Hamia kwenye habari

Ndugu Yegor Baranov na Dada Darya Dulova

SEPTEMBA 8, 2020
URUSI

Ndugu Baranov na Dada Dulova Wenye Umri Mdogo Waonyesha Imani na Ujasiri

Ndugu Baranov na Dada Dulova Wenye Umri Mdogo Waonyesha Imani na Ujasiri

Vijana wawili wapendwa nchini Urusi, Ndugu Yegor Baranov na Dada Darya Dulova, wanaendelea kuonyesha ujasiri licha ya kwamba huenda watahukumiwa kuwa na hatia na kufungwa kwa muda mrefu gerezani. Kwa sasa, Ndugu Baranov, aliye na umri wa miaka 19, yuko mahabusu. Dada Dulova alikuwa na umri wa miaka 18 tu wenye mamlaka walipovamia nyumba yao. Wao ndio wachanga zaidi kati ya ndugu na dada 380 nchini Urusi ambao wameshtakiwa kwa sababu ya imani yao.

Ndugu Baranov amekuwa mahabusu tangu Mei 27, 2020. Dada Dulova anasubiri uamuzi wa mahakama katika kesi mbili za uhalifu. Licha ya hali ngumu wanazokabili, wameazimia kudumisha uaminifu wao kwa Yehova.

Mei 27, maofisa wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) walivamia nyumba ambamo Ndugu Baranov alikuwa akiishi na mama yake. Siku hiyohiyo, Hakimu Aleksey Shatilov aliagiza kwamba ndugu yetu afungwe kwa sababu ya kuwa “mmoja wa viongozi” wa Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo.

Ndugu Baranov anasema kwamba wakati wa uvamizi huo wenye kushtua alitulia baada ya kusali kwa Yehova. Anasema hivi: “Ofisa mmoja aliyekuwa akifanya msako huo alisema nilikuwa nikijiendesha kana kwamba nilikuwa nikiwatarajia.”

Ndugu Baranov anasema yeye hujikumbusha mara nyingi kwamba “ikiwa Yehova aliruhusu hali hii itokee, basi inamaanisha ninaweza kuivumilia.” Anaeleza hivi pia: “Kusali kwa bidii kumwomba Mungu msaada na roho yake takatifu kumenisaidia nisiwe na hofu. Pia, nina uhakika kwa sababu ninajua mimi si mhalifu. Dhamiri yangu ni safi, nami ninateswa kwa sababu ya imani yangu.”

Ndugu Baranov amesema kwamba anajihisi akiwa salama katika mahabusu. Wafungwa wenzake wasio na jeuri wamemtendea kwa heshima na kumwona kama ndugu yao mdogo. Anasema hivi: “Wanajua kwamba sipaswi kuwa hapa.”

Agosti 1, 2018, maofisa walivamia nyumba ambamo Dada Dulova anaishi na mama yake. Dada Dulova anasema kwamba ingawa msako huo na kukamatwa kwake kulimsababishia matatizo ya kihisia, imani yake ni imara. Anasema hivi: “Nimeazimia kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. Nitamtumikia hadi mwisho, hata nini kitokee.”

Kesi ya uhalifu ya Dada Dulova ilianza Septemba 2019 katika Mahakama ya Jiji la Karpinsky katika Eneo la Sverdlovsk. Kesi yake ilipokuwa ikisikilizwa, Dada Dulova alieleza mahakama kwamba ni kawaida kwa watu kuwasimulia wengine mambo yanayowafurahisha. Alisema hivi: “Kwa mfano, ninajua kwamba hivi karibuni Mungu ataigeuza dunia kuwa paradiso, na hivi karibuni tutoa machozi ya shangwe tu. Je, sipaswi kumweleza jirani yangu habari hiyo yenye kufurahisha?”

Licha ya kujitetea kwa njia hiyo inayopatana na akili na kwa ujasiri, Januari 27, 2020 Dada Dulova alihukumiwa kifungo cha nje cha mwaka mmoja. Wakili wake alikata rufaa.

Agosti 6, 2020, Mahakama ya Eneo la Sverdlovsk ilifuta uamuzi wa awali wa kumfunga Dada Dulova. Kesi hiyo ilirudishwa kwenye Mahakama ya Jiji la Karpinsky ili isikilizwe na hakimu mwingine. Tarehe ya kusikilizwa kwa kesi hiyo haijapangwa. Anaposubiri matokeo ya kesi hiyo, yeye, mama yake, na Mashahidi wengine watatu wanakabiliwa na kesi nyingine ya uhalifu.

Ndugu Baranov na Dada Dulova wamejifunza mengi kutokana na majaribu yao.

Dada Dulova anaeleza mambo ambayo yamemsaidia: “Imarisha hali yako ya kiroho kwa kusoma Biblia, kutayarisha mikutano ya kutaniko, na kujifunza nyimbo za Ufalme. Tumia muda mwingi kutafakari maandiko ya Biblia yanayoweza kukusaidia uache kufikiria mahangaiko na wasiwasi unaokabili.”

Ndugu Baranov anasema hivi: “Ili kuvumilia hali hizi, unahitaji kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu. Usipoteze muda. Imarisha urafiki wako na Yehova Mungu sasa hivi.”

Biblia ina mifano mingi ya jinsi Yehova alivyowasaidia vijana waaminifu kuwa imara na jasiri. Tunajua kwamba ataendelea kuwategemeza vijana wetu wapendwa wanaokabili mateso nchini Urusi na katika sehemu nyingine za ulimwengu.​—1 Samweli 1:20; 16:18; 2 Wafalme 5:1-3; Danieli 1:14-17; 3:17-27.