Hamia kwenye habari

Polisi wa Urusi wakiingia ndani ya Jumba la Ufalme la Nezlobnaya kupitia lango walilovunja

JANUARI 12, 2017
URUSI

Shambulio la Muda Mrefu Dhidi ya Uhuru wa Ibada Nchini Urusi Laongezeka

Shambulio la Muda Mrefu Dhidi ya Uhuru wa Ibada Nchini Urusi Laongezeka

Kuanzia Januari 16, 2017, kwa mara nyingine tena Mashahidi wa Yehova nchini Urusi watatoa ombi la kupinga vizuizi dhidi ya uhuru wa ibada ambavyo vimeongezeka katika miaka kumi iliyopita. Wataiomba Mahakama ya Jiji la Moscow kwa mujibu wa sheria ibatilishe onyo lililotolewa dhidi ya makao makuu kwa kuwa halikuwa na msingi wa kisheria wala halikuzingatia sheria. Onyo hilo lililotolewa Machi 2, 2016, na Kaimu Mwendesha-Mashtaka Mkuu V. Ya. Grin, lilitishia kufunga makao makuu ya kitaifa ya Mashahidi ikiwa kutakuwa na uthibitisho mpya wa Mashahidi kujihusisha na “shughuli zenye msimamo mkali” katika kipindi cha mwaka mmoja.

Kuwatafuta Wenye Msimamo Mkali

Waendesha-mashtaka nchini Urusi wanatumia vibaya Sheria ya Shirikisho ya Kupambana na Shughuli Zenye Msimamo Mkali kama msingi wa kuwashtaki Mashahidi wa Yehova kwamba wana msimamo mkali. Baada ya sheria hiyo kurekebishwa mwaka wa 2006, maana ya msimamo mkali haikuhusisha tu kuchochea matendo ya vurugu, badala yake ilimaanisha “kuchochea . . . mgawanyiko wa kidini.” Kupanuliwa kwa maana ya sheria hiyo kunawaruhusu wenye mamlaka kusema kwamba fundisho lolote ambalo linapingana na mafundisho ya dini ambayo watu wameyazoea au linalowafundisha watu kitu tofauti ni kuchochea uadui wa kidini. Gregory Allen, mwanasheria anayesaidia kutetea uhuru wa ibada wa Mashahidi nchini Urusi alisema hivi: “Wenye mamlaka wanatumia maana hii inayonyumbulika kuwaona kuwa na “msimamo mkali” washiriki wote wa dini ambao imani zao hazifanani na za dini za zinazojulikana sana.”

Kuwawinda watu wenye “msimamo mkali” katika baadhi ya dini zenye watu wachache kulianza Januari 2007 baada ya ofisi zote za waendesha-mashtaka nchini Urusi kupokea barua kutoka kwa V. Ya. Grin ambaye ni Kaimu Mwendesha-Mashtaka Mkuu wa Shirikisho la Urusi. Barua hiyo ya kuwachochea wafanye uchunguzi ilifanya kuwe na upekuzi zaidi ya mara 100 kwenye mashirika ya kidini ya Mashahidi wa Yehova kabla ya mwaka huo kwisha.

Kutokeza “Uthibitisho” wa Kwanza

Upekuzi mmoja ulifanyika kwenye jiji la Taganrog, lililoko kwenye pwani ya Bahari Nyeusi. Upekuzi huo ulikuwa chanzo cha karibu mashtaka yote ya msimamo mkali waliyoshtakiwa Mashahidi wa Yehova nchini Urusi. Kufikia Oktoba 2007, Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka ya Mkoa wa Rostov ilikamilisha uchunguzi wake na kutangaza onyo dhidi ya Local Religious Organization (LRO), yaani, Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova la Taganrog na mwaka uliofuata ilifungua mashtaka ya kulifunga shirika hilo. Hata hivyo, Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka ilikosa ushahidi wa kutegemeza madai yao na kuiomba Mahakama ya Mkoa ya Rostov iagize “uchunguzi wa kitaalamu” ufanywe kuchunguza machapisho ya dini ya Mashahidi wa Yehova.

Mbali tu na kuagiza “uchunguzi wa kitaalamu” ufanywe bila ridhaa ya Mashahidi, mahakama hiyo pia ilikataa maombi ya Mashahidi kwamba uchunguzi huru ufanywe. Katika ripoti yao, wataalamu hao waliotumwa na mahakama wote kwa pamoja walifikia uamuzi kwamba machapisho ya dini ya Mashahidi wa Yehova hayachochei matendo ya uadui. Hata hivyo, mahakama ilikazia uangalifu maoni ya wataalamu hao kwamba mazungumzo ya kidini katika machapisho ya Mashahidi yana “uwezo wa kushushia heshima” dini nyingine.

Septemba 11, 2009, Mahakama ya Mkoa ya Rostov, ilipanua maana ya “msimamo mkali” na ikatangaza machapisho 34 ya Mashahidi kuwa na “msimamo mkali” na yaliwekwa kwenye Orodha ya Serikali ya Habari Zinazowachochea Watu Kuwa na Msimamo Mkali (FLEM). Mahakama pia ilitangaza kwamba shirika la LRO la Taganrog “lina msimamo mkali” na kuagiza wenye mamlaka wa shirikisho walifunge, kupiga marufuku utendaji wake, waliweke kwenye orodha ya mashirika yenye msimamo mkali, wakamate machapisho yao ya kidini, na kutaifisha mali zake zimilikiwe na Shirikisho la Urusi. Desemba 8, 2009, Mahakama Kuu ya Shirikisho la Urusi iliunga mkono uamuzi huo, na kuufanya huo uwe uamuzi wa mwisho. a

Kufikia mwanzoni mwa mwaka wa 2016, mahakama hiyo ilikuwa imetangaza machapisho 88 ya kidini kuwa yana “msimamo mkali” na kufunga mashirika matatu ya kidini. Mashirika mengine 18 ya kidini yalikuwa yakichunguzwa. Isitoshe, wenye mamlaka walipiga marufuku na kufunga tovuti rasmi ya Mashahidi wa Yehova ya jw.org, walizuia kuingizwa kwa machapisho na kuifanyia Biblia uchunguzi wa makini kuona ikiwa ni chapisho lenye “msimamo mkali.”

“Uthibitisho” Uliotolewa Ili Kushambulia Makao Makuu

Machi 2016, Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka Mkuu ilitumia “uthibitisho” huo uliokusanywa kutegemeza onyo lake dhidi ya makao makuu ya Mashahidi, ambayo yanajulikana kama Kituo cha Usimamizi cha Mashahidi wa Yehova nchini Urusi, kilicho karibu na St. Petersburg. Mwendesha-mashtaka alihusianisha Kituo cha Usimamizi na machapisho ya kidini yaliyopigwa marufuku na pia na mashirika ya kidini (LRO) ambayo yanachunguzwa au kufungwa, akisema hivi: “Dalili za msimamo mkali zinaendelea kugunduliwa katika utendaji wa matawi ya Kituo cha Usimamizi.”

Muda mfupi baada ya kupokea onyo hilo, Mashahidi walimwomba Mwendesha-Mashtaka Mkuu wa Shirikisho la Urusi, Yuriy Yakovlevich Chayka, abatilishe onyo hilo. Badala ya kulibatilisha, aliliunga mkono na kusema kwamba “hoja kuhusu uthibitisho wa uwongo na matendo mengine ya ukiukwaji wa sheria yaliyotokea wakati wa upekuzi ambayo yalifanywa na wenye mamlaka sio msingi wa kubatilisha onyo hilo, kwa sababu onyo linatokana na maamuzi wa mahakama.” Bw. Allen alisema hivi: “Ni wazi Mwendesha-Mashtaka Mkuu anaamini kwamba mahakama za Urusi zinaweza kuhalalisha uthibitisho wowote wa uwongo unaotolewa na maofisa wa sheria wasio wanyoofu. Ninakumbuka uamuzi wa mahakama ya Moscow ambao uliwapiga marufuku isivyo haki Mashahidi wa Yehova katika jiji hilo na baadaye ulibatilishwa na Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.” b

Baada ya Mwendesha-Mashtaka Mkuu kutoa uamuzi wake, Mashahidi walifungua kesi kupinga onyo hilo kwenye Mahakama ya Wilaya ya Tverskoy jijini Moscow. Oktoba 12, 2016, Hakimu M. S. Moskalenko alikataa kuwaruhusu mashahidi na wataalamu kutoa ushahidi wakati wa kesi, na alitupilia mbali rufani.

Kutofanikiwa kwa jitihada hizo kunamaanisha onyo linaendelea. Kituo cha Usimamizi kinakabili hatari kubwa ya kufungwa ikiwa Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka Mkuu itafaulu kuishawishi mahakama kwamba (1) mashirika ya kidini ya Mashahidi (LRO) yamekuwa yakiendelea kukiuka sheria ya kuchochea msimamo mkali wa kidini, au (2) wenye mamlaka wamepata “mambo mapya ambayo yanathibitisha kuwapo kwa dalili za utendaji unaochochea msimamo mkali wa kidini” katika shughuli za Mashahidi kwa kipindi cha mwaka mmoja baada ya onyo kutolewa.

Kuongezeka kwa “Uthibitisho Mpya” wa Uwongo

Tangu Machi 2, 2016 onyo hilo lilipotolewa, wenye mamlaka nchini Urusi wameendelea kuongeza jitihada za kubuni “uthibitisho mpya.” Kuna matukio 35 yaliyorekodiwa (kati ya zaidi ya matukio 60 tangu 2012) ambayo wenye mamlaka walibuni “makosa ya uhalifu” kwa kupandikiza machapisho ya kidini ambayo Mashahidi wa Yehova waliacha kuyatumia. Mara nyingi upekuzi wa kutafuta “uthibitisho” unaambatana na vitendo vya jeuri vinavyofanywa na polisi na vikosi maalumu vya polisi.

  • Julai 28, 2016, Mashahidi wa Yehova walivamiwa mara mbili na polisi katika Jamhuri ya Karelia. Huko Petrozavodsk, kikosi chenye silaha, chenye wanaume walioziba nyuso zao kutoka katika Kikosi Maalumu cha Polisi walifika kwenye Jumba la Ufalme na kuvuruga mkutano wa ibada. Polisi walipandikiza nakala tano za kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kwenye jengo hilo na baadaye wakadai “walivipata” walipokuwa wakipekua. Maofisa hao hawakuwaonyesha Mashahidi kibali cha mahakama kilichowaruhusu kufanya uvamizi huo na kupekua mali zilizomo. Huko Kostomuksha, maofisa kutoka Idara ya Kitaifa ya Usalama (FSB) na Kituo cha Kupambana na Shughuli za Kidini Zenye Msimamo Mkali walivuruga mkutano wa kidini. Wakati wa upekuzi katika Jumba la Ufalme, walidai kwamba “walipata” machapisho matatu ya Mashahidi yaliyo kwenye orodha ya FLEM.

  • Agosti 20, 2016, maofisa wa kusimamia sheria walivuruga mkutano wa Mashahidi wa Yehova katika jiji la Mayskiy, Jamhuri ya Kabardino-Balkaria. Baada ya kuwatoa watu wote kwa lazima nje ya Jumba la Ufalme, maofisa walidai kwamba “walipata” chapisho walilopandikiza ambalo ni mojawapo ya machapisho yaliyopigwa marufuku ndani ya Jumba. Wenye mamlaka hawakutoa hati au karatasi yoyote yenye kibali cha kuwaruhusu kufanya uvamizi huo.

  • Septemba 20, 2016, kikosi chenye silaha, kikiwa na wanaume walioziba nyuso zao kutoka katika Kikosi Maalumu cha Polisi walifika asubuhi mapema kwenye Jumba la Ufalme lililoko Nezlobnaya, Eneo la Stavropol. Ili kuingia kwenye jengo hilo, walivunja milango kisha wakapandikiza machapisho kadhaa ya Mashahidi yaliyo kwenye orodha ya FLEM. Maofisa walidai kwamba “walipata” machapisho hayo walipokuwa wakipekua baada ya kutokea kwa uvamizi huo.

Polisi wanaonekana wakipandikiza machapisho ndani ya kabati lisilo na chapisho lolote kwenye Jumba la Ufalme la Nezlobnaya, baadaye mkaguzi alidai “aliyagundua” alipokuwa akipekua

Hatua za Kuwashtaki Mashahidi

Hatua za kuwashtaki Mashahidi wa Yehova kwa madai ya msimamo mkali kwa kawaida zilihusisha mambo kama yale yaliyotokea kwenye shirika la kidini la Mashahidi (LRO) katika jiji la Birobidzhan:

  1. Hatua ya 1: Maofisa wa sheria wanaenda kwenye jengo la ibada la Mashahidi na kupandikiza machapisho yaliyo kwenye orodha ya FLEM.

    Polisi na maofisa wa FSB walivuruga mkutano wa kidini wa Mashahidi wa Yehova, wakidai kwamba mkutano huo haukuwa halali kisheria, kisha wanatangaza kufanya upekuzi wa kutafuta “vitabu na habari zinazowachochea watu kuwa na msimamo mkali wa kidini.”

  2. Hatua ya 2: Maofisa wanapekua jengo na kudai “wamegundua” machapisho yaliyopigwa marufuku.

    Maofisa walidai kwamba “walipata” machapisho 12 yaliyo kwenye orodha ya FLEM. Baadaye Mashahidi walitambua kwamba mtu fulani mgeni alikuja kwenye jengo hilo kabla ya mkutano na kuficha “uthibitisho” huo.

  3. Hatua ya 3: Mwendesha-mashtaka anafungua kesi dhidi ya shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova (LRO) au mwenyekiti wake kwa kupinga mamlaka na kusambaza machapisho yanayochochea msimamo mkali, kisha anawatoza faini.

    Mahakama ya wilaya ilimhukumu mwenyekiti wa LRO kuwa na hatia ya kupinga mamlaka na kumtoza faini ya dola 66.88 za Marekani.

  4. Hatua ya 4: Mwendesha-mashtaka anatoa onyo kwa LRO kwamba lisirudie tena kukiuka sheria kwa kipindi cha miezi 12.

    Mwendesha-mashtaka alitoa onyo kwamba kujihusisha katika “utendaji unaochochea msimamo mkali wa kidini” ni kosa.

  5. Hatua ya 5: Muda fulani baadaye, maofisa wa sheria wanarudi tena kwenye jengo la ibada, na kupandikiza tena machapisho yaliyopigwa marufuku ndani ya majengo ya ibada, kisha wanadai “wameyapata” wakati wa upekuzi.

    Maofisa walikatiza mkutano wa dini ili kufanya upekuzi ndani ya jengo kutafuta “machapisho yanayochochea msimamo mkali.” Hata hivyo, Mashahidi waliona chapisho lililopandikizwa mapema kabla ya kupekuliwa na kuliondoa, kwa hiyo, jaribio la kupata uthibitisho wa uwongo la Oktoba 2015 halikufanikiwa. Lakini Januari 21, 2016, maofisa hao walijitayarisha vizuri. Vikosi maalumu vya polisi, polisi wa kawaida, na maofisa wa FSB walikatisha tena mkutano wa kidini wa Mashahidi wa Yehova na kutangaza wanafanya upekuzi ndani ya jengo hilo kutafuta “machapisho yanayochochea msimamo mkali wa kidini.” Shahidi mmoja wa Yehova aliyehudhuria alimwona ofisa mmoja akiwa ameshika mkononi kifurushi cha machapisho. Ofisa mwingine alitafuta katika eneo ambalo tayari lilikuwa limepekuliwa, lakini mara hii alifanya hivyo bila kuwahusisha Mashahidi, na akadai kwamba “amepata” kifurushi cha machapisho.

  6. Hatua ya 6: Kwa kutegemea uthibitisho huo mpya wa madai ya utendaji unaochochea msimamo mkali, ofisi ya mwendesha-mashtaka au Wizara ya Sheria inafungua kesi ya kudai LRO lifungwe.

    Mahakama ya wilaya ilitangaza kwamba mwenyekiti wa LRO alikuwa na hatia ya kukiuka sheria na akatozwa faini ya dola 50.16 za Marekani. Oktoba 3, 2016, mahakama ya mkoa ilisema kwamba “uthibitisho mpya wa dalili ya utendaji unaochochea msimamo mkali katika shughuli za LRO umepatikana” na akatangaza LRO la Birobidzhan “linachochea msimamo mkali wa kidini,” akapiga marufuku utendaji wake, na kuamuru lifungwe.

Ikiwa ni hatua ya mwisho, Mahakama Kuu ya Shirikisho la Urusi imeunga mkono maamuzi ya mahakama za chini za kufunga LRO za Mashahidi kwa kudai kuwa ni “mashirika yanayochochea msimamo mkali wa kidini.” Hivi karibuni mashirika ya Belgorod, Stariy Oskol, Elista, na Orel yamefungwa. Rufani ya Mashahidi kwa ajili ya shirika la Birobidzhan inasubiri kusikilizwa na Mahakama Kuu.

Hilo Linamaanisha Nini? Hali Hiyo Itaishia Wapi?

Vasiliy Kalin, mwakilishi wa Kituo cha Usimamizi, alikumbuka mateso waliyokabili familia yao ilipohamishwa kupelekwa Siberia katika kipindi cha Sovieti: “Nilipokuwa nikikua, wenye mamlaka wangeweza kuingia kwenye nyumba za Mashahidi wakati wowote na kufanya upekuzi wakitafuta machapisho ya kidini. Hata hivyo, hawakuwahi kupandikiza machapisho kwenye nyumba zetu na kujifanya eti wameyapata baadaye. Mbinu hii mpya ya hila inayofanywa na maofisa wa sheria ni uthibitisho kwamba bado hawawezi kupata msingi wowote wa kuwashtaki Mashahidi wa Yehova kwamba wanaendeleza utendaji unaopingana na sheria.”

Januari 16, 2017, Mahakama ya Jiji la Moscow inatarajia kusikiliza rufani ya Mashahidi wa Yehova ya kupinga onyo la Mwendesha-Mashtaka Mkuu na kutoa uamuzi wake. Je, uamuzi utaonyesha kwamba Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka Mkuu haikuwa na msingi wowote wa kukishutumu Kituo cha Usimamizi cha Mashahidi wa Yehova kwa utendaji unaochochea msimamo mkali wa kidini na kubatilisha onyo hilo? Mashahidi wa Yehova na watu wote wanaothamini haki za kibinadamu nchini Urusi na ulimwenguni pote wanatumaini mahakama hiyo itafanya hivyo.

a Mahakama Kuu ya Shirikisho la Urusi ilianzisha wimbi kubwa la matatizo kwa Mashahidi. Ripoti za matukio 1,126 yaliyotokea kati ya Desemba 8, 2009, na Aprili 26, 2012, yanaonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova walitendewa vibaya na kushambuliwa walipokuwa katika utendaji wao wa kidini, waliwekwa vizuizini na kupekuliwa na maofisa wa sheria wa Urusi, na majengo yao ya ibada yakavamiwa.

b Mfuatano wa matukio ya kihalifu na kiraia yaliyokusudiwa kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova jijini Moscow yalianza mwaka wa 1995 lakini mbinu hiyo haikufaulu kwa sababu ya kukosa uthibitisho. Hata hivyo, uamuzi uliofanywa Machi 2004 na Mahakama ya Wilaya ya Golovinskiy ilitumia “uchunguzi wa wataalamu” kama msingi wa kufunga Shirika la Kisheria la Mashahidi jijini Moscow na kutangaza kupigwa marufuku kwa utendaji wake. Katika uamuzi uliotolewa Juni 10, 2010, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ilitambua kwamba Shirikisho la Urusi limeingilia kinyume cha sheria haki ya uhuru wa ibada na haki za shirika la Mashahidi wa Yehova na mahakama hiyo ikaamuru serikali ya Urusi irekebishe madhara makubwa yaliyotokana na matendo yake.