Hamia kwenye habari

DESEMBA 11, 2017
URUSI

Mahakama ya Urusi Yasikiliza Rufaa ya Kupinga Kutangazwa kwa Biblia Kuwa na “Msimamo Mkali”

Mahakama ya Urusi Yasikiliza Rufaa ya Kupinga Kutangazwa kwa Biblia Kuwa na “Msimamo Mkali”

Desemba 6, 2017, Mahakama ya Mkoa ya Leningrad ilisikiliza kesi ya rufaa ya Mashahidi dhidi ya uamuzi wa mahakama ya chini ambao ulipiga marufuku Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Kirusi.

Kesi ilianza kwa mawakili wa Mashahidi kupinga uamuzi wa Mahakama ya Jiji la Vyborg, ambao ulikuwa ukitegemea tu uchunguzi wa “wataalamu” kama msingi wa madai yao. Mahakama hiyo ya jiji haikuwa hata na rejeo moja katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ambalo wataalamu wanasema lina “msimamo mkali.” Hata hivyo, mahakama ilikazia uangalifu mkataa uliotolewa katika uchunguzi wa wataalamu kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inachochea “msimamo mkali” kwa sababu inatumia jina takatifu la Mungu, yaani, Yehova. Mawakili waliikumbusha mahakama kwamba jina hilo takatifu la Mungu limekuwepo katika historia ya utamaduni wa Urusi unaoheshimiwa na linapatikana katika tafsiri nyingi za Biblia. Pia, walizungumzia maelezo yasiyo sahihi ya uchunguzi kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya si Biblia kwa sababu haijielezi waziwazi kuwa ni Biblia. Ili kukanusha madai hayo, walinukuu utangulizi wa toleo la mwaka 2007 ambao unasema hivi: “Hii ni tafsiri mpya ya Biblia ya Kirusi.”

Mahakama ya Mkoa wa Leningrad imeamua kuita jopo la wataalamu kwa ajili ya uchunguzi na ikaahirisha kesi hadi Desemba 20, 2017, saa 8:30 mchana kulingana na saa za Urusi.