Hamia kwenye habari

DESEMBA 19, 2016
URUSI

Mashahidi wa Yehova Watafuta Haki Kwenye Rufani Yao Dhidi ya Onyo

Mashahidi wa Yehova Watafuta Haki Kwenye Rufani Yao Dhidi ya Onyo

Mahakama ya Jiji la Moscow imepanga kusikiliza rufani ya Mashahidi wa Yehova nchini Urusi ya kutaka kujua uhalali wa onyo lililotolewa dhidi ya Kituo chao cha Usimamizi. Januari 16, 2017, saa 5:10 asubuhi kulingana na Kipimo cha Wakati cha Moscow, mahakama itasikiliza rufani hiyo na inawezekana itatoa maamuzi siku hiyohiyo.

Mashahidi wanataka kuthibitisha kwamba mashtaka ya “utendaji wenye msimamo mkali” yanategemea ushahidi wa uwongo na maelezo ya uwongo ambayo yamepangwa na wenye mamlaka ili kuifanya ibada inayofanywa kwa unyoofu ionekane kuwa shughuli ya uhalifu. Katika kesi iliyosikilizwa Oktoba 12, 2016, Hakimu M. S. Moskalenko wa Mahakama ya Wilaya ya Tverskoy ya jijini Moscow hakuruhusu ushahidi au video zinazoonyesha matendo yasiyo ya haki ya baadhi ya wenye mamlaka zitolewe.

Mwanasheria wa kimataifa wa haki za kibinadamu James Andrik, alisema hivi: “Vyovyote vile, kusikilizwa kwa rufani hii ni muhimu sana. Ikiwa Mahakama ya Jiji la Moscow itatupilia mbali rufani hiyo, Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka Mkuu itaweza kutenda kulingana na tishio lake dhidi ya Kituo cha Usimamizi. Itaweza kukifunga Kituo cha Usimamizi na kuwatendea kwa njia mbaya zaidi washiriki wa dini ya Mashahidi wa Yehova na kupiga marufuku ibada yao katika nchi nzima ya Urusi. Ikiwa kwa upande mwingine, mahakama itaunga mkono rufani hiyo, haki itakuwa imetekelezwa.”