Hamia kwenye habari

Ndugu Dmitriy Vinogradov akiwa na mke wake, Zhanargul, na binti zake, Arina (kushoto) na Olesya (kulia)

MEI 18, 2021
URUSI

Ndugu Dmitriy Vinogradov Anahisi Baraka za Yehova Anapovumilia Mateso

Ndugu Dmitriy Vinogradov Anahisi Baraka za Yehova Anapovumilia Mateso

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yakataa Rufaa

Oktoba 28, 2021, Mahakama ya Eneo la Chelyabinsk ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Vinogradov. Hukumu yake ya awali inaendelea kutumika. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Juni 7, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Tsentralniy iliyoko Chelyabinsk ilimhukumu Ndugu Dmitriy Vinogradov kifungo cha nje cha miaka miwili.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Dmitriy Vinogradov

  • Alizaliwa: 1963 (Chelyabinsk)

  • Maisha Yake: Alilelewa na mama yake baada ya wazazi wake kutalikiana. Kwa kuwa alipenda mchezo wa chess aliamua kuufanya uwe kazi yake maishani na hivyo akawa gwiji. Anawafundisha watu kucheza chess katika shule ya kibinafsi. Alifunga ndoa na Zhanargul katika mwaka wa 1990. Wana watoto wanne, wawili wa mwisho bado wanaishi nyumbani

    Sikuzote alijiuliza kwa nini watu wenye akili huchafua sayari yetu na kuwaumiza wengine. Alipata majibu yenye kuridhisha katika Biblia. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova katika mwaka wa 2014

Historia ya Kesi

Mwishoni mwa mwaka wa 2018, wapelelezi walitumiwa ili kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na Dmitriy. Kufikia Januari 2020, wenye mamlaka walikuwa wamekusanya kiasi cha kutosha cha walichokiita ushahidi ili kufungua kesi ya uhalifu dhidi yake. Miezi miwili baadaye, maofisa waliingia nyumbani kwake na kufanya upekuzi alipokuwa ametoka.

Dmitriy anasumbuliwa na kupanda kwa shinikizo la damu na ana matatizo ya kuona. Anasema hivi: “Hata hivyo, uhusiano wangu na Mungu hautegemei afya yangu ya kimwili. Ninafurahi na kujivunia kwamba ninaweza kutoa ushahidi mahakamani.”

Dmitriy na familia yake wamesitawisha mazoea mazuri ya kusomba Biblia na kutafakari na vilevile kutayarisha, kuhudhuria, na kutoa maelezo kwenye mikutano. Kadiri ambavyo miaka imepita, kufanya hivyo kumesaidia familia yao kumkaribia Yehova na kuwa na uhusiano mzuri kati yao na pia kuwa tayari kuvumilia mateso. Anasema hivi pia: “Sala za akina ndugu na dada ni mojawapo ya mambo muhimu zaidi yanayotusaidia. Yehova husikia sala za watumishi hao waadilifu, na kwa sababu hiyo familia yetu imepata baraka nyingi kutoka kwa Yehova.”

Tunajifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu na dada zetu waaminifu ambao wanavumilia mateso kwa ujasiri na shangwe. Tunawafikiria tunaposoma maneno ya 2 Wathesalonike 1:4: “Tunajivunia ninyi kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu na imani yenu katika mateso yenu yote na taabu mnayopata.”