Hamia kwenye habari

Ndugu Konstantin Moiseyenko akiwa pamoja na mke wake, Margarita

JULAI 7, 2021
URUSI

Ndugu Konstantin Moiseyenko Aimarishwa Kupitia Mifano ya Wengine

Ndugu Konstantin Moiseyenko Aimarishwa Kupitia Mifano ya Wengine

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yakataa Ombi la Rufaa

Septemba 9, 2021, Mahakama ya Eneo la Amur ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Moiseyenko. Hukumu yake ya awali inaendelea kutumika. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Julai 14, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Zeyskiy katika Eneo la Amur ilimhukumu Ndugu Konstantin Moiseyenko kifungo cha nje cha miaka sita. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Konstantin Moiseyenko

  • Alizaliwa: 1976 (Abakan, Jamhuri ya Khakassia)

  • Maisha Yake: Ana wadogo zake ambao ni mapacha wa kiume. Alipokuwa kijana alipenda karate. Amefanya kazi ya kudumisha utendaji wa mitambo ya kompyuta na pia uhandisi

    Alifunga ndoa na Margarita, ambaye ni mwana-mitindo mwaka wa 1998. Kwa pamoja walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova mwanzoni mwa mwaka wa 2000. Usahihi wa kihistoria na wa kisayansi wa Biblia ulimchochea Konstantin kujifunza zaidi. Walibatizwa pamoja baadaye mwaka huohuo

    Baba yake alikufa miaka kumi iliyopita. Alimtunza nyanya yake aliyekuwa kipofu kwa miaka sita hadi alipokufa hivi majuzi

Historia ya Kesi

Machi 11, 2019, Idara ya Uchunguzi ya Usalama wa Taifa (FSB) iliyo katika eneo la Amur ilifungua kesi ya uhalifu dhidi ya Ndugu Konstantin Moiseyenko. Kisha maofisa hao walivamia nyumba tano za Mashahidi, kutia ndani nyumba ya Konstantin. Wenye mamlaka walichukua kompyuta, simu zao, na stakabadhi za kibinafsi. Jina la Konstantin limeongezwa kwenye orodha ya watu wenye msimamo mkali ya Shirikisho la Urusi, na hilo linamzuia asiweze kutumia akaunti yake ya benki.

Konstantin anakumbuka jambo aliloona alipohudhuria kusanyiko pamoja na mke wake huko Seoul, Korea Kusini, mwaka wa 2018 lilivyomtia moyo. Wakati wa programu hiyo, msemaji mmoja aliwaomba wahudhuriaji ambao wamewahi kufungwa kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote wasimame. Konstantin anasema: “Karibu ndugu wote waliokuwa uwanjani walisimama, na msemaji akasema: ‘Tazama! Wako hai na ni wenye afya njema!’ Hili lilinisaidia kuona waziwazi kwamba inawezekana kuvumilia chini ya majaribu. Na pia alisoma Zaburi 23:5: “Wewe huniandalia meza mbele ya maadui wangu. Unakiburudisha kichwa changu kwa mafuta, kikombe changu kimejazwa vizuri.” Konstantin anasema kwamba maneno hayo yalimgusa moyo kwelikweli.

Konstantin anathamini msaada wa undugu wa ulimwenguni pote. Anapendezwa kwamba Mashahidi ulimwenguni pote wanataka sana kujua jinsi kesi yake inavyoendelea na wanasali kwa niaba yake. Anasema: “Ninaona kikundi kikubwa cha ndugu na dada wakiwa wamesimama pamoja na kila ndugu na dada anayeteswa katika nchi yetu. Hawa ndugu na dada zetu wanatenda kulingana na maneno ya 1 Yohana 3:16, inayosema hivi kwa sehemu: ‘Tuna wajibu wa kutoa uhai wetu kwa ajili ya ndugu zetu.’”

Tunashangilia tunaposikia kwamba Yehova anaendelea kuwategemeza na kuwatia nguvu ndugu na dada zetu nchini Urusi. Tunazidi kuwa na uhakika kwamba atatupa sisi pia “uwezo na nguvu” tutakapokabili mateso kama hayo.—Zaburi 68:35.