Hamia kwenye habari

JANUARI 19, 2021
URUSI

Ndugu Sergey Britvin na Vadim Levchuk Wanaendelea Kuwa Imara Licha ya Kupoteza Rufaa

Ndugu Sergey Britvin na Vadim Levchuk Wanaendelea Kuwa Imara Licha ya Kupoteza Rufaa

Januari 19, 2021, Mahakama ya Eneo la Kemerovo imekataa ombi la rufaa la Ndugu Sergey Britvin na Ndugu Vadim Levchuk. Hukumu yao ya awali ya miaka minne gerezani sasa itatekelezwa. Kwa sababu ya muda ambao tayari wametumia katika mahabusu na kifungo cha nyumbani, inahesabiwa kwamba wametumikia zaidi ya miaka mitatu ya kifungo chao. Kwa sababu hiyo, wanaweza kuachiliwa huru baada ya mwaka mmoja hivi. Wote wawili wameazimia kuendelea kuwa imara na kukabiliana na hali yao kwa njia inayofaa.

Mwishoni mwa kesi yao ya awali, ndugu hao walizungumza kwa ujasiri kuhusu imani yao katika Yehova na jinsi walivyonufaika kwa kumtumikia.

Sergey aliiambia mahakama hivi: “Mwendesha-mashtaka alitarajia nini kutoka kwangu? Kwamba niikane imani yangu? Imani hiyo katika Yehova ndiyo imenisaidia kuboresha utu wangu na kuwa raia wa Urusi anayeheshimika. Ninamshukuru Mungu kwamba amenisaidia kuiokoa ndoa yangu na kuboresha maisha yangu. Ninamshukuru Yehova kwamba nimepata kusudi halisi maishani na uhakika wa kuwa na wakati ujao mzuri zaidi. Uhusiano wa karibu na Mungu, Yehova, ndilo jambo lenye thamani zaidi maishani mwangu. Ninathamini urafiki wangu pamoja naye, haidhuru ninashtakiwa kwa jambo gani.”

Vadim alisema hivi: “Wakati wa shughuli hii yote, mimi binafsi nimepata utulivu mwingi kwa sababu Yehova yuko upande wangu nami niko upande wa Yehova! Maoni ya Mungu ndiyo muhimu kwangu haidhuru ni uamuzi gani utakaotolewa. Hakuna tofauti kwangu nitakuwa wapi ninapoendelea kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu, kama vile upendo, shangwe, amani, fadhili, upole, na kujizuia.”