Hamia kwenye habari

Ndugu Andrey Andreyev (katikati) akiwa pamoja na (kuanzia kushoto kwenda kulia) binti yake, Albina; mke wake, Svetlana; binti yake, Anzhelika na mume wake, Anatoliy; (picha ndogo) Ndugu Andreyev akimkumbatia mke wake baada ya kuachiliwa kutoka gerezani

FEBRUARI 27, 2023
URUSI

Ndugu Andrey Andreyev Aachiliwa Kutoka Gerezani Nchini Urusi

Ndugu Andrey Andreyev Aachiliwa Kutoka Gerezani Nchini Urusi

Februari 22, 2023, Ndugu Andrey Andreyev aliachiliwa kutoka gerezani nchini Urusi baada ya kukaa mahabusu kwa zaidi ya miaka mitatu.

Oktoba 16, 2019, Andrey pamoja na ndugu wengine walikamatwa na kuhojiwa baada ya msako mkubwa wa kutafuta Mashahidi wa Yehova katika jiji la Kursk. Alikaa mahabusu kwa zaidi ya miezi 20 akisubiri kesi yake ianze kusikilizwa, baadaye, Juni 3, 2021, alihukumiwa kifungo cha gerezani.

Katika kipindi ambacho Andrey alikuwa gerezani kwa sababu ya imani yake, Andrey alifanya yote anayoweza ili kukidhi mahitaji ya kiroho ya mke wake, Svetlana, na mabinti wao wawili, Anzhelika na Albina. Aliwaandikia barua na katika barua hizo alikuwa na kawaida ya kuwapatia kitia-moyo kinachotegemea Biblia, hata aliandika hotuba ya harusi kwa ajili ya binti yake, Anzhelika, ambaye aliolewa Andrey alipokuwa gerezani. Anzhelika anasema hivi: “Aliandika hotuba inayogusa moyo, nzuri sana. Ilichochea hisia za wageni tuliowaalika . . . tulihisi kana kwamba alikuwa pamoja na sisi siku hiyo.”

Familia ya Andrey ilisafiri kwa saa nane kwa basi ili kumtembelea. Ingawa safari hiyo haikuwa rahisi, Svetlana anasema kwamba yeye pamoja na mabinti wake walitegemezwa na Mashahidi wanaoishi karibu na gerezani. Waliwasaidia kupata sehemu ya kulala, chakula, na waliwapeleka hadi gerezani. Wakati mwingine Mashahidi hao hata walisimama usiku kucha kwenye foleni ya wageni wanaotembelea wafungwa ili Svetlana na mabinti wake waweze kumwona Andrey kesho yake.

Watu wa familia pamoja na marafiki wa Ndugu Andreyev walioenda kumpokea baada ya kuachiliwa kutoka gerezani

Licha ya kwamba Andrey alitendewa kikatili alipokuwa gerezani, bado ana hali nzuri sana ya kiroho. Utu wake wa Kikristo ulimsaidia kuheshimiwa na wenye mamlaka, na kwa sababu ya mwenendo wake mzuri walimruhusu kuwa na wageni wengi zaidi. Andrey anasema hivi kuhusu kifungo chake cha gerezani: “Sijaweka kinyongo, sina hasira, wala sina chuki kumwelekea mtu yeyote. Kwa msaada wa Mungu, nimefanikiwa na hilo linanifanya niwe na furaha.”

Kwa sababu, Andrey aliendelea kuonyesha upendo wa Kikristo bila kuchoka, tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kubariki roho hiyo.​—1 Yohana 4:16.