Hamia kwenye habari

Ndugu Albert Batchaev

MEI 24, 2021
URUSI

Ndugu Albert Batchaev Aendelea Kudumisha Uaminifu Wake Akiwa Mahabusu na Katika Kifungo cha Nyumbani

Ndugu Albert Batchaev Aendelea Kudumisha Uaminifu Wake Akiwa Mahabusu na Katika Kifungo cha Nyumbani

Hukumu Inatarajiwa

Mahakama ya Jiji la Circassian iliyo katika Jamhuri ya Karachayevo-Circassian itatangaza hivi karibuni hukumu yake katika kesi inayomhusu Ndugu Albert Batchaev. a

Maelezo Mafupi Kumhusu

Albert Batchaev

  • Alizaliwa: 1976 (Karachayevsk)

  • Maisha Yake: Ana dada watatu na ndugu mmoja. Mama yao alikufa na wanamtunza baba yao mwenye umri mkubwa. Alisomea kuwa mwanasheria katika shule ya kijeshi na alifanya kazi kama mkuu wa wachunguzi wa kesi za uhalifu

    Alijifunza Biblia na kujithibitishia kwamba inasema kweli. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 2004. Alifunga ndoa na Zhanna mwaka wa 2007. Sasa, anafanya kazi ya kuwekea watu milango. Afya yake iliyodhoofika inamfanya asiweze kufanya mambo mengi. Yeye na mke wake wanafurahia kuzunguka na gari na wakati mwingine kutembea kwa miguu kwenye milima iliyo katika eneo lao na pia kufurahia mambo mengine wanayoweza kufanya wakiwa nje

Historia ya Kesi

Desemba 16, 2019, maofisa wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) walifanya upekuzi katika nyumba kumi hivi katika jiji la Cherkessk. Hivyo, ndugu wengi waliwekwa kizuizini.

Siku moja baada ya uvamizi huo, wote waliachiliwa huru isipokuwa Ndugu Albert Batchaev. Aliwekwa kizuizini kwa karibu saa 72 na kushtakiwa kwa kufanya mipango ili wengine waimbe na kusali kwa Yehova. Baada ya kesi hiyo kufunguliwa, rafiki zake na watu wengine wanaoshirikiana naye wameripoti kwamba wamekuwa wakifuatwa na wenye mamlaka.

Albert alisema hivi: “Waliponipeleka mahabusu na kufunga mlango wao mzito wa chuma uliotokeza sauti ukifungwa, na kuufunga kwa mnyororo, nilihisi woga mwingi. Nilifikiri kwamba singewahi kutoka hapo; ningekufa hapo. Nilikuwa na wasiwasi sana kuhusu hali ya mke wangu na ndugu wengine.”

Albert alikaa karibu miezi miwili mahabusu kisha akapewa kifungo cha nyumbani. Lakini baada ya juma moja, alipelekwa tena kizuizini, na akakaa huko kwa majuma saba. Anaeleza hivi: “Nilipokuwa gerezani, hasa nilipowekwa katika kifungo cha upweke, nilijenga uthamini zaidi kuelekea umuhimu wa kuwa na ratiba yangu ya kiroho na wa kuwa na mengi ya kufanya katika kazi za Ufalme. Yalinipa nguvu nilizohitaji ili nisidhoofike na kupoteza imani, uvumilivu, tumaini, au upendo wangu kumwelekea Yehova na wanadamu wengine.”

Aliweza kupata Biblia ingawa mara nyingi hazipatikani gerezani. Albert anaeleza hivi: “Biblia ilinisaidia kuvumilia. Iliniokoa ili nisivunjike moyo kwa sababu ya kuwakosa wale ninaowapenda sana.” Wakati huo, kuliko wakati mwingine wowote, alielewa hisia za watu waaminifu walioandikwa katika Biblia waliokabiliana na hali ngumu na kufungwa gerezani. Anaeleza hivi: “Walikuwa watu halisi, walio hai na walio karibu nami nilipokuwa gerezani. Sasa ninahisi nina rafiki wengi wanaoishi sasa na walioishi zamani.”

Aprili 2020, mahakama ilimhamishia Albert kwenye kifungo cha nyumbani cha miezi miwili mwanzoni. Lakini kifungo hicho kimerefushwa kwa mara nne. Machi 2021, kifungo chake kilirefushwa tena na kinatarajiwa kuisha Juni 2021.

Tunajua kwamba Yehova ataendelea kumwimarisha na kumtunza Ndugu Batchaev na watumishi Wake wote washikamanifu walioshtakiwa.—1 Mambo ya Nyakati 29:12.

a Tarehe ya hukumu haitolewi mapema pindi zote.