Hamia kwenye habari

Ndugu Anatoliy Vilitkevich akiwa na mke wake, Alyona

APRILI 7, 2021
URUSI

Ndugu Anatoliy Vilitkevich Anaendelea Kuwa Imara Anaposubiri Hukumu

Ndugu Anatoliy Vilitkevich Anaendelea Kuwa Imara Anaposubiri Hukumu

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yamhukumu Ndugu Vilitkevich

Septemba 27, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Leninskiy huko Ufa ilimhukumu Ndugu Anatoliy Vilitkevich kifungo cha nje cha miaka miwili. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Anatoliy Vilitkevich

  • Alizaliwa: 1986 (Eneo la Khabarovsk)

  • Maisha Yake: Anafanya kazi akiwa seremala. Alifunga ndoa na Alyona mnamo 2008. Wanapenda kupiga kambi na kwenda matembezi

    Wazazi wake walimsaidia kumpenda Muumba alipokuwa kijana. Alipenda hasa ahadi kwamba siku moja wanadamu na wanyama wataishi pamoja kwa amani. Alibatizwa mnamo 1997 akiwa na umri wa miaka 11

Historia ya Kesi

Agosti 8, 2018, jina la Ndugu Anatoliy Vilitkevich liliongezwa kwenye orodha ya watu wanaoshukiwa kuwa magaidi nchini Urusi. Akiwa pamoja na Ndugu Dennis Christensen, Anatoliy alikuwa mmoja kati ya Mashahidi wa kwanza kuwekwa mahabusu baada ya Mahakama Kuu ya Shirikisho la Urusi kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova mnamo Aprili 2017.

Wapelelezi waliweka kamera kisiri katika nyumba ya Anatoliy na Alyona. Wapelelezi hao walimrekodi Anatoliy akifanya “uhalifu” wa kuongoza mazungumzo ya Biblia pamoja na rafiki zake. Sasa ameshtakiwa kwa kupanga utendaji wa shirika linalodaiwa kuwa lenye msimamo mkali.

Anatoliy alipokamatwa na polisi, ofisa mmoja alimwambia Alyona kwa dharau ‘atafute mume mpya.’ Anatoliy anasema kwamba alipokuwa akihojiwa alipatwa “na mkazo mwingi sana wa kihisia. Waliniambia kwamba ikiwa sitakubali mashtaka, mke wangu pamoja na wote waliokuwa nyumbani kwetu kwa ajili ya mikutano hiyo watapatwa na madhara mengine. Niliambiwa mara nyingi sana kwamba mke wangu atafungwa pia. Pindi hizo nilisali kwa Yehova na kumwomba anipe amani ya akili.”

Anatoliy amevumilia miezi miwili mahabusu, miezi tisa ya kifungo cha nyumbani, na zaidi ya mwaka mmoja na nusu ya vizuizi vya kusafiri. Alipokuwa gerezani, aliandika katika kitabu mifano iliyo katika Biblia ya wale ambao pia walivumilia mateso. Anasema hivi: “Nilikumbuka kwamba Yehova hakuzuia wasipatwe na matatizo, lakini wakati huohuo hakuwaacha kamwe. Hilo liliniimarisha sana na kunihakikishia kwamba Yehova atanitendea kwa njia hiyohiyo. Jambo kuu ni kuendelea kuwa mshikamanifu.” Barua ambazo mke wake alimwandikia zilimtia moyo sana. Anatoliy anasema hivi: “Katika barua moja aliyonitumia mwanzoni, Alyona aliweka picha kadhaa tulizopiga na marafiki na wapendwa wetu. Kila jioni nilitazama picha hizo na kujaribu kukumbuka kitu kinachopendeza kilichotukia katika yangu na mtu niliyekuwa nikimtazama katika picha. Hilo lilinisaidia kuhisi wako pamoja nami.”

Mifano ya uaminifu ya Anatoliy na Alyona inatutia moyo sisi sote. Tunashangilia kujua kwamba ndugu na dada zetu nchini Urusi wanaendelea kumkaribia Yehova licha ya mateso makali. Tunamshukuru Yehova kwa kusikiliza sala zetu kwa ajili yao.—2 Wakorintho 1:11.