Hamia kwenye habari

Ndugu Aleksandr Bondarchuk akiwa na mke wake, Elena, (kushoto) na Ndugu Sergey Yavushkin akiwa na mke wake, Tatiana (kulia)

APRILI 2, 2021
URUSI

Ndugu Aleksandr Bondarchuk na Ndugu Sergey Yavushkin Wanasubiri Uamuzi wa Mahakama Baada ya Kifungo cha Nyumbani

Ndugu Aleksandr Bondarchuk na Ndugu Sergey Yavushkin Wanasubiri Uamuzi wa Mahakama Baada ya Kifungo cha Nyumbani

HABARI YA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yakataa Ombi la Rufaa

Februari 16, 2022, Mahakama ya Eneo la Kemerovo ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Aleksandr Bondarchuk na Ndugu Sergey Yavushkin. Hawatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Juni 22, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Zavodskoy iliyoko Kemerovo ilimhukumu Aleksandr na Sergey kifungo cha nje cha miaka minne.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Aleksandr Bondarchuk

  • Alizaliwa: 1974 (Topki, Eneo la Kemerovo)

  • Maisha Yake: Alikuwa na umri wa miaka 19 baba yake alipokufa. Alisomea jinsi ya kuendesha magari na mashine kubwa zinazotumiwa katika ujenzi. Baadaye alijifunza useremala. Kwa sasa anafanya kazi ya kurekebisha mifumo ya kupasha nyumba joto. Anapenda kuvua, kuteleza kwenye theluji, kuendesha baiskeli, na kukimbia

  • Alifunga ndoa na Elena mnamo 1992. Elena ndiye aliyeanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Ndoa yao iliokolewa kwa sababu ya kutumia kanuni za Biblia. Wana watoto wawili wa kiume.

Sergey Yavushkin

  • Alizaliwa: 1960 (Rubtsovsk, Eneo la Altai)

  • Maisha Yake: Alifanya kazi ya kuchomelea vyuma kwa miaka mingi. Kwa sasa anafanya kazi ya kurekebisha makufuli. Tangu alipokuwa kijana alipenda kucheza gitaa na michezo mingine mbalimbali

  • Alifunga ndoa na Tatiana mnamo 1990. Muda mfupi baada ya hapo, walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kilichowapendeza hasa ni kwamba licha ya Biblia kuwa kitabu cha zamani sana, bado kinafaa leo. Wana mwana mmoja na binti mmoja

Historia ya Kesi

Julai 22, 2019, saa 12:00 asubuhi, maofisa wa usalama walivamia nyumba ya Ndugu Aleksandr Bondarchuk na ya Ndugu Sergey Yavushkin kwa mara ya pili. Hata hivyo, pindi hii ndugu hao walikamatwa na wake zao wakahojiwa. Pia, maofisa hao walichukua vifaa vyao vya kielektroni.

Aleksandr na Sergey walizuiliwa kwa siku mbili. Baadaye, Mahakama ya Wilaya ya Kati iliyoko Kemerovo iliwahukumu kifungo cha nyumbani cha miezi miwili. Kifungo hicho kimeongezwa mara sita.

Wakiwa katika kifungo hicho, ndugu hao hawaruhusiwi kwenda umbali wa mita 300 kutoka kwenye nyumba zao. Hivyo, hawawezi kwenda kazini. Hata hivyo, kabla ya mashtaka hayo ya uhalifu, ndugu hao wawili walikuwa wamejitengenezea jina zuri katika jamii na mbele ya waajiri wao. Kwa sababu hiyo, waajiri wa ndugu hao walimpigia simu mpelelezi anayeshughulikia kesi yao wakiomba ndugu hao waruhusiwe kusafiri. Maombi ya waajiri wao yalikataliwa.

Aleksandr na familia yake wameona jinsi Yehova amewasaidia mara kadhaa. Kwa kuwa hawezi kwenda kazini na akaunti zao za benki zimefungwa, hali yao ya kiuchumi ni ngumu. Hata hivyo, anasema hivi: “Kesi hii imenifundisha kumtegemea na kumtumaini Yehova hata zaidi. Inaonekana kwamba huenda hapo awali, si pindi zote nilipotambua mkono wa Yehova ulipokuwa ukinisaidia, lakini sasa ninaona kwamba Yehova ananisaidia kila saa, kila siku. Hajawahi kuniacha mimi na familia yangu bila utegemezo na upendo wake.”

Kesi ya uhalifu imemletea Sergey mkazo na mahangaiko mengi. Kwa sababu hiyo, alipatwa na kiharusi. Licha ya tatizo hilo la afya, amedumisha mtazamo mzuri. Anasema hivi: “Tunahitaji kuyaona matatizo ya muda ambayo yanatupata sasa kuwa mambo madogo, ingawa si rahisi nyakati zote kuvumilia kila jambo linalotupata.”

Andiko la 1 Wakorintho 15:58 linamwimarisha sana Sergey kwa kuwa linasema kwamba “kazi yenu si ya bure kuhusiana na Bwana.” Sergey anasema hivi: “Yehova anakumbuka kila kitu, na sikuzote atakumbuka kazi nzuri tunazofanya.”

Tunasali kwa ajili ya ndugu na dada zetu nchini Urusi ambao kwa subira wamekuwa wakivumilia mateso kwa miaka mingi. Tunasali kwamba waendelee kupata faraja na nguvu kupitia Neno la Mungu linalosema hivi: “Yehova anafurahishwa na wale wanaomwogopa, wale wanaongojea upendo wake mshikamanifu.”​—Zaburi 147:11.