Hamia kwenye habari

MEI 30, 2019
UZBEKISTAN

Ndugu Nchini Uzbekistani Waadhimisha Ukumbusho wa Kifo cha Kristo Hadharani Nchini Kote

Ndugu Nchini Uzbekistani Waadhimisha Ukumbusho wa Kifo cha Kristo Hadharani Nchini Kote

Aprili 19, 2019, kwa mara ya kwanza katika miaka ya karibuni, ndugu zetu kotekote nchini Uzbekistani waliadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo hadharani.

Mashahidi wa Yehova wameandikishwa rasmi katika jiji la Chirchik pekee, lililo karibu na Tashkent, nchini Uzibekistani. Katika miaka ya karibuni, ndugu zetu wanaoishi nje ya eneo la Chirchik waliadhimisha Ukumbusho kisiri ili kuepuka uwezekano wa kuingiliwa na polisi. Mwaka huu, ndugu waliwajulisha maofisa wa polisi kuhusu Ukumbusho na kuwaalika. Maofisa wa polisi waliitikia vizuri na hata walichukua hatua za kuhakikisha kwamba watu waliohudhuria walikuwa salama. Katika maeneo fulani maofisa wa polisi walihudhuria programu hiyo.

Ndugu Mark Sanderson wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba katika Jumba la Ufalme la Chirchik, kama picha kubwa inavyoonyesha. Programu hiyo ilitafsiriwa katika Kirusi. Watu 781 walihudhuria. Baadaye jioni hiyo, kulikuwa na maadhimisho mawili ya Ukumbusho katika majumba hayo ya Ufalme.

Wakati wa ziara yake, Ndugu Sanderson, aliyeandamana na Paul Gillies kutoka makao makuu na ndugu wawili kutoka Asia ya Kati, walikutana na maofisa wa cheo cha juu katika Wizara ya Haki na Kituo cha Kitaifa cha Haki za Kibinadamu. Wakati wa mikutano, ndugu zetu waliruhusiwa kutoa habari sahihi kuhusu imani yetu na tengenezo letu. Inatumainiwa kwamba maofisa wenye habari sahihi wataunga mkono kuandikishwa katika maeneo yaliyo nje ya Chirchik, jambo ambalo litawasaidia ndugu kupata majengo yanayofaa kwa ajili ya ibada.

Ndugu Mark Sanderson pamoja na ndugu walioenda kutuwakilisha wakiwa nje ya Wizara ya Haki ya Jamhuri ya Uzbekistani

Kuadhimisha Ukumbusho hadharani na kukutana kwa heshima na maofisa ni jambo linalopendeza nchini Uzbekistani. Kwa miezi sita iliyopita, hakukuwa na uvamizi, kutozwa faini, au kukamatwa kwa Mashahidi wa Yehova. Na mwaka mmoja hivi uliopita, yaani, Mei 14, 2018, Bw. Javlon Vakhabov, balozi wa Uzbekistani nchini Marekani, alisema hadharani kwamba bunge litafanya kazi ili kubadili sheria na kuifanya iwe rahisi kwa Mashahidi wa Yehova kuandikishwa kisheria.

Tunamtegemea Yehova abariki jitihada za ndugu zetu nchini Uzbekistani wanapoendelea kuishi “kwa amani na utulivu na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.”—1 Timotheo 2:2.