Hamia kwenye habari

Ndugu Rinat Kiramov akiwa mahakamani Aprili 2023

JUNI 20, 2024
URUSI

Rinat Kiramov Ateswa kwa Siku Nne Akiwa Gerezani Nchini Urusi

Rinat Kiramov Ateswa kwa Siku Nne Akiwa Gerezani Nchini Urusi

Aprili 2023, Ndugu Rinat Kiramov alihukumiwa kifungo cha miaka saba gerezani na hivi sasa anaendelea kutumikia kifungo hicho. Aprili 2024, mwaka mmoja baada ya hukumu hiyo, Rinat alihamishwa bila sababu ya msingi na kupelekwa kwenye gereza lililo na huduma za kitiba. Wenye mamlaka walidai kwamba eti “wanahisi” Rinat ana kifua kikuu. Siku mbili baada ya kuhamishiwa huko, kikundi cha wafungwa kilianza kumhoji. Wafungwa hao walijaribu kumlazimisha awape habari kuwahusu Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika jiji alilotoka la Akhtubinsk. Rinat alipokataa wakaanza kumtesa. Walimtesa kwa siku nne mfululizo, wakitumia njia mbalimbali za kumuumiza kimwili na hata walimpiga kwa umeme. Mbali na hilo, hawakumruhusu Rinat apate usingizi, aketi chini, au hata kuoga. Walihakikisha yuko macho mchana na usiku akiwa amesimama. Rinat aliruhusiwa kula mlo mmoja tu kwa siku.

Galina, mke wa Rinat alimtembelea mume wake gerezani siku chache baada ya hilo kutokea. Naye alishtuka alipomwona kwa sababu uso wake ulikuwa na majeraha, hakuweza kutembea vizuri, na mikono yake ilikuwa ikitetemeka. Rinat alimsimulia mke wake kilichotokea. Mara moja, Galina alimjulisha wakili wa Rinat. Na bila kukawia, wakili huyo alitoa ombi kwamba Rinat apimwe na daktari ili kuchunguza chanzo cha majeraha yake.

Hilo lilipowasilishwa kwenye ofisi ya mwendesha-mashtaka, Rinat akafanyiwa uchunguzi wa kiafya. Walipata ushahidi wa kutosha kuonyesha kwamba aliteswa na kupigwa vibaya, hivyo, kesi yake imepelekwa kwenye Wizara ya Mambo ya Ndani. Kwa kuongezea, uchunguzi huo ulithibitisha kwamba Rinat hakuwa na kifua kikuu, hivyo Mei 17, 2024, alirudishwa gereza alilokuwa awali.

Rinat na Galina kabla ya kwenda gerezani

Rinat alimwambia Galina jambo lililomsaidia kuvumilia: “Sikuweza kujikinga lakini niliweza kusali na pia nilijaribu kukumbuka mistari mbalimbali ya Biblia. Hayo ni mambo ambayo hakuna mtu anayeweza kuninyang’anya. Angalau zoea nililokuwa nalo awali la kusoma Biblia limetokeza matunda mazuri hivi kwamba niliweza kukumbuka maandiko mengi sana.” Rinat aliongezea hivi: “Kuna watu ambao wamevumilia mateso makali wakiwa wanaharakati wa jambo fulani bila msaada wa roho takatifu ya Yehova. Lakini kwa upande wangu, mimi nilikuwa na nguvu za Yehova zisizo na mipaka ambazo ziliniimarisha. Kwa hiyo nilijiambia: ‘Sasa, kuliko wakati mwingine wowote maishani mwangu, ninaweza kumthibitishia Yehova kwamba nimejitoa kwake. Sitakata tamaa.’”

Ingawa tunahuzunika sana kusikia jinsi Rinat alivyoteswa kinyama, tunafarijika kukumbuka kwamba sikuzote Yehova atatupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili kuvumilia.​—2 Wakorintho 4:7.