Hamia kwenye habari

Jengo la Mahakama ya Mkoa ya Leningrad, ambapo rufaa ilisikilizwa

DESEMBA 27, 2017
URUSI

Rufaa Yakataliwa​—Mahakama ya Urusi Yaunga Mkono Uamuzi wa Kuitangaza Biblia Kuwa na “Msimamo Mkali”

Rufaa Yakataliwa​—Mahakama ya Urusi Yaunga Mkono Uamuzi wa Kuitangaza Biblia Kuwa na “Msimamo Mkali”

Mahakama ya rufaa iliunga mkono uamuzi wa awali wa mahakama ambao uliitangaza Biblia TakatifuTafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kirusi kuwa chapisho “lenye msimamo mkali.” Uamuzi huo unatekelezwa sasa, ukithibitisha kwamba Biblia hii imepigwa marufuku na karibuni itawekwa kwenye Orodha ya Serikali ya Vitabu na Habari Zinazowachochea Watu Kuwa na Msimamo Mkali. Na sasa ni kosa la jinai kwa mtu yoyote kuwasambazia wengine Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata tu kumiliki nakala ya Biblia hiyo kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi kunaweza kumweka mtu kwenye hatari ya kutozwa faini kubwa au jambo lingine baya zaidi.

Mahakama Yapuuza Ukosefu wa Uthibitisho Kutoka kwa “Wataalamu”

Desemba 20, 2017, Mahakama ya Mkoa ya Leningrad iliunga mkono uamuzi wa Mahakama ya Jiji ya Vyborg wa kuitangaza Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kuwa na “msimamo mkali” licha ya kutokuwa na uthibitisho wa kutosha kutoka kwa mwendesha-mashtaka au “wataalamu” waliochaguliwa na mahakama kwa ajili ya kufanya uchunguzi. Uamuzi wa mahakama ulitegemea uchunguzi mmoja wa “wataalamu” ambao unachambua tafsiri hii ya kisasa ya Biblia ya Kirusi.

Mahakimu watatu wa mahakama ya mkoa walitambua kwamba mambo yaliyozungumziwa na “wataalamu” waliofanya uchunguzi kuhusu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya yalikuwa yakipingana na waliwaita mahakamani ili kuwauliza maswali. Wakati hakimu Larisa Gorbatova aliyekuwa akiendesha kesi alipomuuliza Bi. Kryukova, aliyekuwa kiongozi wa uchunguzi huo, ikiwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni Biblia; Bi. Kryukova alijibu kwamba si Biblia “kwa sababu hailingani na maoni ya Ukristo wa Othodoksi.” Wakili wa upande wa utetezi alipomuuliza anukuu andiko hata moja linaloonyesha dalili za msimamo mkali, Bi. Kryukova hakuweza kujibu swali hilo. Hatimaye, Hakimu Gorbatova alimuuliza Bi. Kryukova ni nini kilichofanya waseme kwamba tafsiri hiyo ya Biblia ina msimamo mkali, lakini alikataa kujibu akidai kwamba hilo lilikuwa “swali la kisheria.”

Wakili mmoja wa upande wa utetezi alipouliza kuhusu kigezo kinachotumiwa ili kutambua ikiwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni Biblia, Bi. Kryukova alisema kwamba ilipaswa kuwa na alama iliyosema “kwa baraka za askofu mkuu” au ifanane neno kwa neno na tafsiri ambayo ina maelezo hayo. Kisha Bi. Kryukova aliulizwa kwa nini uchunguzi wa wataalamu ulifikia mkataa kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya “si tafsiri inayofaa.” Hakuna “mtaalamu” yeyote ambaye aliweza kueleza sababu kwa ufasaha, na mahakama ilimaliza kuwauliza maswali “wataalamu” hao.

Kisha wakili wa Mashahidi aliomba mahakama ikubali uthibitisho unaoonyesha “wataalamu” walikuwa na upendeleo kwa kuonyesha kwamba uchunguzi wao ulitegemea kwa kiwango kikubwa habari kutoka katika Wikipedia na kwa mwanafunzi wa seminari ya Othodoksi. Hakimu alikubali uthibitisho huo utolewe lakini alikataa ombi la kuwataka wataalamu wa kweli wachunguze Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na kisha kesi ianze upya.

Kusudi la Shambulizi Hili la Biblia Ni Nini?

Mwishoni mwa mjadala, wakili wa Mashahidi aliuliza mahakama swali hili: “Ofisi ya mwendesha-mashtaka ina kusudi gani la kisheria? Inataka kutimiza nini? Je, mamia ya maelfu ya raia wanaozungumza Kirusi ambao wanasoma Biblia hii wazichome? Au ikiwa hawatataka kuzichoma, je, watashtakiwa kwa makosa ya uhalifu?”

Mashahidi wengi wa Yehova nchini Urusi hawana imani kwa sababu ya matendo yasiyo ya haki yanayofanywa na wenye mamlaka wanapotekeleza maamuzi ya wakati uliopita ya kutangazwa kwa machapisho ya Mashahidi kuwa yenye “msimamo mkali.” Sheria ya Urusi ya msimamo mkali inakataza kusambaza machapisho au kuyahifadhi kwa ajili ya kusudi la kusambaza, wenye mamlaka nchini Urusi wamekiuka kwa njia kubwa sheria hiyo. Wamepekua nyumba za Mashahidi na kumfungulia kesi mtu wanayemkuta na machapisho hata machache ambayo ameyatunza kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Isitoshe, wenye mamlaka wamepandikiza nakala chache za machapisho yaliyopigwa marufuku katika majengo ya ibada ya Mashahidi katika jitihada zao za kutokeza uthibitisho wa uwongo. Kisha, wanatumia machapisho “waliyogundua” kama msingi wa kupiga marufuku mashirika ya kisheria ya Mashahidi na hata kuwafungulia Mashahidi mashtaka ya uhalifu.

Je, nyumba za Mashahidi zitaendelea kupekuliwa kwa jeuri? Je, watafunguliwa kesi za uhalifu kwa sababu tu ya kuwa na nakala za kibinafsi za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya? Hatujui kikamili jinsi wenye mamlaka nchini Urusi watakavyotumia uamuzi huu kama silaha nyingine ya kukandamiza uhuru wa ibada wa Mashahidi.