Hamia kwenye habari

Sergey Verkhoturov pamoja na mke wake, Viktoriya

FEBRUARI 26, 2021
URUSI

Ndugu Sergey Verkhoturov Anaendelea Kuwa Imara Licha ya Kukabili Miaka Saba Gerezani

Ndugu Sergey Verkhoturov Anaendelea Kuwa Imara Licha ya Kukabili Miaka Saba Gerezani

Hukumu Inatarajiwa

Machi 1, 2021, a Mahakama ya Wilaya ya Priokskiy iliyoko Nizhny Novgorod inaweza kutangaza uamuzi wake katika kesi kumhusu Ndugu Sergey Verkhoturov. Anakabili kifungo cha miaka saba gerezani.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Sergey Verkhoturov

  • Alizaliwa: 1974 (Eneo la Baikalsk, Irkutsk)

  • Maisha Yake: Alikuwa fundi wa vifaa vya umeme kwa miaka kumi. Hivi karibuni amefanya kazi akiwa mshauri wa mambo ya kisheria katika kampuni ya uzalishaji

  • Akiwa na umri mdogo alipendezwa na Biblia. Alipokuwa mtu mzima alivutiwa na mwenendo mzuri wa mfanyakazi mwenzake aliyefundishwa Biblia na Mashahidi wa Yehova. Mwishowe, alikubali funzo la Biblia. Alivutiwa sana na jinsi ambavyo Biblia inapatana na ni rahisi kuielewa. Alibatizwa mwaka wa 1995. Alifunga ndoa na mke wake, Viktoriya mwaka 2001

Historia ya Kesi

Julai 16 na 17, 2019, wenye mamlaka nchini Urusi walifanya msako katika nyumba 35 za Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika Eneo la Nizhny Novgorod, kutia ndani nyumba ya Verkhoturov. Maofisa walipoanza kufanya msako katika nyumba yake, Sergey anasema: “Nilihofu kidogo, lakini nilikuwa mtulivu.” Kisha maofisa hao walimtishia na kusema kwamba watamfunga gerezani Viktoriya ikiwa hatatoa taarifa za siri. Sergey anasema hivi: “Jambo hilo lilikuwa gumu sana kwangu.” Kwa msaada wa Yehova, aliendelea kubaki imara, na Viktoriya b hakufungwa gerezani.

Anasema hivi: “Nimejifunza kutoogopa mambo ambayo hayajatokea kwa sababu mara nyingi mambo huwa tofauti na jinsi unavyotarajia. Unapokuwa chini ya jaribu unagundua kwamba kwa wale wanaokutazama, jaribu hilo ni kubwa sana. Unapopitia majaribu, unajionea na kuhisi jinsi Yehova anavyokutegemeza katika njia ya pekee.”

Ili kudumisha shangwe yake, Sergey anakazia fikira kumtumikia Yehova na kuwasaidia wengine. Anasema hivi: “Nina kusudi moja tu—kwamba Yehova ajitukuze mwenyewe. Nimesali na nitaendelea kusali kuhusu hilo. Ninasali pia kwamba niendelee kuvumilia majaribu katika njia ambayo italiletea sifa jina lake na nitaweza kutoa ushahidi kupitia hilo. Watu nilioshughulika nao wakati wa kesi yangu ama hawajui lolote kumhusu Mungu au wanajua mambo machache kumhusu. Ninamsihi Yehova kwa moyo wangu wote awasaidie wamjue.”

Kadiri ndugu na dada zetu nchi Urusi wanavyoendelea kuteswa, tunakubaliana na maneno ya mtume Paulo aliyesema hivi: “Bwana wa amani na aendelee kuwapa amani kwa kila njia. Bwana awe nanyi nyote.”—2 Wathesalonike 3:16.

a Inaweza kubadilishwa

b Machi 2020, wenye mamlaka walifungua kesi nyingine ya uhalifu dhidi ya Viktoriya