Hamia kwenye habari

Kuanzia juu kushoto: Ndugu Yevgeniy Deshko; Ndugu Ruslan Korolyov; Ndugu Viktor Malkov na mke wake, Vera; Ndugu Valeriy Shalev na mke wake, Svetlana. Ndugu Malkov, ambaye alihukumiwa pamoja na ndugu hao wengine alikufa kabla ya kesi yao kwisha

MACHI 24, 2021
URUSI

Ndugu Wanne Huko Smolensk Wavumilia Mateso na Kifungo kwa Sababu ya Imani Yao

Ndugu Wanne Huko Smolensk Wavumilia Mateso na Kifungo kwa Sababu ya Imani Yao

HABARI ZA SASA | Mahakama ya Urusi Imekataa Ombi la Rufaa

Agosti 31, 2021, Mahakama ya Eneo la Smolensk ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Deshko, Ndugu Korolyov, na Ndugu Shalev. Hukumu yao ya awali itaendelea kutumika. Hawatahitaji kwenda gerezani wakati huu.

Mahakama ya Urusi Yawatangaza Ndugu Watatu Kuwa na Hatia ya “Msimamo Mkali”

Aprili 23, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Viwanda huko Smolensk imewahukumu Ndugu Yevgeniy Deshko, Ndugu Ruslan Korolyov, na Ndugu Valeriy Shalev kuwa na hatia. Ndugu Korolyov na Ndugu Shalev wamehukumiwa kifungo cha nje cha miaka sita na nusu. Ndugu Deshko amehukumiwa kifungo cha nje cha miaka sita.

Maelezo Mafupi Kuwahusu

Yevgeniy Deshko

  • Alizaliwa: 1989 (Sochi)

  • Maisha Yake: Amefanya kazi ya kuwakanda watu mwili, udereva, na fundi umeme. Alilelewa na wazazi Mashahidi. Baada ya kuheshimu kile ambacho Biblia inafundisha, aliamua kukataa utumishi wa kijeshi. Alibatizwa mnamo 2012. Kuanzia 2012 hadi 2014, alifanya utumishi wa badala wa kiraia akiwa msaidizi katika hospitali ya kuwatunzia wazee

Ruslan Korolyov

  • Alizaliwa: 1982 (Smolensk)

  • Maisha Yake: Alipokuwa na umri mdogo, alifurahia kujifunza jinsi ya kurekebisha vifaa vya kielektroni. Baadaye akawa mekanika. Alitumikia katika jeshi la Urusi. Alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na akapata faraja kupitia kweli ya Biblia. Alibatizwa mnamo 2004

Viktor Malkov

  • Alizaliwa: 1959 (Smolensk)

  • Maisha Yake: Alifanya kazi akiwa mekanika, seremala, na kuezeka paa. Alifunga ndoa na Vera mnamo 1992. Alipokuwa kijana alipenda kucheza mpira. Alisaidia kumtunza ndugu yake aliye na matatizo ya kuona

    Kwa kuwa alikuwa mwenye jeuri, alifungwa kwa miaka saba. Alikuwa karibu sana kutalikiana na mke wake. Baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alianza kuwa raia mwenye amani, anayefuata haki, na mume mzuri sana. Alibatizwa katika mwaka wa 2008. Alikufa Aprili 26, 2020

Valeriy Shalev

  • Alizaliwa: 1977 (Yartsevo)

  • Maisha Yake: Alijifunza Kiingereza alipokuwa kijana. Alihitimu kutoka kwenye shule ya kijeshi. Alihamia upande wa Mashariki ya Mbali ya Urusi ili akafanye kazi akiwa mhasibu wa jeshi. Baada ya kuondoka jeshini, alifanya kazi akiwa mshauri wa kifedha. Mwaka wa 1999, alifunga ndoa na Svetlana ambaye walikutana wakiwa chuo na akawa baba-mlezi wa mwana wa Svetlana aliyekuwa na umri wa miaka minne. Anafanya mazoezi kwa kucheza mpira na kukimbia

    Mama yake alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na akamweleza mambo aliyokuwa akijifunza. Valeriy alijaribu kukosoa mambo ambayo mama yake alikuwa akijifunza lakini hatimaye aligundua ni ya kweli. Alibatizwa mnamo 2002

Historia ya Kesi

Mateso katika eneo la Smolensk yalianza kabla ya uamuzi wa 2017 wa Mahakama Kuu ambao ulipiga marufuku utendaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Urusi. Desemba 18, 2016, maofisa 15 wa polisi waliokuwa na silaha walikatiza mkutano wa kutaniko kwenye Jumba la Ufalme huko Smolensk. Ndugu na dada 60 walikuwa wamehudhuria mkutano huo. Wakati wa uvamizi huo, maofisa walipandikiza machapisho ambayo serikali ya Urusi ilikuwa imesema ni yenye “msimamo mkali” kisha wakajifanya kwamba “wameyagundua.”

Kati ya mwaka wa 2018 na 2019, maofisa hao waliendelea kufanya upekuzi wa baadhi ya nyumba za ndugu na dada, wakawakamata baadhi yao, na kuwafunga baadhi yao. Aprili 25, 2019, maofisa walivamia baadhi ya nyumba na kuwakamata Ndugu Ruslan Korolyov, Ndugu Valeriy Shalev, na Ndugu Viktor Malkov. Viktor aliwauliza maofisa hao hivi: “Nilifungwa kwa miaka saba kwa sababu nilikuwa mwenye jeuri, kisha nikawa Shahidi wa Yehova. Sasa mnataka kunifunga kwa sababu ya . . . kuhubiri habari njema?”

Ndugu Yevgeniy Deshko alikamatwa na kuwekwa mahabusu kwa siku kadhaa baada ya wale ndugu wengine. Yevgeniy anasema hivi: “Nilijua kwamba ninaweza kukamatwa pia, kwa hiyo nilijitayarisha.” Anasema kwamba maneno ambayo Yehova alimwambia Yoshua yanamtia moyo sana: “Uwe jasiri na imara. Usitetemeke wala kuogopa, kwa maana mimi Yehova Mungu wako nipo pamoja nawe mahali popote utakapoenda.” (Yoshua 1:9) Yevgeniy anaeleza hivi: “Katika andiko hilo Yehova anatutia moyo tuwe jasiri, na pia anatuahidi kwamba atatusaidia.”

Ruslan anasema kwamba alipokuwa mahabusu, alitafakari maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:34. Badala ya kuogopa mambo ambayo yangempata, Ruslan anasema hivi: “Nilitumia muda wangu kuandika barua, kusoma Biblia, na kuzungumza na wafungwa wenzangu kuhusu kweli. Sikuwa na wakati wa kulemewa na mahangaiko.”

Machi 2020, mpelelezi wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) G. P. Bezrukov, alipunguza vizuizi vya akina ndugu hao na kuondoa kifungo chao cha nyumbani. Walikuwa wamefungwa kwa karibu mwaka mmoja gerezani na katika nyumba zao. Walipewa uhuru huo kwa sababu ya kutii wenye mamlaka na kushirikiana nao walipokuwa gerezani. Mpelelezi huyo alikuwa na uhakika kwamba akiwaachilia hawataathiri uchunguzi au kuwa wenye jeuri ikiwa wangehitaji kuhojiwa tena.

Kwa kusikitisha, Viktor alikufa muda mfupi baada ya hapo. Inasemekana kwamba afya yake iliathiriwa vibaya sana na hali mbaya iliyokuwepo alipokuwa mahabusu na mkazo aliopata kutokana na kesi hiyo ya uhalifu.

Ruslan, Valeriy, na Yevgeniy wameazimia kufuata mfano wa Viktor na wengine wengi ambao wamedumisha uaminifu wao mpaka mwisho. Kwa kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, si eti tu watavumilia mateso bali pia watakuwa na shangwe licha ya mateso hayo.

Valeriy anasema hivi: “Kwa sababu ya kufungwa, nilikuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova. Hapo awali uhusiano huo haukuwa wa karibu sana. Ninasoma Biblia kila wakati. Gerezani si mahali pazuri pa kuishi, lakini watu wanafaulu kuishi hata bila msaada wa Yehova. Kwa hiyo, ikiwa Yehova anatutegemeza bila shaka tutavumilia.”

Yevgeniy anasema kwamba sasa amesadikishwa zaidi kwamba Yehova hutusaidia. Anasema hivi: “Ninasadiki kwamba Baba yetu hutusaidia, hasa katika hali ambazo tunahitaji kuvumilia majaribu makali. Kwa hiyo, sasa sina hofu sana ni majaribu gani ambayo huenda nitakabili wakati ujao.”

Hata mahakama ifikie uamuzi gani katika kesi yao, Yevgeniy anasema hivi: “Nimeazimia kuendelea kufanya yote niwezayo ili kuvumilia hali zote ngumu na kuendelea kuwa mwaminifu.”

Kwa msaada wa Yehova, tunajua kwamba ndugu hawa na familia zao wataendelea kuvumilia kwa shangwe licha ya kipindi hiki kigumu.—2 Wathesalonike 3:5.