Hamia kwenye habari

Ndugu Vasiliy Reznichenko

MACHI 26, 2021
URUSI

Ndugu Vasiliy Reznichenko Mwenye Umri wa Miaka 78 Ameshtakiwa Kuwa na “Msimamo Mkali” kwa Kumwabudu Mungu kwa Amani

Ndugu Vasiliy Reznichenko Mwenye Umri wa Miaka 78 Ameshtakiwa Kuwa na “Msimamo Mkali” kwa Kumwabudu Mungu kwa Amani

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yamhukumu Ndugu Vasiliy Reznichenko Kuwa na Hatia

Juni  2, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Zeya katika Eneo la Amur ilimhukumu Ndugu Vasiliy Reznichenko kifungo cha nje cha miaka miwili. Hatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Hukumu Inatarajiwa

Mahakama ya Wilaya ya Zeya katika Eneo la Amur itatangaza hivi karibuni uamuzi wake katika kesi kumhusu Ndugu Vasiliy Reznichenko. a Mwendesha-mashtaka bado hajatoa ombi la hukumu anayopendekeza itolewe.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Vasiliy Reznichenko

  • Alizaliwa: 1942 (Murovka, Eneo la Primorye)

  • Maisha Yake: Alizaliwa akiwa wa mwisho katika familia ya watoto watano. Alizoezwa kuendesha tingatinga na baadaye akazoezwa kuwa msaidizi wa nahodha wa meli na pia umekanika. Alitumikia jeshini. Baada ya utumishi wa kijeshi, alifanya kazi akiwa msaidizi wa nahodha wa meli na hatimaye akapandishwa cheo kuwa nahodha. Alipata cheo cha heshima “Mfanyakazi Mstaafu wa Muungano wa Sovieti”

    Alifunga ndoa na Valentina mnamo 1969. Alipata wana watatu. Valentina alimweleza kuhusu kweli za Biblia mnamo 1990. Baada ya kujifunza kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia, alipendezwa sana kujifunza Biblia. Vasiliy alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova katika mwaka wa 1996. Mke wake alikufa katika mwaka wa 2016

Historia ya Kesi

Machi 21, 2019, maofisa katika mji wa Zeya walifanya upekuzi katika nyumba ya Ndugu Vasiliy Reznichenko. Walichukua kompyuta yake, simu, na hati zake. Tangu wakati huo, amewekwa katika orodha ya “watu wenye msimamo mkali” nchini Urusi na amezuiwa kutumia pesa zilizo katika akaunti yake ya benki. Pia hawezi kuondoa katika eneo la kwao.

Vasiliy anaendelea kumtegemea Yehova ili kupata msaada. Anaendelea kuwa mtulivu kwa kudumisha ratiba nzuri ya kiroho, inayotia ndani kusoma Biblia kila siku pamoja na andiko la siku. Pia anathamini upendo kutoka kwa ndugu na dada zake Wakristo.

Anaeleza hivi: “Siku moja baada ya wenye mamlaka kupekua nyumba yangu na kunihoji, ndugu na dada kutoka katika kutaniko langu walinitembelea. Baadhi ya [nyumba zao] zilikuwa pia zimepekuliwa. Siku mbili baadaye, ndugu kadhaa walisafiri kutoka majiji jirani ili kunitembelea. Nilitambua kwamba walihatarisha uhuru wao ili kunitembelea. Nilitiwa moyo sana kwa kuwa walinitembelea. Bado ninatokwa na machozi ninapokumbuka pindi hiyo ambayo walinitembelea.” Anaongezea hivi: “Mambo hayo nilijionea yaliimarisha uhusiano wangu na Yehova. Nimemkaribia zaidi.”

Vasiliy amefarijika na kuimarishwa na maneno yaliyo kwenye Waebrania 13:5. Anaeleza hivi: “Ningependa kuendelea kuwa na uhakika katika ahadi ya Yehova inayosema: ‘Sitakuacha wala kukutupa kamwe.’” Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwategemeza ndugu na dada zetu ambao wanateswa kwa sababu ya imani yao.

a Tarehe ya hukumu haitolewi mapema pindi zote.