Hamia kwenye habari

APRILI 19, 2017
URUSI

Siku ya Tano: Mahakama Kuu Yachunguza Ushahidi Katika Kesi ya Kuwapiga Marufuku Mashahidi wa Yehova

Siku ya Tano: Mahakama Kuu Yachunguza Ushahidi Katika Kesi ya Kuwapiga Marufuku Mashahidi wa Yehova

Leo, Mahakama Kuu ya Shirikisho la Urusi ilianza kupitia faili kubwa za kesi hii—mabuku 43 yaliyojaa hati. Pia, iliwaruhusu mawakili wa Kituo cha Usimamizi kuwasilisha ushahidi mpya kuhusu mashambulizi yaliyofanywa wakati wa huduma za kidini za Mashahidi wa Yehova. Katika miezi ya Machi na Aprili 2017, maofisa wa usalama walikatiza mikutano ya kidini na kuwatisha wahudhuriaji kwamba watashtakiwa kama wahalifu.

Katika uchunguzi wake wa ombi la Wizara ya Haki (Wizara) la kufunga mashirika ya 395 ya kidini yaliyopo (Local Religious Organizations au LRO), Mahakama ilisikiliza maelezo kuhusu muundo wa kisheria na wa kidini wa Mashahidi wa Yehova. Mahakama ilipokagua maamuzi ya mapema ya kupiga marufuku mashirika manane ya kidini (LRO), mawakili wa Mashahidi walionyesha kwamba maamuzi hayo yalitegemea ushahidi uliopandikizwa na kulikuwa na makosa mengi katika uendeshaji wa uchunguzi.

Isitoshe, mawakili wa Kituo cha Usimamizi walikazia kwamba Wizara haina msimamo. Wakati wa kesi za kufunga LRO hizo, Wizara ilishikilia msimamo kwamba Kituo cha Usimamizi hakina uhusiano wowote na utendaji wa LRO hizo. Pia, Kituo cha Usimamizi kilipotaka kuhusika katika kesi hizo mahakamani, Wizara ilizuia jitihada zote hizo. Hata hivyo, katika kesi hii, Wizara inadai kwamba Kituo cha Usimamizi kinalaumika katika makosa yote yanayodaiwa kuwa yalifanywa na LRO na kwa mawazo yenye “msimamo mkali” yanayopatikana katika machapisho ya Mashahidi.

Wizara imefanya uchunguzi mwingi katika mashirika ya kidini ya Mashahidi na kuwasilisha Mahakamani mabuku mengi yenye ripoti za uchunguzi wao. Hata hivyo, Wizara ilipohojiwa, ilishindwa kutambulisha hata tukio moja ambalo Mashahidi walihusika katika utendaji wenye msimamo mkali.

Mahakama itaendelea kusikiliza kesi hiyo Aprili 20, 2017, saa 8:00 alasiri.