Hamia kwenye habari

Mkutano wa waandishi wa habari uliofanywa jijini Moscow Aprili 1, 2021, uliadhimisha miaka 70 ya uhamisho wa Mashahidi wa Yehova kwa gari-moshi na kupelekwa Siberia

APRILI 5, 2021
URUSI

Mkutano wa Waandishi wa Habari wa Kuadhimisha Miaka 70 ya “Oparesheni Kaskazini” Jijini Moscow

Mashahidi 10,000 Hivi wa Yehova Walihamishiwa Siberia

Mkutano wa Waandishi wa Habari wa Kuadhimisha Miaka 70 ya “Oparesheni Kaskazini” Jijini Moscow

Aprili 1, 2021, mkutano ulifanywa na waandishi wa habari jijini Moscow kuhusu mwadhimisho wa miaka 70 ya ile iliyoitwa Oparesheni Kaskazini, yaani, kazi iliyofanywa mwaka wa 1951 ya kuwahamisha Mashahidi 10,000 hivi wa Yehova kwa gari-moshi kutoka katika jamhuri sita za ule uliokuwa muungano wa Sovieti na kuwapeleka Siberia. Jopo la wasemaji sita, kutia ndani wasomi na watetezi wa haki za kibinadamu, walizungumza na kujibu maswali ya waandishi wa habari. Jopo hilo halikuzungumzia tu mambo yaliyohusiana na Oparesheni Kaskazini bali walihusianisha tukio hilo na mateso yanayoendelea nchini Urusi. Mkutano mzima ulipeperushwa moja kwa moja kwenye Intaneti.

Yaroslav Sivulsky, mwakilishi wa European Association of Jehovah’s Witnesses na ambaye familia yao iliathiriwa moja kwa moja na Oparesheni Kaskazini, alizungumzia kirefu kuhusu hali mbaya waliyokabili wakati wa uhamisho huo. Sivulsky alisema hivi: “Tulipochunguza nyaraka za kihistoria, tuliweza kuthibitisha kwamba jumla ya Mashahidi 9,793 wa Yehova walipelekwa uhamishoni. Idadi hiyo inatia ndani wale waliokufa na kuzaliwa walipokuwa njiani.”

Sergey Ivanenko, msomi wa mambo ya kidini nchini Urusi alizungumzia fungu lililotimizwa na propaganda ya Muungano wa Sovieti dhidi ya Mashahidi wa Yehova wakati wa Oparesheni Kaskazini, na pia fungu lake katika mateso yanayoendelea wakati huu nchini Urusi. Akitoa maelezo kamili, Ivanenko pia alikazia uvumilivu wa Mashahidi kwa kusema hivi: “Sera ya kuwakandamiza Mashahidi wa Yehova, ambayo imetekelezwa na Shirikisho la Urusi tangu 2017, haitakuwa na matokeo yoyote. Mambo tuliyojifunza kutokana na Oparesheni Kaskazini na tunapochanganua mambo yanayoendelea sasa, kutia ndani uimara wa Mashahidi wa Yehova wa kutetea imani yao, kunatuthibitishia jambo hilo. Inaonekana kwamba jambo linalofaa, kwa manufaa ya taifa la Urusi, ni kuanzisha mchakato utakaowaondolea Mashahidi wa Yehova marufuku waliyowekewa.”

Artur Artemyev, msomi wa mambo ya kidini nchini Kazakhstan na mwandishi wa kitabu Jehovah’s Witnesses in Kazakhstan: A Social-Historical and Religious Analysis (kilichorekebishwa mnamo 2020), alisema kwamba hata mbinu kali zaidi za Muungano wa Sovieti hazikuwakomesha Mashahidi wa Yehova wala kudhoofisha bidii yao. Badala yake, idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kazakhstan iliongezeka wakati wa utawala wa Wasovieti. Vivyo hivyo, Valery Borschev mtaalamu wa haki za kibinadamu wa Kikundi cha Moscow Helsinki alisema hivi: “Jambo pekee ambalo mateso hutimiza ni kuwaimarisha Mashahidi wa Yehova. Wenye mamlaka wanahitaji kutambua jambo hilo.”

Valentin Gefter, mshiriki wa Baraza la Wataalamu chini ya Kamishna wa Haki za Kibinadamu nchini Urusi, alizungumzia kichwa “Jinsi Wafungwa wa Dhamiri Wanavyotokea Katika Urusi ya Kisasa.” Mashahidi wanaofungwa nchini Urusi si wafungwa wa kisiasa, bali kwa usahihi zaidi wanapaswa kurejelewa kuwa wafungwa wa dhamiri. Alisisitiza hivi: “Mashahidi wa Yehova hawaipingi serikali.” Aliendelea kusema kwamba imani ya kidini ya Mashahidi inawachochea tu kuchukua msimamo wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Kwa sababu hiyo, wenye mamlaka wanawafunga Mashahidi bila sababu na bila haki.

Msemaji wa mwisho alikuwa Aleksandr Verkhovsky. Yeye ni mshiriki wa Kamati ya Rais ya Haki za Kibinadamu na msimamizi wa Kituo cha Kuchunguza na Kukagua Habari SOVA. Kituo cha SOVA hutafuta na kurekodi kesi zote ambazo sheria kuhusu msimamo mkali ilitumiwa vibaya, kutia ndani kesi zinazohusu Mashahidi wa Yehova. Aliandaa ripoti kuhusu mateso ya sasa nchini Urusi. “Je, kampeni hii dhidi ya Mashahidi wa Yehova itakomeshwa? Hilo ni swali muhimu, lakini hatuna jibu.” Bw. Verkhovsky anasadiki kwamba wakati utafika ambapo lazima wenye mamlaka nchini Urusi wataacha kuwakandamiza Mashahidi wa Yehova. Alitoa mapendekezo kadhaa kwa ajili ya wanaotunga sheria yanayoweza kuwasaidia kurekebisha sheria dhidi ya utendaji wenye msimamo mkali utakaohakikisha nchi inalindwa dhidi ya utendaji wa aina hiyo bila kukiuka haki za watu wanaoabudu kwa amani, kama vile Mashahidi.

Waandishi wa habari waliruhusiwa kuuliza jopo hilo maswali kuhusu mambo yaliyozungumziwa.

Siku hiyohiyo mkutano wa wasomi ulifanywa katika jiji la Chisinau, Moldova. Mkutano huo ulipangwa na Taasisi ya Historia ya Chuo cha Sayansi cha Moldova, Chuo Kikuu cha Taifa cha Alecu Russo kilichoko Balti, na Chuo Kikuu cha Taifa cha Bogdan Petriceicu Hasdeu kilichoko Cahul. Mkutano mwingine umepangwa kufanywa Aprili 9 nchini Ukrainia.