Hamia kwenye habari

Ndugu Yevgeniy Golik akiwa nje ya mahakama Desemba 2020

JANUARI 21, 2021
URUSI

Ndugu Yevgeniy Golik Ahukumiwa Kifungo cha Nje

Ndugu Yevgeniy Golik Ahukumiwa Kifungo cha Nje

Hukumu

Januari 20, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Birobidzhan ya Eneo Lililotengewa Wayahudi ilimhukumu Ndugu Yevgeniy Golik. Alihukumiwa miaka miwili na nusu ya kifungo cha nje. Hatahitaji kwenda gerezani kwa sasa. Atakata rufaa hukumu hiyo.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Yevgeniy Golik

  • Alizaliwa: 1975 (Birobidzhan, Eneo Lililotengewa Wayahudi)

  • Maisha Yake: Alijifunza kazi ya kuchomelea vyuma. Anafanya kazi ya kusimamia mitambo ya kuchemsha maji. Alitumikia katika jeshi la Urusi kabla ya kuwa Shahidi wa Yehova

    Alijifunza kweli kutoka kwa mama yake. Alipata majibu ya maswali yake kuhusu kusudi la uhai. Pia, mafundisho ya Biblia yalimsaidia kuwajali watu wengine zaidi

Historia ya Kesi

Mapema asubuhi ya Mei 17, 2018, maofisa 150 wa Usalama wa Taifa (FSB) walivamia nyumba 22 za Mashahidi katika jiji la Birobidzhan, lililoko mbali upande wa Mashariki mwa Urusi. Uvamizi huo wa FSB ulipewa jina la siri “Siku ya Hukumu.” Wenye mamlaka katika jiji hilo walifungua kesi dhidi ya Ndugu Yevgeniy Golik na ndugu na dada wengine 21 wanaoishi katika Eneo Lililotengewa Wayahudi. Kesi yake ya uhalifu ilianza Januari 29, 2020.

Mwendesha-mashtaka aliwasilisha ushahidi uliotia ndani video zilizomwonyesha Yevgeniy akijifunza Biblia na baadhi ya machapisho yetu yanayotegemea Biblia.

Si rahisi kuvumilia ukosefu mbaya wa haki. Hata hivyo, Yevgeniy anasema hivi: “ Kuwa na ratiba ya kiroho kunanisaidia nimkazie fikira Yehova na nisijikazie fikira. Mawazo yanayofaa kuhusu Neno la Mungu hunipa shangwe, ambayo hunichochea kuwaeleza wengine mambo hayo.”

Yevgeniy amenufaika kwa kutafakari Zaburi 23:4. Anasema hivi: “[Andiko hilo] limenisaidia niwe jasiri na nivumilie kwa shangwe. Hata ikiwa uhai wetu uko hatarini, ninajua sikuzote Yehova atakuwa hapohapo pamoja nasi.”

Waabudu wengine wa Yehova wamemuunga mkono Yevgeniy. Anasema hivi: “Ndugu na dada walikuja mahakamani kesi hiyo ya uhalifu ilipoanza na hilo lilinitia moyo sana. Pia, mke wangu ambaye Yehova alinipa, amekuwa msaidizi anayefaa kabisa kwa ajili ya wakati huu mgumu. Nina shangwe ambayo haiishi. Nina chakula cha kiroho na cha kimwili na ninapata msaada mwingi sana.”

Yevgeniy ameazimia kudumisha uhusiano wake na Yehova ukiwa imara. Ili kuwasaidia wengine ambao hawajakabili mateso ya moja kwa moja, anasihi hivi: “Jifunze nyimbo [za Ufalme], zoeza moyo wako kuwapenda adui zako, na ujizoeze kuwa mtumishi mwenye shangwe wa Mungu chini ya hali yoyote ile.”

Sote na tuendelee kujifunza masomo muhimu kutoka kwa ndugu na dada zetu nchini Urusi. Na kama tu Yehova anavyowategemeza wanapokabili majaribu, ndivyo atakavyotutegemeza pia.—Zaburi 29:11.