Hamia kwenye habari

JUNI 2, 2014
URUSI

Mashahidi wa Yehova Waendelea Kushtakiwa Jijini Taganrog, Urusi

Mashahidi wa Yehova Waendelea Kushtakiwa Jijini Taganrog, Urusi

Mashtaka ya uhalifu dhidi ya Mashahidi 16 wa Yehova katika Mahakama ya Jiji la Taganrog yameendelea kupamba moto kufikia mwezi wa Mei 2014. Hiyo ndiyo kesi pekee nchini Urusi ambapo raia wake wanashinikizwa waikane imani yao la sivyo washtakiwe kwa makosa ya jinai. Mmoja wa washtakiwa hao alisema: “Wanataka niwe kama wengine, hawataki niwe tofauti. Hawataki nizungumze na watu kuhusu Biblia. Sijui mwisho wa mambo haya ni nini.”

Wenye mamlaka nchini Urusi wanaitumia vibaya Sheria ya Kupambana na Shughuli Zenye Msimamo Mkali. Wanaitumia vibaya dhidi ya Mashahidi wa Yehova ambapo tangu mwaka wa 2009 wenye mamlaka wamekuwa wakiwasumbua sana. Victor Zhenkov, wakili wa Mashahidi, anasema: “Nimechunguza matukio ya miaka ya hivi karibuni kuhusiana na mashtaka ambayo Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakikabili na nimekata kauli kwamba mashirika ya kutekeleza sheria yamekusudia hasa kuwalenga Mashahidi wa Yehova.” Wenye mamlaka jijini Taganrog wameongeza jitihada za kuwakandamiza Mashahidi na kuwatendea kana kwamba wamepigwa marufuku katika eneo hilo, licha ya kwamba Mashahidi wa Yehova walisajiliwa katika Shirikisho la Urusi mwaka wa 1992. Bila shaka nia ya wenye mamlaka hao iko wazi. Shahidi mwingine aliyeshtakiwa alisimulia kisa chake akisema: “Mpelelezi aliniambia waziwazi ofisini mwake: ‘Tia sahihi karatasi hii kuonyesha unakana kwamba wewe si Shahidi wa Yehova, ukifanya hivyo tutafuta kesi yako na kukuachilia huru—uende kokote unakotaka.’”

Ikitegemea uamuzi wa mahakama, Mashahidi hao 16 wanaweza kutozwa faini, wanaweza kuhukumiwa wafanye kazi za kulazimishwa, au kufungwa gerezani. Wakipatikana na hatia, basi uhuru wa kidini kotekote nchini Urusi utakuwa hatarini. Mashahidi wote wa Yehova nchini Urusi watakabili tisho la kushtakiwa kama wahalifu kwa sababu ya kuendeleza shughuli zao za kidini zenye amani. Alyona Borodina, wakili mwingine wa Mashahidi wa Yehova, anasema: “Mashahidi wanakabili tatizo la kudhulumiwa mara kwa mara na wenye mamlaka nchini. Machapisho yao yamewekwa kwenye orodha ya vitabu vyenye msimamo mkali sana wa kidini. Mahakama inapofikia uamuzi kwamba kitabu fulani kina msimamo mkali sana wa kidini, kitabu hicho huharibiwa. Mwandishi mmoja alisema hivi: ‘Ikiwa wanachoma vitabu, basi inaonekana kwamba hatimaye watawachoma wanadamu.’ Uhuru wa kidini uko hatarini.”

Hakimu anatarajiwa kutoa uamuzi wake wa mwisho mwezi wa Juni mwaka wa 2014. Mashahidi wa Yehova kote duniani pamoja na wale wote wanaopenda uhuru wa kidini wanataka sana kujua ni uamuzi gani utakaofikiwa.