kesi yake yalimwezesha Anastasiya kufafanua jinsi Biblia ilivyomsaidia maishani mwake. Alisema hivi kwa sehemu: “Leo, ninahukumiwa kwa sababu ya imani yangu na kwa kuendelea na utendaji wangu wa kidini, yaani, kusoma Biblia, kukutana pamoja na rafiki zangu na kuzungumzia Maandiko, kuimba nyimbo za kumsifu Yehova, na kusali kwake.

“Ninawezaje kukataa kutii amri inayopatikana katika barua ya Waebrania sura ya 10, mstari wa 24 na 25? Ninanukuu: ‘Na acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.’ Ikiwa Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova mwenyewe, ananiambia nikutane pamoja na rafiki zangu, waamini wenzangu, ili kusoma Biblia, kutiana moyo na kutendeana kwa fadhili, ninawezaje kukataa kutii? Ninampenda sana, ninamheshimu, na ninamwabudu Yeye.”

Tunafurahi kusikia jinsi Anastasiya alivyotetea imani yake kwa ujasiri na kuonyesha kwamba yuko imara na ni mwenye uhakika. Tunasali kwamba aendelee kudumisha shangwe yake na kwamba jaribu hili la imani analokabili, liendelee kuimarisha uvumilivu wake.—Yakobo 1:2, 3.