Hamia kwenye habari

JULAI 27, 2017
URUSI

Urusi Inataka Kuitangaza Biblia kuwa na “Msimamo Mkali”

Urusi Inataka Kuitangaza Biblia kuwa na “Msimamo Mkali”

TAARIFA: Mahakama ya Jiji la Vyborg imeahirisha kesi hadi Agosti 9, 2017.

Julai 28, 2017, Mahakama ya Jiji la Vyborg itaendelea kusikiliza kesi kuhusu kutangazwa kwa Biblia Takatifu Tafsiri ya Ulimwengu mpya iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova katika Kirusi kuwa na “msimamo mkali.” Kesi hiyo ilikuwa imeahirishwa tangu Aprili 2016 baada ya hakimu kutoa hukumu iliyounga mkono madai ya Mwendesha Mashtaka wa Usafirishaji wa Leningrad-Finlyandskiy ya kuagiza ufanyike “uchunguzi wa kitaalamu” ili kutangaza Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kuwa na “msimamo mkali.”

Baada ya kucheleweshwa, hatimaye uchunguzi ulikamilika na ukawasilishwa mahakamani Juni 22, 2017. Kama Mashahidi walivyotarajia, uchunguzi huo uliunga mkono madai ya kutangazwa Biblia hiyo kuwa ni chapisho lenye “msimamo mkali.” Uchunguzi huo ulidai kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya “si Biblia.” Walitangaza kwamba hiyo si Biblia ili kuepuka kwa ujanja kubanwa na Sheria ya Kupambana na Utendaji Wenye Msimamo Mkali ambayo inazuia kutangaza maandishi matakatifu kama vile Biblia, kuwa na msimamo mkali. Isitoshe, matokeo ya “uchunguzi wa kitaalamu” yalitegemea masuala ya kidini. Jambo kuu walilopinga ni kurejelewa kwa Tetragramatoni a kuwa “Yehova” na wakadai kwa uwongo kwamba maandishi yalibadilishwa ili yafaane na mafundisho ya Mashahidi.

a Tetragramatoni ni herufi nne za jina la Mungu katika Kiebrania (יהוה), zinazotafsiriwa YHWH na zinapatikana katika Maandiko ya Kiebrania karibu mara 7,000 hivi.