Hamia kwenye habari

Ndugu Artur Lokhvitskiy pamoja na mke wake, Anna

JANUARI 26, 2021
URUSI

Ndugu Artur Lokhvitskiy Anakabili Kifungo cha Miaka Minne Gerezani Baada ya Nyumba Katika Birobidzhan Kufanyiwa Msako

Ndugu Artur Lokhvitskiy Anakabili Kifungo cha Miaka Minne Gerezani Baada ya Nyumba Katika Birobidzhan Kufanyiwa Msako

Hukumu Inatarajiwa

Februari 2, 2021, a Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan iliyo katika Eneo Lililotengewa Wayahudi imepanga kutangaza uamuzi katika kesi inayomhusu Ndugu Artur Lokhvitskiy. Anakabili kifungo cha miaka minne gerezani.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Artur Lokhvitskiy

  • Alizaliwa: 1986 (Belgorodskoye, Eneo Lililotengewa Wayahudi)

  • Maisha Yake: Baba ya Artur alikufa alipokuwa na umri wa miaka saba. Yenye ni fundi wa umeme na mtaalamu wa mbinu za kujilinda na moto. Amepewa tuzo mbalimbali kwa sababu ya bidii yake katika kazi

    Artur alipokuwa mtoto, mama yake alimfundisha kumpenda Yehova. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1998 alipokuwa na umri wa miaka 11. Alifunga ndoa na Anna mwaka wa 2018. Wanapenda kusafiri na kufanya matembezi

Historia ya Kesi

Mei 2018, miezi mitatu baada ya Artur na Anna kufunga ndoa, askari walifanya msako katika nyumba yao. Msako huo ulikuwa sehemu ya kampeni iliyopewa jina la “Siku ya Hukumu,” ambapo maofisa 150 wa usalama walifanya msako katika nyumba 22 za Mashahidi wa Yehova. Nyumba ya Irina, mama ya Artur, ilipekuliwa pia. Julai 31, 2019, maofisa wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) wa Birobidzhan, walifungua kesi ya uhalifu dhidi ya Artur kwa madai ya kwamba alishiriki katika utendaji wenye msimamo mkali. Pia, Anna na Irina walishtakiwa katika kesi nyingine.

Kesi ya uhalifu dhidi ya familia hii inasababisha changamoto kubwa ya kifedha. Wenye mamlaka wamemzuia Artur asitumie pesa katika akaunti yake ya benki. Kwa kuongezea, mwajiri wake amesema kwamba atamfuta kazi.

Uchunguzi unaoendelea wa mashtaka ya uhalifu unavuruga sana ratiba ya kila siku ya familia hiyo. Artur anasema hivi: “Maisha yetu ya kila siku yamebadilika sana. Ni vigumu sana kupanga mambo tutakayofanya katika juma au siku. [Polisi] hutupigia simu muda wowote unaowafaa wao. Hivyo, kila mara tunalazimika kubadili ratiba zetu.”

Artur na Anna wanathamini sana msaada wanaopata kutoka kwa waamini wenzao. Artur anasema hivi: “Ndugu zetu wanatutegemeza sana kihisia na kiroho. . . . Maneno hayatoshi kuonyesha furaha yetu kwa utegemezi huo kutoka kwa watu wa Yehova na pendeleo letu la kutetea jina la Yehova kupitia kesi hii! Ni wazi kabisa kwamba Yehova hawaachi watu wake!”

Familia ya Lokhviskiy imeimarishwa na kuwa jasiri kwa kuendelea na ratiba yao nzuri ya kiroho. Hata hivyo, mambo si rahisi kila mara. Muda mfupi baada ya msako wa “Siku ya Hukumu,” Artur anasema hivi: “Hatukuwa na chakula chochote cha kiroho.” Mwanzoni, Artur alihangaishwa na jambo hilo. Alifikiria sana jinsi watakavyoweza kuendelea na ratiba yao ya kiroho. Lakini alikumbuka kweli hii ya msingi: “[FSB] hawawezi kutuzuia kusali. Mara moja tukaanza kufanya hivyo. Sala ilitusaidia sana.”

Yehova alijibu sala zao mara moja kwa kuwapatia chakula cha kiroho walichohitaji ili kuendelea na ratiba yao ya kiroho. Artur anasema hivi: “Tulijitahidi kufanya ibada ya familia kwa ukawaida, kutayarisha mikutano, na kusoma Biblia tukiwa familia. Jambo hilo lilitusaidia kuwa karibu na pia kuona Mungu akitutegemeza katika maisha yetu na kudumisha mtazamo unaofaa licha ya hali zetu.”

Zaidi ya kusoma na kutafakari Neno la Mungu, walinufaika sana pia kwa kutafakari baraka za wakati ujao. Artur anasema hivi: “Tulianza kutafakari zaidi kuhusu tumaini la wakati ujao, tukiwa katika ulimwengu mpya.” Aliongezea hivi: “Tungependa kushiriki katika kazi ya kuisafisha dunia na ujenzi wakati ujao. Kutafakari mambo hayo hutuimarisha na kutuchochea.”

Kabla ya siku hiyo kufika, Artur na Anna wanatafakari kwa ukawaida andiko la Waebrania 13:6, linalosema hivi: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?” Artur anasema: “Tunakazia fikira ukweli wa kwamba hata tukikosa uhuru wa kukutana pamoja, au hata kuonana sisi wenyewe, hawataweza kamwe kutuzuia kuwa na mambo tunayothamini sana—uhusiano wetu na Yehova, sala, na tumaini letu la wakati ujao.”

a Huenda itabadilika.