Hamia kwenye habari

Ndugu Nikolay Aliyev na mke wake, Alesya

MACHI 25, 2021
URUSI

Ndugu Nikolay Aliyev Aonyesha Ujasiri Anapovumilia Mateso kwa Sababu ya Imani Yake

Ndugu Nikolay Aliyev Aonyesha Ujasiri Anapovumilia Mateso kwa Sababu ya Imani Yake

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yakataa Ombi la Rufaa

Septemba 2, 2021, Mahakama ya Eneo la Khabarovsk ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Nikolay Aliyev. Hukumu yake itaendelea kutumika. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Ndugu Nikolay Aliyev Amehukumiwa Kifungo cha Nje

Juni 4, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Kati ya Komsomolsk-on-Amur ilimhukumu Ndugu Nikolay Aliyev kifungo cha nje cha miaka minne na nusu.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Nikolay Aliyev

  • Alizaliwa: 1978 (Komsomolsk-on-Amur)

  • Maisha Yake: Alipokuwa mtoto alijiuliza kuhusu kusudi la uhai na ulimwengu. Hilo lilimfanya atafute majibu katika Biblia. Aliacha michezo ya kupigana baada ya kufikiria kwa kina kuhusu mambo ambayo Yesu alifundisha na mfano alioweka wa kufanya amani. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova katika mwaka wa 1993

    Alifunga ndoa na Alesya mnamo 2016. Anafurahia mambo mengi kutia ndani kusafiri, kwenda matembezi, na kuteleza kwenye theluji

Historia ya Kesi

Mapema asubuhi ya Mei 22, 2020, maofisa wa usalama katika jiji la Komsomolsk-on-Amur walivamia nyumba ya Nikolay na Alesya. Maofisa hao walipoingia, walimpiga Nikolay hivi kwamba akaanguka chini nao wakapekua nyumba yao kwa saa tano kabla ya kuwapeleka kizuizini. Wakati wa mahojiano, wenye mamlaka walipendekeza Nikolay abadili dini yake. Pia, walimsihi Alesya aonyeshe ushirikiano ili mume wake “asipatwe na jambo lolote.” Licha ya vitisho vyao, waliachiliwa jioni hiyo na kuruhusiwa kurudi nyumbani.

Nikolay ameimarishwa kwa kufikiria njia nyingi ambazo Yehova amemtegemeza wakati wa kipindi hiki kigumu. Anaeleza hivi: “Unapokabili majaribu, unaelewa kwamba huwezi kuyavumilia kwa nguvu zako mwenyewe. Nilitambua zaidi jinsi Yehova anavyojibu sala na kuandaa mwongozo. Nilisadiki ukweli wa maneno ya Paulo: ‘Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.’”—2 Wakorintho 12:10.

Nikolay na Alesya wanaendelea kutafuta njia za kusitawisha ujasiri na kuwa watulivu. Wamechapisha andiko la Isaya 41:10 na kulibandika kwenye friji yao. Nikolay anasema hivi: “Mambo yanapokuwa magumu sana, mimi husoma andiko hilo, na linanipunguzia mkazo. Maneno hayo hunitia moyo nisiogope. Kinachoniimarisha zaidi ni uhakika wa Yehova kwamba yuko kando yangu, yuko karibu sana hivi kwamba ni kana kwamba mkono wake wa kulia umenikumbatia kama rafiki wa karibu.” Tuna uhakika kwamba sikuzote Yehova atawaimarisha waaminifu wake.