Hamia kwenye habari

Kuanzia kushoto kwenda kulia: Wataalamu wa haki za kibinadamu—Valeriy Borshchev, Aleksandr Guryanov, na Sergey Davidis—wakati wa kongamano lililofanywa kwenye Taasisi ya Maadhimisho ya Kimataifa iliyoko Moscow. Kongamano hilo la Aprili 6, 2021 liliadhimisha miaka 70 ya uhamisho wa Mashahidi wa Yehova kupelekwa Siberia

APRILI 12, 2021
URUSI

Taasisi ya Maadhimisho ya Kimataifa Yafanya Kongamano Kukumbuka Miaka 70 ya Mashahidi wa Yehova Kuhamishiwa Siberia na Wasovieti

Taasisi ya Maadhimisho ya Kimataifa Yafanya Kongamano Kukumbuka Miaka 70 ya Mashahidi wa Yehova Kuhamishiwa Siberia na Wasovieti

Siku chache tu baada ya mkutano wa waandishi wa habari uliofanywa Moscow Aprili 1, 2021, ili kuadhimisha miaka 70 ya kuwahamisha Mashahidi wa Yehova kuwapeleka Siberia, Taasisi ya Maadhimisho ya Kimataifa iliwaalika wasomi kadhaa wa Urusi na watetezi wa haki za kibinadamu kwenye kongamano lililofanywa Aprili 6. Mbali na kuzungumzia uhamisho huo uliofanywa mwaka wa 1951—ulioitwa na Wasovieti Oparesheni Kaskazini—wasemaji walizungumzia pia kuhusu historia ndefu ya mateso ambayo Mashahidi wa Yehova wamevumilia nchini Urusi.

Oparesheni Kaskazini ilipangwa na Wizara ya Usalama wa Ndani ya Sovieti (MGB). Mapema katika mwaka wa 1951, MGB ilimtumia ripoti Joseph Stalin, aliyekuwa kiongozi wa Muungano wa Sovieti, iliyosema hivi: “Ili kukomesha utendaji wa Mashahidi wanaofanya mambo yao kichinichini ya kupinga Usovieti, MGB ya USSR imeona ni lazima, kuwakamata viongozi wa dhehebu la Wayehova na kuwahamisha wote wanaotambulishwa kuwa Wayehova kutoka kwenye mipaka ya Ukrainia, Belarus, Moldova, Latvia, Lithuania, na Estonia—pamoja na familia zao—na kuwapeleka kwenye maeneo ya Irkutsk na Tomsk.” Jumla ya watu 10,000 hivi walihamishwa, zaidi ya familia 3,000. Huo ndio ulikuwa uhamisho mkubwa zaidi wa kidini katika historia ya Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti (USSR).

Aleksandr Guryanov, mwenyekiti wa kongamano hilo, alisema hivi katika maelezo yake ya ufunguzi: “Mateso ya kikundi hiki cha kidini . . . bado yanaendelea leo, jambo linalokazia umuhimu wa uchunguzi wa historia ya Oparesheni Kaskazini tunaofanya leo.”

Pavel Polyan, ambaye ni mwanahistoria, mwanajiografia, na mtaalamu katika somo la uhamisho wa lazima uliofanywa na USSR, alizungumza kuhusu historia ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti na kueleza mojawapo ya sababu zilizowafanya Mashahidi wapelekwe uhamishoni. Katika miaka ya mwishoni ya 1940 na ya mwanzoni mwa 1950, MGB ilianza kutambua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na utaratibu sana. Isitoshe, Bw. Polyan alisema hivi: “[Mashahidi wa Yehova] ni wamishonari bora, jambo ambalo halikuifurahisha serikali hiyo ambayo iliamini hakuna Mungu.”

Valeriy Borshchev, mtetezi wa haki za kibinadamu na mwenyekiti msaidizi wa Kikundi cha Moscow Helsinki, alizungumzia jinsi Wasovieti walivyojaribu “kuwaelimisha upya” Mashahidi wa Yehova kwa kutumia propaganda na njia nyingine. Bw. Borshchev anasema kwamba baada ya muda, “kamishna [wa mambo ya kidini] alitambua ni kupoteza wakati kwa sababu mbinu hiyo haingefanya kazi. Lazima tuwapongeze Mashahidi wa Yehova. Waliazimia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu wao.”

Sergey Davidis, mshiriki wa Baraza la Makumbusho ya Haki za Kibinadamu na msimamizi wa programu ya Kutoa Msaada kwa Wafungwa wa Kisiasa, alizungumzia mateso yanayozidi kuongezeka dhidi ya Mashahidi wa Yehova nchini Urusi kuanzia 1998. Alisema kwamba uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu Aprili 2017 wa kufunga mashirika ya kisheria yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ulitokana hasa na sababu ya kwamba Mashahidi wa Yehova wanadai kuwa ndio dini pekee ya kweli. Bw.  Davidis alikazia hivi: “Shtaka linalotolewa dhidi yao halipatani na akili hata kidogo. Kila mtu wa dini huamini kwamba dini yake ndiyo ya kweli inapolinganishwa na dini nyingine yoyote.”

Ndugu Yaroslav Sivulskiy, mwakilishi wa European Association of Jehovah’s Witnesses, alisimulia mambo ambayo wazazi wake waliopelekwa uhamishoni Siberia walimweleza, kuhusu changamoto nyingi ambazo Mashahidi walikabili huko. Familia fulani ziliachwa katika misitu yenye baridi kali ya Siberia bila kuwa na mahali pa kuishi. Akina ndugu walichimba mashimo chini ya ardhi ili waishi humo. Familia zao zililazimika kuishi humo kwa miezi kadhaa kabla ya kujenga makao ya kudumu. Walipokuwa huko msituni, mara nyingi Mashahidi walikula upupu na magome ya miti. Wengi walikufa kutokana na njaa au magonjwa.

Ndugu mmoja na dada saba wakijitayarisha kujenga eneo la kuishi katika msitu wa Siberia

Ndugu Sivulskiy alisema kwamba Mashahidi walihamishwa katika mwaka wa 1951 kwa sababu ileile inayowafanya wateswe na serikali ya Urusi leo. Wenye mamlaka wanafikiri kimakosa kwamba kwa kuwa Mashahidi hawaungi mkono upande wowote basi hawatambui mamlaka ya serikali. Wenye mamlaka wanasahau kwamba Mashahidi wanajulikana kwa kuheshimu mamlaka, kutii sheria, na kufanya kazi kwa bidii.

Aleksandr Guryanov, mwenyekiti wa kongamano hilo, alitoa maelezo machache ya kumalizia kuhusu hali ya sasa nchini Urusi. Alisema hivi: “Serikali inawachukia hasa Mashahidi wa Yehova.” Wote waliokuwepo walikumbushwa kwamba miaka 70 baada ya uhamisho, kwa mara nyingine serikali ya Urusi ilikuwa ikirudia mateso yaleyale dhidi ya Mashahidi. Raia wanaofuata sheria wa nchi hiyo wanatangazwa tena kuwa wahalifu kwa kufuata imani yao ya kidini, jambo linalolindwa na katiba ya nchi hiyo.

Video ya kongamano hilo inapatikana mtandaoni katika Kirusi tu.