Hamia kwenye habari

Ndugu Andrey Gubin

APRILI 5, 2021
URUSI

Ndugu Andrey Gubin Anadumisha Uaminifu Anapokabili Kesi ya Imani Yake

Ndugu Andrey Gubin Anadumisha Uaminifu Anapokabili Kesi ya Imani Yake

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yamhukumu Ndugu Gubin

Septemba 9, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi ilimhukumu Ndugu Andrey Gubin kifungo cha nje cha miaka miwili na miezi sita. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Andrey Gubin

  • Alizaliwa: 1974 (Jiji la Saran, Kazakhstan)

  • Maisha Yake: Ana ndugu na dada wenye umri mkubwa. Alipokuwa kijana, alifanya kazi ya muda baada ya shule ya kutengeneza funguo na kufuli ili kuitegemeza familia yao. Baadaye, alifanya kazi ya kuendesha mashine kubwa za ujenzi. Anapenda michezo, kuandika mashairi, na kupiga ala za muziki

  • Tangu alipokuwa kijana, alisikitishwa na ukosefu wa haki na uovu uliopo ulimwenguni. Alipata amani na kusudi maishani baada ya kujifunza Biblia. Ahadi ya Biblia ya kurudisha haki na amani kwa wanadamu ilimchochea kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Alibatizwa katika mwaka wa 1991 akiwa na umri wa miaka 17. Alifunga ndoa na Tatyana mnamo 2007. Alihamia Birobidzhan katika mwaka wa 2011

Historia ya Kesi

Februari 12, 2020, maofisa wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) walianza kumpeleleza Ndugu Andrey Gubin. Septemba 17, 2020 kesi yake ya uhalifu ikaanza kusikilizwa.

Kesi hiyo ni moja tu katika kesi nyingine 19 za uhalifu dhidi ya ndugu na dada zetu katika Eneo Lililotengewa Wayahudi. Kesi hizo zinatokana na uvamizi mkubwa wa nyumba za ndugu zetu ulioitwa “Siku ya Hukumu.” Mei 17, 2018, maofisa 150 wa usalama walifanya upekuzi katika nyumba 22 za Mashahidi wa Yehova. Wenye mamlaka walichukua kadi za benki, pesa, picha, kompyuta, na vifaa vya kielektroni.

Wenye mamlaka wamemzuia Andrey na Tatyana wasitumie akaunti zao za benki. Kwa sababu hiyo, wamekabili hali ngumu sana ya kiuchumi. Kesi hiyo, ambayo imendelea kwa miezi kadhaa, imeathiri sana afya ya Tatyana. Hata hivyo, wenzi hao wa ndoa wamefarijika sana kwa kusoma Biblia kwa ukawaida. Wamenufaika sana kutokana na ushauri wa Biblia wa kukabiliana na hali ngumu.

Uhakika wa Andrey katika Yehova na tengenezo Lake umeimarishwa kutokana na utegemezo mwingi ambao amepata kutoka kwa ndugu na dada zake wa kiroho. Kwa mfano, siku moja Andrey alikuwa na wasiwasi kuhusu hali yake. Alimweleza hisia zake ndugu mmoja ambaye pia ameshtakiwa kuwa mhalifu. Ndugu huyo alimhakikisha kwamba kwa sababu ya hali yake hisia zake zinaeleweka. Kisha ndugu huyo akamkumbusha Andrey kwamba Yesu aliona kuwa ni pendeleo kuteswa kwa ajili ya jina la Yehova. Andrey anasema: “Baada ya hapo nilitulia. Nimeazimia kuendelea kufanya mapenzi ya Baba yetu.”

Tunasali kwamba Andrey na Tatyana wataendelea kutegemea faraja na nguvu zinazotokana na Neno la Mungu na familia yetu ya kiroho. Tunahakikishiwa kwamba “mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli.”—Mhubiri 8:12.