Hamia kwenye habari

Ndugu Yevgeniy Yakku na mke wake, Irina

MEI 17, 2021
URUSI

Ndugu Yevgeniy Yakku Anategemea Hekima ya Yehova Wakati wa Kesi Yake

Ndugu Yevgeniy Yakku Anategemea Hekima ya Yehova Wakati wa Kesi Yake

HABARI ZA KARIBUNI | Mahakama ya Urusi Yakataa Ombi la Rufaa

Oktoba 1, 2021, Mahakama ya Eneo la Arkhangelsk ilikataa ombi la rufaa la Ndugu Yakku. Uamuzi wa mahakama ya chini haujabadilishwa.

Julai 19, 2021, Mahakama ya Wilaya ya Solombalskiy iliyoko Arkhangelsk ilimhukumu Ndugu Yevgeniy Yakku na kumtoza faini ya rubo 880,000 (dola 12,082 za Marekani). Hatahitaji kwenda gerezani.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Yevgeniy Yakku

  • Alizaliwa: 1980 (Kijiji cha Sosnovets, Jamhuri ya Karelia)

  • Maisha Yake: Alipokuwa kijana, alipendezwa sana na utimizo wa unabii wa Biblia. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova katika mwaka wa 2006. Alihamia ili kusomea katika shule ya biashara. Alifunga ndoa na Irina mwaka wa 2007. Wanapenda kusafiri na kwenda matembezi

Historia ya Kesi

Asubuhi ya Februari 18, 2019, maofisa wa Urusi walivamia nyumba ya Ndugu Yevgeniy Yakku na kumkamata wakidai alijihusisha katika utendaji wenye “msimamo mkali.” Maofisa wa polisi wa eneo hilo walimpeleka kizuizini. Alizuiliwa kwa siku mbili. Rafiki zake na watu wa familia hawakujulishwa alipokuwa.

Baada ya kuachiliwa, Yevgeniy alikatazwa asitoke nyumbani kwake usiku, wala asiwe na kikusanyiko cha aina yoyote nyumbani mwake, na pia asiwasiliane na wengine waliohusika katika kesi hiyo, iwe kupitia simu, barua-pepe, au Intaneti. Baada ya miezi saba hivi, mahakama iliondoa baadhi ya vizuizi hivyo na kumruhusu atoke nyumbani jioni.

Novemba 25, 2019, Yevgeniy alihukumiwa kwa dai la kupanga utendaji wenye “msimamo mkali.” Baadaye, mashtaka zaidi yalifunguliwa dhidi yake. Akipatikana kuwa na hatia anaweza kufungwa hata kwa miaka 15 gerezani. Yevgeniy alipoteza kazi, akaunti zake za benki zikazuiliwa, na magari yake mawili yakachukuliwa kwa sababu ya kesi hiyo.

Yevgeniy na Irina wamemtegemea Yehova hata zaidi wakati wa kipindi hiki. Irina anasema hivi: “Siwezi kueleza jinsi ninavyoshukuru ninapoona jinsi Yehova anavyojibu sala kwa njia hususa na kunitunza mimi na Zhenya [Yevgeniy].”

Kwa mfano, Irina alisali kihususa kwamba Yehova ampe yeye na mume wake mioyo mitulivu na uwezo wa kueleza imani yake kwa njia nzuri wakati wa kesi. Yevgeniy alisali kuhusu jambo hilohilo. Alisema hivi: “Kila mara nilipohitaji kwenda mbele ya halmashauri ya uchunguzi au mahakamani, nilimwomba Yehova anipe hekima.” Anahisi kwamba Yehova alijibu sala zake. “Nilisema mambo niliyohitaji kusema lakini sikusema kupita kiasi.” Anaongezea hivi: “Yehova ananionyesha kwamba hajaniacha na anajibu sala zangu kwa njia ninazoweza kutambua. Sasa, ninajionea mkono wake maishani mwangu kwa njia ya wazi zaidi.”

Tunaposubiri uamuzi wa kesi yake, tunajua kwamba Yehova ataendelea kumpa Yevgeniy ujasiri wa kujitetea “kwa upole na heshima kubwa.”—1 Petro 3:15.