Hamia kwenye habari

MEI 29, 2017
URUSI

Polisi wa Urusi Wavamia Ibada Jijini Oryol na Kumweka Mahabusu Raia wa Denmark

Polisi wa Urusi Wavamia Ibada Jijini Oryol na Kumweka Mahabusu Raia wa Denmark

Mei 25, 2017, maofisa wa polisi wenye silaha na wawakilishi wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) walivuruga mkutano wa kidini uliokuwa ukifanywa kwa amani na Mashahidi wa Yehova jijini Oryol, Russia. Wenye mamlaka walitangaza kwamba watawafungulia kesi ya uhalifu Mashahidi kwa madai ya kuendelea kufanya utendaji wa tengenezo lenye msimamo mkali. Serikali ililifunga Shirika la Kidini la Oryol (LRO) kwa mashtaka ya kujihusisha na msimamo mkali mnamo Juni 14, 2016. Isitoshe, wenye mamlaka walichukua rekodi za kibinafsi za kila mtu aliyehudhuria mkutano huo wa kidini, walipora vifaa vyao vya kielektroniki, na baadaye walipekua nyumba ya kila Shahidi jijini Oryol.

Wenye mamlaka waliwachukua wanaume wa kutaniko la Oryol na kuwapeleka kwenye ofisi za FSB na wamemweka mahabusu mwanamume raia wa Denmark anayeitwa Dennis Christensen, ambaye ni mzee wa kutaniko. Mwendesha mashtaka alituma maombi ya dharura kwenda Mahakama ya Wilaya ya Sovietskiy kumwomba Bw. Christensen aendelee kuwekwa mahabusu ili kuipa FSB wakati wa kutosha wa kutafuta uthibitisho na mashahidi wa kesi ili kuanzisha kesi. Hakimu Svetlana Naumova alikubali maombi hayo, akaamuru Bw. Christensen aendelee kuwa mahabusu kwa miezi miwili. Malalamiko dhidi ya amri hiyo yatapelekwa leo. Ikiwa atapatikana na hatia, anaweza kufungwa kwa miaka sita hadi kumi gerezani chini ya Sheria ya 282.2, sehemu ya 1, ya Makosa ya Uhalifu.

Kutaniko la Mashahidi wa Yehova jijini Oryol walifanya ibada yao kama kikundi cha waabudu—na si kama kikundi cha shirika la kisheria. Tendo hilo la wenye mamlaka wa Urusi linaonyesha kwamba wanalenga ibada ya Mashahidi na si muundo wao wa Kisheria (LROs). Jambo hilo ni sawa na lile lililotukia katika jiji la Taganrog, ambapo wenye mamlaka walifunga LRO kwanza na kisha kuwafungulia mashtaka ya msimamo mkali Mashahidi 16 kwa sababu waliendelea kukusanyika kwa amani kwa ajili ya ibada. Mnamo Novemba 2015, Mashahidi wote 16 walikamatwa lakini hukumu zao na faini walizotozwa zilifutwa. Kesi yao inachunguzwa upya na Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.