Hamia kwenye habari

Siku kumi na nne baada ya kuachiliwa huru kutoka gerezani nchini Urusi, Ndugu Konstantin Bazhenov akiwa pamoja na mke wake, Irina, nchini Ukrainia baada ya kuvuka mpaka Mei 19, 2021

MEI 20, 2021
URUSI

Ndugu Konstantin Bazhenov Amewasili Salama Nchini Ukrainia Baada ya Kuhamishwa Kutoka Urusi

Ndugu Konstantin Bazhenov Amewasili Salama Nchini Ukrainia Baada ya Kuhamishwa Kutoka Urusi

Mei 5, 2021, Ndugu Konstantin Bazhenov aliachiliwa kutoka gerezani nchini Urusi. a Baada ya kuzuiliwa kwa muda, alihamishiwa nchini Ukrainia Mei 19, 2021. Mke wake, Irina, alitangulia ili ampokee atakapowasili. Konstantin alihamishwa kwa sababu Urusi ilikataa uraia wake mnamo Mei 2020.

Baada ya kuvuka mpaka na kuingia Ukrainia, Ndugu Konstantin Bazhenov na mke wake, Irina, wakikaribishwa na wenzi wengine waliobeba bango lenye maneno ya Isaya 54:17 kwa sehemu: “Hakuna silaha yoyote itakayotokezwa dhidi yako itakayofanikiwa, . . . asema Yehova.”

Maelezo Mafupi Kumhusu

Konstantin alizaliwa mwaka wa 1975 katika familia isiyo ya kidini magharibi mwa jiji la Veliky Novgorod, nchini Urusi. Alipokuwa mtoto, familia yao ilihamia Ukrainia. Konstantin alicheza sarakasi alipokuwa kijana na alipenda muziki sana. Alihitimu katika shule ya muziki na kuwa kiongozi wa bendi.

Hata kabla ya kuanza kujifunza Biblia, Konstantin aliamini kwamba jeuri na vita yalikuwa mambo mabaya. Hivyo, alipoitwa kutumikia katika jeshi la Ukrainia, alikataa. Alipokuwa chuo, alijiuliza maswali kuhusu maisha na dini. Alichunguza madhehebu kadhaa na mwishowe alipata majibu aliyokuwa akitafuta alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alibatizwa mwaka wa 1996.

Konstantin alifunga ndoa na Irina mwaka wa 2001. Alitegemeza familia yake kwa kufanya kazi ya kujenga majiko ya kuokea na maeneo ya kuwasha kuni za kupasha joto nyumba kwa kutumia matofali ya kuchoma. Walihamia Urusi mwaka wa 2009.

Uvamizi na Kuwekwa Mahabusu

Juni 12, 2018, polisi waliobeba silaha walivamia nyumba saba za Mashahidi wa Yehova jijini Saratov, kutia ndani nyumba ya Konstantin na Irina. Konstantin alikamatwa pamoja na ndugu wengine wawili na kuwekwa mahabusu.

Pindi alipofika tu, Konstantin alijua kwamba alihitaji faraja na utegemezo wa Neno la Mungu, lakini hakuweza kupata Biblia. Anasema hivi: “Mke wangu alinitumia daftari, na kila siku niliandika mistari ya Biblia niliyoweza kukumbuka.” Yehova alinisaidia kukumbuka mistari 500 katika miezi miwili tu! Alipopata Biblia, aliisoma kwa shauku ukurasa mmoja baada ya mwingine kwa miezi minne tu. Maandiko yalimwimarisha sana. Alipata shangwe tele aliposhiriki mambo yanayotia moyo katika barua alizowaandikia rafiki zake na mke wake.

Konstantin alisali mara nyingi na kumwomba Yehova amsaidie kuvumilia wakati huo alipokuwa mahabusu, hasa alipojihisi mpweke na kumkosa mke wake. Anaeleza hivi: “Ningepiga magoti na kulia machozi niliposali kwa Yehova. Niliamua kumwandikia Yehova maombi yangu kwenye karatasi na kutia alama zile alizojibu. Nilikuwa na uhakika zaidi kwamba Yehova alikuwa karibu sana na mimi.” Aliachiliwa huru Mei 20, 2019. Lakini changamoto zake hazikuwa zimeisha.

Hukumu

Konstantin pamoja na ndugu wengine watano katika jiji la Saratov walihukumiwa na kupelekwa gerezani Septemba 19, 2019. Baada ya kushindwa kesi walipokata rufaa, ndugu watano walihamishiwa kwenye gereza lililo Orenburg. Konstantin alipelekwa gereza lililo Dimitrovgrad, iliyo umbali wa kilomita 500 kutoka Saratov, alipotokea na mke wake alipo.

Konstantin akifanya ukumbusho wa mwaka 2020 akiwa gerezani

Kwa kipindi ambacho Irina ametenganishwa na Konstantin, ametiwa moyo kwa kusoma Habari za JW na sehemu za “maisha yake” inayoelezea maisha ya zamani ya ndugu na dada ambao wameonyesha ujasiri na kuvumilia mateso kwa shangwe. Irina alitiwa moyo pia na jinsi Konstantin amesimama imara akiwa na amani ya moyoni. Alipoulizwa wakati Konstantin bado alikuwa gerezani, alisema hivi: “Siku zote ana mtazamo mzuri!” Aliporuhusiwa kumpigia simu Konstantin, waliimba nyimbo pamoja, walisali na kujifunza pamoja. Alisema kwamba mazungumzo yao ya Biblia yaliimarisha imani yake katika Yehova na kulimsaidia kudumisha shangwe yake licha ya hali aliyokuwa akipitia.

Konstantin alikaa mahabusu kwa zaidi ya miezi 14 na zaidi ya mwaka na nusu gerezani kwa sababu ya imani yake. Aliachiliwa huru miezi tisa kabla ya hukumu yake ya miaka mitatu na nusu kutimia. Hili liliwezekana kwa sababu muda aliokaa kizuizini unahesabiwa kama uliopunguza muda aliokaa gerezani kwa kuzidishwa kwa mara moja na nusu. Kwa kuongezea hakulazimika kumalizia miezi miwili inayobaki kwa sababu alipewa msamaha.

Tunashangilia kwamba Konstantin ameachiliwa huru na kuwa na mke wake tena. Ndugu na dada zetu wote wanaovumilia mateso wanaonyesha kwamba wanachukua maneno ya Mfalme Daudi kwa uzito: “Ninakimbilia kivuli cha mabawa yako mpaka matatizo haya yapite.”—Zaburi 57:1.

a Konstantin alipoachiliwa huru, Irina alikuwa pamoja na ndugu na dada wengine 20 hivi wakimsubiri nje ya gereza ili wamsalimie, kabla ya kumpeleka mahabusu atakaposubiri uhamisho wake. Maofisa waliopewa mgawo wa kumsindikiza Konstantin walimruhusu azungumze na mke wake kwa dakika 30 kabla ya kumpeleka mahabusu.