Hamia kwenye habari

Andrey na mke wake, Svetlana, wakiwa nje ya mahakama baada ya kutolewa kwa uamuzi wa kumwachilia huru kutoka kwenye kifungo cha nyumbani

AGOSTI 22, 2019
URUSI

Mahakama ya Rufaa Yaamuru Ndugu Andrey Suvorkov Aachiliwe Huru Kutoka Kwenye Kifungo cha Nyumbani

Mahakama ya Rufaa Yaamuru Ndugu Andrey Suvorkov Aachiliwe Huru Kutoka Kwenye Kifungo cha Nyumbani

Agosti 13, 2019, mahakama ya rufaa katika jiji la Kirov iliamuru Ndugu Andrey Suvorkov mwenye umri wa miaka 26 aachiliwe huru kutoka kwenye kifungo cha nyumbani. Ingawa Ndugu Suvorkov amepewa uhuru zaidi, bado yuko chini ya vizuizi vya kisheria.

Kama ilivyoripotiwa awali, Ndugu Suvorkov alikamatwa pamoja na baba yake wa kambo na ndugu wengine watatu wakati polisi wa eneo hilo na kikosi maalumu cha polisi waliofunika nyuso zao walipovamia nyumba 19 jijini Kirov Oktoba 9, 2018.

Ndugu Suvorkov anasema hivi anapokumbuka wakati ambapo nyumba yake ilipekuliwa: “Vitu vyetu vingi vyenye thamani vilichukuliwa. Lakini mimi na mke wangu hatukuwa na wasiwasi kwa sababu sikuzote tumejitahidi kuishi maisha rahisi na kutopenda sana vitu vya kimwili. Pia, shauri lililo kwenye Mathayo 6:21, linalosema ‘mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa,’ lilitusaidia kuwa watulivu.”

Baada ya uvamizi huo, Ndugu Suvorkov, baba yake wa kambo na wale ndugu wengine watatu walifunguliwa kesi za uhalifu kwa sababu ya kuimba nyimbo za Ufalme, kusoma vitabu vya kidini, na kumiliki nakala ya Kirusi ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Wote waliwekwa mahabusu wakisubiri mahakama ifanye uamuzi ama wa kuwaachilia huru au kuendelea kubaki mahabusu.

Ndugu Suvorkov anasimulia mambo aliyopitia: “Nilikaa mahabusu kwa siku mbili. Nilikuwa nikisali muda wote. Nilikuwa na uhakika kwamba Yehova atanisikiliza na kunitegemeza. Nilikumbuka muziki wa nyimbo za Ufalme na kuanza kuimba. Baadaye, nilikumbuka maneno ya nyimbo zaidi ya 50.”

Mahakama iliamua kwamba Ndugu Suvorkov na wenzake waendelee kubaki mahabusu. Katika juma la kwanza la kuwa mahabusu, Ndugu Suvorkov alikazia fikira kuwasaidia wengine. Anakumbuka hivi: “Niliamua kuwataja akina ndugu kwa majina katika sala zangu na niliwaandikia barua za kuwatia moyo ndugu wote niliokumbuka anwani zao. Hilo lilifanya niwe na furaha.”—Matendo 20:35.

Kadiri miezi ilivyopita, ndugu wote waliokuwa mahabusu walihukumiwa kifungo cha nyumbani isipokuwa Ndugu Andrzej Oniszczuk. Ndugu Suvorkov ndiye wa kwanza jijini Kirov kuachiliwa kutoka kwenye kifungo cha nyumbani.

Ndugu Suvorkov anasema hivi: “Ninapokumbuka kipindi hicho, ninafurahi sana kwamba nilifungwa gerezani. . . . Sijui kitakachotokea wakati ujao, au hata ikiwa nitafungwa tena. Sasa nina uhakika kwamba nitategemezwa na Yehova na tengenezo lake hata ikiwa nitafungwa. Sasa siogopi tena kufungwa gerezani.”